Back Index Next

Mimi naamini kuwa, watu hawa hawasemi kutoka katika nafsi zao, bali wao wanatumwa na maadui wa Uislamu wanaoupiga vita Uislamu kupitia nyuma ya pazia. Lengo lao ni kuiangamiza maana nzima ya Uislamu, na kisha kuwapotosha wasichana na wavulana wa Kiislamu. Jambo la kusikitisha na kuhuzunisha ni kwamba, kauli kama hizi zimekuwa zikirudiwa mara kwa mara na katika nyakati tofauti, ima ndani ya magazeti na majarida na au katika mikutano mbali mbali. Kuna lugha nyingi zinazotumika katika kampeni hii ikiwemo lugha ya Kiarabu ambayo inawaunganisha Waislamu wa dunia nzima kama lugha ya dini yao.

Yote haya ndugu Waislamu, ni majaribio ya makusudi kabisa yenye lengo la kuivuruga na kuipoteza jamii takatifu ya Kiislamu. Kinachotakiwa kwa Waislamu wenye uchungu na dini yao ni kunyanyuka na kuyapinga magazeti haya kwa kuwa yenyewe ndiyo sauti ya vita vya kuutokomeza Uislamu na Waislamu. Kwa hakika wajibu wa kisheria unamtaka kila Mwislamu kupambana na majaribio haya hatari kwa uwezo wake wote kinadharia na kivitendo, hadi lengo la maadui hawa lisitimizwe katika nchi zetu tukufu za Kiislamu na jamii za Kiislamu popote zilipo duniani.

Kadhalika kukabiliana na maadui hawa dhidi ya njama zao za kutaka kugeuza nchi zetu kuwa ni mapori ya wanyama kufuatia mila zao wanazokusudia kuturithisha.Watu hawa madhalimu, katika nchi zao wamebadilika kutoka katika mila ya wanaadamu na wamekuwa na tabia za wanyama, kiasi kwamba mwanamke na mwanaume wanakidhi matamanio yao mabarabarani kama wafanyavyo wanyama bila kuwa na hisiya zozote za kuona haya wala kuogopa kwamba wao ni viumbe teule na watakatifu kwa kuumbwa kwao kama wanaadamu.

VIPI WAMEFAULU KUTUPOTOSHA?

Sasa tuangalie namna gani watu hawa wamefanikiwa kutupotosha, kwa kuwavua binti zetu na wake zetu mavazi ya Kiislamu. Pia ni kwa vipi wamefaulu kututeka kwa kupitia anuani ya kutetea uhuru wa mwanamke. Ili kupata ufumbuzi wa suala hili hatuna budi kufanya ziyara ya uchunguzi katika nchi za magharibi na kuiangalia jamii yao, na ni vema pia kufuatilia magazeti yao na majarida ili tuyaone mazingira mabaya wanayoishi wanawake wasio na Hijabu huko kwao. Kwa watu wa magharibi mambo hayaishii kwenye kukosa Hijabu na kutembea kichwa wazi na miundi nje basi. Bali hali yao inakwenda mbele zaidi kiasi kwamba kifua nacho huwa wazi, na wanawake hao kadhalika huvaa nguo nyepesi inayodhihirisha rangi ya mwili hadi kufikia kufanana na mtu aliye uchi kabisa.

Matokeo ya mavazi haya ni umalaya au kutekwa nyara na baadaye kubebeshwa mimba za haramu kisha kuingia katika kufanya mauaji pindi wanapotaka kuzitoa mimba hizo. Linalojitokeza hapa ni kudhulumu kiumbe hicho kinachotolewa kwa nguvu au muhusika kukumbwa na kifo wakati wa zoezi hilo. Hali hii ndiyo iliyoko kwenye nchi zinazoitwa zimeendelea. Nchi zetu za Kiislamu na Waislamu kwa jumla kwa sasa wanakabiliwa na tishio la hatari hii inayokuja kwa kasi ya ajabu kutoka kwenye hizo nchi za mashariki na magharibi. Kinachotakiwa kwa Waislamu ni kuwa na tahadhari kubwa na kuikabili kasi hii ya hatari inayokuja kutoka katika nchi hizo za mashariki na magharibi. Kwa hakika wameeneza uovu wao katika jamii yetu chini ya kivuli cha utaalamu na elimu. Idadi kubwa ya makosa ya jinai yanayotokea katika nchi zinazodaiwa kuwa zimeendelea ni mengi mno, ukilinganisha na matukio kama hayo yanayotokea katika nchi zetu za Kiislamu.

