Index Next

HIJAB

VAZI LA MWANAMKE WA KIISLAMU

Kimeandikwa na:

MUHAMMAD IBRAHIM KADHIM AL-QAZ-WINI.

Kimetarjumiwa na:

Shaikh Msabah Sha’ban Mapinda

NENO LA MCHAPISHAJI

Kitabu kilichoko mikononi mwako, ni tarjuma ya kitabu cha

Kiarabu, kwa jina la: Al-Hijab Saa’datun laa shiqaaun, kilichoandikwa na, Sheikh Muhammad Ibrahim El-Qazwiniy.

Kitabu hiki kinahusu vazi la Hijabu; vazi ambalo ni rasimi kwa wanawake wa ki-Islamu kwa ajili ya kustiri maungo yao. Maadui wa Uislamu wanalibeza sana vazi hili kiasi cha kutaka kuwakatisha tamaa wavaaji wake - ambao ni wanawake wa kiIslamu. Mazingira ya sasa tayari yanaonesha kwamba, azma ya maadui hawa wa Uislamu kiasi fulani inafanikiwa. Kwani sasa hivi katika miji yetu asilimia kubwa ya wanawake wanatembea nusu uchi, na hali ni mbaya sana. Hivyo tulipo kiona kitabu hiki, tukaona ni wakati muafaka tukitoe kwa lugha ya kiswahili, kwa kutekeleza amri ile ya Mwenyezi Mungu ya, “kuamrisha mema na kukataza maovu.”

Mwandishi wa kitabu hiki ameelezea kwa ufasaha sana falsafa na hekima ya vazi hili, na kuvunja hoja za wale wote wanaolipinga.

Katika kufanya hivyo ametumia elimu, akili na hoja zenye mantiki. Tunamshukuru ndugu yetu, Sheikh Msabah S. Mapinda kwa kukubali kwake kuchukuwa jukumu hili la kutarjum kitabu hiki,

kutoka lugha yake ya asili ya Kiarabu kwenda lugha ya Kiswahili. Halikadhalika tunawashukuru wale wote walioshiriki kwa njia moja au nyingine hadi kufanikisha kuchapishwa kwa kitabu hiki.

Ni matumaini yetu kwamba kitabu hiki kitakuwa ni chenye manufaa kwa wasomaji wetu, hususan wanawake wa kiIslamu na kuiokoa jamii yetu kutokana na maovu.

Mchapishaji:

Al-Itrah Foundation

S. L. P. 19701

Dar-es-Salaam.

DIBAJI

Kijitabu hiki ni tarjuma ya kijitabu kiitwacho Al-Hijab Saa’datun laa shiqaaun, kilichoandikwa na Sheikh Muhammad Ibrahim El-Qaz-wini mwaka 1979. Ingawaje ni kiasi cha miaka ishirini na minne imepita tangu kilipoandikwa, maelezo na mafunzo yaliyomo yanaafikiana kabisa na hali iliyopo ndani ya jamii yetu leo hii. Mwandishi amejitahidi sana kufafanua maana ya Hijabu,ikiwa ni pamoja na kuleta mifano mbali mbali na matukio ya kweli ili kuonesha umuhimu wa Hijabu katika maana inayokusudiwa na sheria ya KiIslamu. Hoja zilizotumika nimadhubuti na zinakubalika iwapo tu uadilifu utatumika katika maamuzi, bila kujali zimesemwa na Uislamu au kinyume chake.

Kijitabu hiki kimekuwa katika lugha ya Kiarabu kwa kipindi kirefu, na baadaye ikapendekezwa kifanyiwe tarjuma ya kiswahili, kwa matarajio ya kuwanufaisha watu wengi wa eneo la mashariki ya Afrika na kwingineko inakozungumzwa lugha ya Kiswahili. Kwa mara ya kwanza tarjuma ya kijtabu hiki ilifanywa mnamo mwaka 1991. Ndugu yetu Bwana Qurban Khaki alikuwa ni mtu wa kwanza kupendekeza tarjuma hiyo. Mwenyezi Mungu amlipe kila la kheri katika kuhudumia Uislamu na Waislamu.