Tofauti hii ni kwa sababu Uislamu unahimiza na kutilia mkazo watu wawe na maadili mema, tabia nzuri na waepukane na kila tabia chafu. Pamoja na hali hii ambayo kwa kiasi fulani inaonesha tofauti baina ya nchi za Kiislamu na hizo za magharibi, Ni lazima kwa Waislamu kuchukua tahadhari, wasihadaike na hali waliyonayo, kwani hatari inakuja na shari zinaandaliwa dhidi yao, na ni wajibu wa kila Mwislamu kuwa na tahadhari. Yafuatayo ni baadhi ya mambo yanayotendeka katika nchi ambazo ndizo zinazoongoza katika kupiga vita utamaduni wa Kiislamu.

1. Nchini Uingereza peke yake karibu filamu 10 zinazohusu mambo machafu hukamilika kutengenezwa kila wiki na kutumwa nchi za nje. Kwa hali hii basi kila mwaka filamu zisizopungua 500 hutengenezwa nchini Uingereza na zote ni za kuonesha mambo ya aibu tupu na uchafu ambao jamii yetu inapotea na kuangamia kutokana na yaliyomo ndani ya filamu hizi.

2. Mwaka 1961 polisi wa Uingereza walijaribu kuwaangamiza wanawake wapatao laki moja, ambao kazi yao ilikuwa umalaya na machafu mengineyo, lakini baadaye walitangaza kushindwa kwa jaribio hilo.[29]

3. Mjini Rome kuna majumba yapatayo mia tano ya malaya, humo ndani mna maelfu ya wanawake ambao kazi yao ni kusubiri wanaume.[30]

Gazeti la “The Gurdian” liliandika kwamba takwimu za polisi zinaonesha kuwa, makosa ya jinai ya kubaka yanaongezeka mwaka hadi mwaka. Katika mji wa Washington peke yake kila baada ya dakika kumi na tano huwa kuna tukio la kubaka. Na katika mji mkuu wa Ungereza (London) yalitokea matukio 2095 ya kubaka wanawake na wasichana mwaka 1970 peke yake. Haya ni machache katika mengi ambayo tungeweza kukuorodheshea.

EWE DADA WA KIISLAMU

Ewe dada wa kiislamu nakuomba uyafanyie mazingatio baadhi ya mafunzo ya Kiislamu ambayo Mwenyezi Mungu Mtukufu amekupangia ili uweze kufanikiwa duniani na akhera. Mafunzo hayo ni mafunzo mema yatakayo kupandisha daraja ya ubora, imani, na utukufu. Na sina shaka kwamba utafanikiwa na kupata kheri nyingi mno, lakini sharti uyatumie na kushikamana nayo maishani mwako.

Hijabu kabla ya mambo mengine: Hijabu pekee ndiyo kinga yako ya kuaminika ambayo itakulinda kutokana na maovu na waovu, na ni hifadhi madhubuti dhidi ya kila aina ya uchafu na wahusikao na uchafu huo. Vazi la Hijabu ewe dada wa Kiislamu, ni ujumbe rasmi wa Mwenyezi Mungu kwako, basi mtii Mola wako na tekeleza amri yake. Hakika Hijabu ni kwa faida yako na umewekewa kwa ajili ya kulinda hadhi yako wewe mwenyewe. Dada mpendwa, Muumba wako ni mpole kwako naye anakwambia katika Qur-an,

“Na wala msioneshe mapambo yenu kama walivyokuwa wakionyesha mapambo yao wanawake wa zama za jahiliya.”Q. 33:33

Na anasema tena Muumba wako.

“Wanawake wateremshe (vizuri) shungi zao hadi vifuani mwao na wala wasioneshe mapambo yao.” 24:31

Maelekezo ya Mola wako ndiyo haya, ole wako ukiyapa mgongo utaangamia duniani na akhera.

Dada mpendwa, ufunguo bora wenye thamani kubwa utakaoweza kufungua milango ya dini yako, dunia yako na heshima yako umo ndani ya Hijabu, hebu jitahidi kufuata amri ya Mola wako ili uupate ufunguo huo. Pia fahamu kwamba uzuri wako, thamani yako na heshima yako vimo ndani ya Hijabu. Ole wako kama utaiacha Hijabu, basi uzuri wako na heshima yako vitaporomoka.

Ningependa pia ufahamu kwamba, njia ya wewe kupata radhi za Mwenyezi Mungu na kuingia peponi imo ndani ya Hijabu. Kwa hiyo radhi za Mola wako na pepo utavikosa iwapo utaitupa Hijabu. Kadhalika dada mpendwa fahamu kwamba, njia inayoelekea kwenye ghadhabu za Mwenyezi Mungu na motoni inapitia kwenye kuvua Hijabu na kutoitekeleza. Basi ole wako usijeanguka ndani ya kina kirefu cha moto wa Jahanam.

Imamu Ali (a.s.) amesema: “Mwanamke ni kama mmea mzuri wenye harufu nzuri, na wala siyo kama nyenzo.”Basi ni juu yako ewe dada ujifahamu thamani yako. Usiruhusu mwili wako na mapambo yako yachezewe na kila mtu, isipokuwa mumeo tu.[31]

Katika kumsifu mwanamke mchamungu, Bwana Mtume (s.a.w.w.) anasema; “Mwanamke mchamungu ni yule anayejihifadhi na kujisitiri mbele ya wanaume wengine, lakini huuacha wazi mwili wake anapokuwa faragha na mumewe, husikiliza ni kitu gani akitakacho32 mumewe, ni mtiifu kwa mumewe, na wakikaa faragha humpa akitakacho.” Dada yangu katika Uislamu, angalia sana usije ukawa mfano wa bidhaa zilizotandazwa sokoni, au bidhaa za dukani kila mmoja huangalia na kuzikamata kamata apendavyo.[32]

Usitumie vifaa vya kujirembesha na manukato ila unapokuwa nyumbani mwako na nduguzo wanaokuhusu kisheria. Tahadhari tena tahadhari sana na tabia ya kujirembesha kisha ukatoka barabarani, jambo hili ni hatari unaweza ukafanyiwa maovu, pia litakusababishia ghadhabu na laana za Mwenyezi Mungu. Bwana Mtume (s.a.w.w.) amesema:”Usijifananishe na wanaume katika mavazi na mambo mengine, bali bakia katika maisha na maumbile yako ya kike.”Bwana Mtume (s.a.w).w amesema: “Mwenyezi Mungu awalaani wanawake wanaojifananisha na wanaume (katika mavavi na mengineyo) na awalaani pia wanaume wanaojifananisha na wanawake.”[33] Ewe dada mpendwa, usipeane mkono na mwanamume asiye kuhusu, japo kuwa yeye ni miongoni mwa jamaa zako, kama watoto wa ami zako au watoto wa mjomba. Iwapo mwanaume atanyoosha mkono wake kwako mwambie; “Dini yangu na Mola wangu ananizuia kupeana nawe mkono.

Usimuogope mtu ikiwa atachukia au kukasirika kwani radhi ya Mwenyezi Mungu ni bora kuliko radhi za watu. Na kuogopa kukasirikiwa na Mwenyezi Mungu ni bora kuliko kukasirikiwa na watu. Imesimuliwa ya kwamba Mwenyezi Mungu alimwambia Mtume Isa (a.s.); “Ewe Isa iwapo Mimi nitakukasirikia, basi hapana radhi ya mtu yeyote itakayokunufaisha, na iwapo mimi nitakuridhia hapana ghadhabu ya mtu yeyote itakayokudhuru.”[34]

Usione haya kuvaa Hijabu, bali shikamana nayo kila inapokuwa. Ni lazima popote pale japo iwe ni katika jamii isiyovaa Hijabu, au hata kama umo ndani ya shule au chuo ambacho wengi wao hawana Hijabu wala hawataki kuvaa. Inakupasa uwe na msimamo wa dini yako sawa sawa kama alivyosema Mwenyezi Mungu katika Qur’an;

 “Uwe imara (na msimamo) kama ulivyoamrishwa. 11:112

Mwenyezi Mungu amesema tena.

 “Hakika wale waliosema Mola wetu ni Allah kisha wakawa na msimamo (katika dini yao) huteremkiwa na malaika (wakati wa kutoka roho zao na wakawaambia) msiogope wala msihuzunike na furahini kwa pepo mliyokuwa mkiahidiwa.” 41:30

Usijali kelele za wapinzani, sawa sawa wakiwa ni wanawake au wanaume, bali waambie kama alivyosema Mwenyezi Mungu,

 “Ikiwa ninyi mnatukejeli basi na sisi tutawakejeli kama mnavyotukejeli.” Hud; 11:38

Hapana shaka kwamba tabia ya wapinzani wa sheria za Mwenyezi Mungu siku zote imejaa kejeli na dharau dhidi ya Waumini na Watu Watakatifu. Yote hayo wanayafanya kwani wao hawana utu, na wala hawana dalili wala hoja ya kutetea upinzani na upotofu wao. Na kwa ajli hiyo basi wao hutegemea zaidi njia za kutukatisha tamaa ili tu wapate kufanikisha maovu na maasi yao. Hapana shaka kwamba njia hizi za upinzani ulioshindwa dhidi yetu, ndizo hizo hizo walizokuwa wakizitumia kupambana na Mitume wa Mwenyezi Mungu na watu wema na waumini tangu hapo zamani katika historia ya ulimwengu. Mwenyezi Mungu anasema:

 “Na hapana Mtume yeyote aliyewafikia isipokuwa wao walimfanyia kejeli.” Al-Hijr: 15:11

Na anasema tena Mwenyezi Mungu:

 “Hakika wenye kutenda maovu walikuwa wakiwacheka walioamini. Na wanapopita karibu yao wanakonyezana.” 83:29-30

 “Na pindi wanapowaona husema kuwa hakika hawa wamepotea. 83:32

Ewe dada yangu katika Uislamu, je unafahamu kwamba mwenda wazimu hujiona kuwa yeye pekee ndiye mwenye akili na wengine wote ni wenda wazimu, wakati ukweli hauko hivyo?[35]

Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

 “Basi leo Walioamini watawacheka wale waliokufuru.” 83:34

Hapana shaka kwamba, iko siku Mwenyezi Mungu na waumini watawakejeli wapinzani hawa wanaozicheza shere sheria na kanuni za Mwenyezi Mungu.

Mwenyezi Mungu anasema;

 “Mwenyezi Mungu atawalipa kejeli zao na watapata adhabu kali.” 9:79

Anasema Mwenyezi Mungu;

 “Yakawazunguka wale waliyofanya mzaha miongoni mwao, yale waliyokuwa wakiyafanyia mzaha.” 6:10

Mwenyezi Mungu anasema tena:

 “Moto utababua nyuso zao nao watakuwa humo wenye kukenya (meno yao kwa adhabu). (Waambie) Je hamkusomewa Aya zangu na ninyi mkazipinga? Watasema; Mola wetu! Uovu wetu ulituzidi na tukawa ni watu wenye kupotea.” 23:104-106

Maneno haya ya Mwenyezi Mungu yanaonesha namna watakavyokiri watu hao wenye kejeli kwamba wao katika ulimwengu huu walikuwa waovu, wenye kupoteana kutangatanga. Lakini Mwenyezi Mungu atawajibu kwa jawabu kali;

“Atasema (kuwaambia watu hao) Dhalilikeni humo motoni na wala msinisemeshe. (Kumbukeni kwamba) Bila shaka kulikuwa na kundi katika waja wangu likisema; Mola wetu tumeamini basi utusamehe na utuhurumie kwani wewe ndiwe Mbora wa wanaohurumia. Lakini ninyi mliwafanyia mzaha hata wakakusahaulisheni kunikumbuka na mlikuwa mkiwacheka. Hakika leo nimewalipa (wema) kwa sababu ya kusubiri kwao, bila shaka hao ndiyo wenye kufuzu.” 23:108- 111

Kwa hiyo jione mwenye fahari kwa kuvaa Hijabu, kwani umo katika hali ya kuonesha utiifu wako kwa Allah (s.w.t), na unapata thawabu kila hatua yako moja utembeayo.

 “Kilichoko kwa Allah (s.w.t.) ni bora na ni chenye kudumu Basi Je, Hamfahamu?” 28:60.

 “Na radhi za Mwenyezi Mungu ni kubwa.”9:72

Kinyume chake katika thawabu ni, yule mwanamke asiye na Hijabu, kwa kuwa anapata madhambi kwa kila hatua yake moja anayotembea. Wapo wanawake wasemao; “Mimi najiamini nafsi yangu siwezi kufanya maasi na maovu, hivyo sioni sababu ya kunilazimisha kuvaa Hijabu.”Jawabu la fikra kama hii ni hili lifuatalo. Kwanza: ni lazima ifahamike kwamba vazi la Hijabu ni jambo la wajibu juu yako kwa mujibu wa sheria katika hali yoyote ile iwayo, sawa sawa ukiwa unajiamini au la. Pili: Kujiamini peke yake hakutoshi kwa sababu.

 “Hapana shaka kwamba nafsi ni yenye kuchochea maovu isipokuwa ambayo Mola wangu ameirehemu.” 12:53

Kuna wasichana wengi wameteleza na wakajikuta wameingia ndani ya maovu kwa sabau ya kuacha Hijabu. Tatu: Kuishi bila sitara ya Kiislamu kunasababisha kuamsha hisia za kimaumbile kwa wanaume wanaokutazama, pia inaweza kuwa sababu ya kukufanyia uchafu bila wewe kutarajia. Je! Hili haliwezekani? Hali kama hii ikikufika, huko kujiamini kwako kutakusaidia na au kunaweza kuizuwia hali kama hii isitokee?

Ewe msichana na mwanamke wa Ki-Islamu, usihadaike na fikra potofu, maadui wa Uislamu ndiyo hao hao maadui wa mwanamke, wanaipiga vita Hijabu kwa njia nyingi. Huna budi kuzinduka na kuepuka kampeni hizo sizizo na hekima. Wala usidanganyike na mitego yao iliyomo ndani ya mtizamo wao. Kwa kukuzindua ni kwamba; maneno wayasemayo huenda yakawa yanavutia hasa yanapokuja kwa lugha ya kutaka eti kukukomboa. Maneno yao haya ni sawa na asali tamu lakini ina sumu ukiila itakudhuru. Angalia iwapo utahadaika utakuwa umeiuza nafsi yako na dini yako kwa maadui wa Mwenyezi Mungu, pia fahamu ya kwamba utakuwa umeshawauzia kwa thamani ya kukuangamiza wewe mwenyewe.

Hebu jitahidi kuwa Mwislamu kwa ulimi wako na vitendo vyako. Wachana na nyendo za kiulaya, kwani miongoni mwa malengo yao ni kumtumia mwanamke kama chombo cha kutangaza biashara hali ya kuwa hana sitara. Jilinde kwa Mwenyezi Mungu akuepushe na nyendo zao ambazo nia yake ni kuichafua jamii ya Kiislamu na kuiangamiza. Fahamu ewe dada mpendwa kwamba, maendeleo na uungawana kwa mwanamke ni kuwa na sitara inayokubaliana na mazingira na hali yake kama mwanamke.

Dada wa Kiislamu, utamaduni na uhuru wa kweli unapatikana ndani ya Uislamu na kanuni zake toka mbinguni. Elewa pia kwamba, uovu na fedheha vitakupata iwapo utakwenda kinyume na kanuni za Ki-Islamu. Ni wajibu wako kutangaza na kuelimisha hekima ya Hijabu na falsafa yake kwa nduguzo, jamaa na marafiki. Kazi hii ifanye popote, ikiwa nyumbani, shuleni, chuoni, ofisini na sehemu nyinginezo unazoweza kufanya hivyo katika muda wote wa uhai wako. Kufanya tabligh siyo kazi ya wanaume peke yao, bali na wanawake inawahusu kikamilifu. Mtume (s.a.w.w.) anasema; “Kila mmoja wenu ni mchungaji na ataulizwa kuhusu uchungaji wake aliokabidhiwa.” Historia inatuonesha kwamba Bibi Fatma (a.s.) alikuwa akifafanua mambo yanayohusu sheria kwa wanawake wa Madina. Bibi Zainab binti Ali bin Abi Twalib alikuwa akifundisha tafsiri ya Qur’an kwa wanawake wa mji wa Al-Kufah huko Iraq. Fahamu ya kwamba Mwenyezi Mungu atakulipa thawabu nyingi kwa kila msichana au mwanake atakayefuata nasaha yako ya kuvaa Hijabu na akaongoka kupitia mkononi mwako. Imesimuliwa ndani ya hadithi kwamba, Mwenyezi Mungu alimpelekea ufunuo Nabii Musa (a.s.) akamwambia; “Ewe Musa ikiwa utamrejesha mlangoni kwangu mtu ambaye ni mwenye kuniasi au ukamrejesha uwanjani kwangu mtu aliyepotea, ni bora mno jambo hilo kwako kuliko ibada ya miaka mia moja ambayo mchana utakuwa umefunga saumu na ukasimama usiku ukisali.”[36]

Hapana shaka kwamba mwanamke asiyevaa Hijabu ni muasi anayeziasi kanuni zitokazo mbinguni. Basi mtu kama huyu akirudi kwenye uwanja wa Mwenyezi Mungu kisha akashikamana na Hijabu kutokana na juhudi zako na maelekezo yako, hapana shaka utapata malipo yaliyomo ndani ya hadithi iliyotajwa hapo juu. Kwa hakika hayo ni malipo makubwa mno na ni thawabu nyingi. Hivyo basi ifanye nafsi yako iwe miongoni mwa watu wa tabligh hasa kuhusu Hijabu na elekeza tabligh yako baina ya wasichana wenzio na wanawake wenzio.

Usikatae kuolewa: Dada mpendwa endapo atakuja mtu kukuposa, tafadhali chunguza vitu muhimu na vya msingi. Vitu hivyo ni kama vile Dini yake na tabia yake. Iwapo mtu huyu kakamilika sawasawa kwa sifa mbili hizi usibabaike baina ya kuolewa au hapana. Kwani Dini na tabia ndiyo msingi wa mafanikio ya maisha yako ya ndoa. Usichunguze shahada yake au jinsi yake (utaifa) wala usiangalie suala la mahari kwamba ni kiasi gani anachotoa. Pia nakusihi acha visingizio vya eti mpaka nikamilishe masomo yangu ili nipate shahada ya juu, na sababu zingine zisizokuwa na maana ambazo huenda zikakusababishia kuharibikiwa na Mwenyezi Mungu hatakuridhia. Mtume (s.a.w.w.) anasema: “Atakapokujieni mtu ambaye mwenendo wake na dini yake vinakuridhisheni, basi muozeni mtu huyo, na iwapo hamtamuozesha mtasababisha fitina na uchafu duniani.”

Kuolewa ni sawa na kiota cha dhahabu ambacho ukikipata utatulia na kustarehe ndani yake, na ukweli ulivyo kitakulinda na kuyadhibiti maumbile yako. Mwenyezi Mungu hakumuumba mwanamke ili aishi maisha ya ujane na upweke, bali amemuumba aishi na mume bega kwa bega ili wajenge familia na jamii bora katika kuendeleza kizazi cha wanaadamu. Kwa maelezo haya elewa jambo jingine muhimu nalo ni kuwa: Kuchelewa kuolewa ni makosa na ni hatari, chukua tahadhari ya jambo hili. “Mtume (s.a.w).w. anasema: “Enyi watu! Jibril amenijia kutoka kwa Allah (s.w.t) akaniambia, hakika wasichana bikra ni sawa na matunda yaliyomo mtini, matunda hayo yakishawiva na yakachelewa kuchumwa jua litayaharibu, upepo nao ukivuma utayaangusha chini, hiyo ndiyo hali ya wasichana bikra wakisha vunja ungo hakuna dawa nyingine kwao isipokuwa ni kupata mume (waolewe) na kama hawakuolewa basi hawatasalimika na dhambi, kwani wao ni wanaadamu.”

Baada ya Mtume kumaliza kusema maneno haya, alisimama mtu fulani akasema: ‘Tumuoze nani basi?’ Mtume akajibu: ‘Wanaume wanaostahiki kuwaowa.’ Yule mtu akauliza ni kina nani hao? Mtume akajibu; ‘Waumini baadhi yao ni stahiki kwa baadhi nyingine.’ Akakariri mara mbili.”[37] Ama ikiwa mchumba atakayekuja ni muasi wa Dini yake au kuna kitu kibaya katika tabia yake, kwa mfano asiyeswali, mlevi na mengineyo, huyu mkatae wala usitishike kwa mali yake au cheo chake. Maisha ya upweke ni bora kuliko kuishi na Mume muasi wa Mungu au mwenye tabia mbaya, japo awe na mali au cheo kikubwa. Ewe dada yangu wa Kiislamu, muombe Mwenyezi Mungu akukadirie upate mume mwema ambaye ni muumini aliyekusanya sifa za uzuri wa sura, Dini na tabia njema, kwani Yeye Mwenyezi Mungu anasema:

Back Index Next