Chapa uliyonayo mkononi sasa hivi ni chapa ya pili ya tarjuma ya kijitabu cha Al Hijab Saadatun laa Shiqaaun, ambacho kimechapishwa na Al Itrah Foundation. Kama ile chapa ya kwanza katika kutarjum kijitabu hiki, tulichokizingatia zaidi ni maana aliyoikusudia mwandishi. Hivyo basi tarjuma hii siyo neno kwa neno ingawaje safari hii mwandishi wa kijitabu hiki amejitahidi kufanya marekebisho ya kukiboresha kwa kuweka mambo mengi ndani ya chapa mpya iliyoko katika lugha ya Kiarabu. Isitoshe sisi wenyewe tumejaribu kufanya ufafanuzi katika maeneo kadhaa ya kijitabu hiki kutokana na umuhimu tuliouona, hasa kwa kuzingatia hali na mazingira tunayoishi

hapa kwetu Tanzania na hata kwa majirani zetu wa eneo hili la mashariki ya Afrika. Kijitabu hiki kimechapishwa mara kumi katika lugha ya Kiarabu kutokana na umuhimu wa maudhui ya Hijabu kwa umma wa kiislamu na wanaadamu wote kwa jumla.

Napenda kuitumia nafasi hii kumshukuru Dr Mohamed Kanju kwa msaada wake mkubwa wa kukipitia kijitabu hiki. Si hivyo tu bali namshukuru tena kwa mchango wake wa kututolea tarjuma

za Habari moto moto tulizozinasa kutoka kwenye mtandao wa internet wakati wa kumalizia tarjuma ya kitabu hiki. Habari hizo kwa umuhimu wake tumezitia mwishoni kitabuni humu kwa

kuwa ni miongoni mwa njama za wapinzani wa Uislamu na Waislamu katika utekelezaji wa Sheria hii tukufu inayomtaka mwanamke wa kiislamu avae Hijabu. Tunamuomba Mwenyezi Mungu atujalie tuwe ni wenye kunufaika na miongozo iliyomo kitabuni humu, na tuonyeke kwa kila onyo lililomo.

Was-salaam Alaikum,

Msabah S. Mapinda.

Mtarjumi.

19/10/03.

Utangulizi

Bismillahi Rahmani Rahimi.

Amesema Mwenyezi Mungu Mtukufu ndani ya kitabu chake kitukufu: “Na mnapowauliza kitu (wakeze Mtume) waulizeni nyuma ya pazia”.[1]

Baada ya kauli hii ya Mwenyezi Mungu, ni wajibu wetu kuufahamisha ulimwengu mzima ya kwamba, Mwanamke ni kiungo muhimu katika jamii, na anayo haki na heshima kama mtu mwingine yeyote anayeishi katika dunia. Siyo kweli kwamba yeye ni kiumbe tofauti, au ni kiumbe kigeni katika suala zima la maisha ya kila siku, bali yuko katikati ya mazingira na matukio yake daima. Kwa kuwa Uislamu ni dini inayoshughulikia hali ya maisha ya wanadamu kwa kila nyanja, imetoa umuhimu wa pekee katika kulinda na kutetea utu, heshima, pamoja na haki za mwanamke. Kwa sababu hiyo basi, Uislamu umemuwekea mwanamke kanuni za sheria zitakazomfaa kulingana na mazingira yake kimaisha, iwe katika maisha yake peke yake au katika ndoa, na au ndani ya familia na jamii yote kwa ujumla.

Kadhalika Uislamu umempa mwanamke nafasi ya kushughulikia masuala yanayomhusu katika dunia na pia akhera, kama yalivyoelekezwa kisheria. Nafasi hii inaweza kumfikisha katika safu za Malaika na kumfanya kuwa kiumbe kitakatifu hapa duniani na akhera. Kutokana na umuhimu wa mwanamke katika jamii ya wanadamu, Qur’an inayo sura nzima inayoitwa Sura An-nisaa, ambayo inataja baadhi ya masuala yanayowahusu wanawake.

Isitoshe ndani ya Qur’an zimo Aya nyingi zinazozungumzia miongozo mbali mbali juu ya mwanamke, ikiwemo namna ya mienendo na mavazi yake ndani ya jamii, halikadhalika na haki zake. Yote haya lengo lake ni kuonesha umuhimu wa mwanamke na kumtakia mafanikio na usalama wake.

Maumbile ya mwanamke yanapoangaliwa kwa makini sana, hapana shaka yoyote yanaonekana kwamba, yanatofautiana mno na maumbile ya mwanaume, kisaikolojia na katika sehemu fulani

ya mazingira ya kijamii. Kutokana na tofauti hii, ilibidi pia kuwe na tofauti kati ya mwanamke na mwanaume katika baadhi ya hukumu za kisheria na kanuni. Tofauti hii imekuja kutokana na hali halisi ya maumbile ya mwanamke. Kwa hiyo basi, kanuni na sheria nazo zikaja katika baadhi ya nyakati kufuatia hali na maumbile ya mwanamke. Siyo kweli kwamba tofauti hii ni kwa ajili eti ya kumdhalilisha na kumfanya mwanamke kuwa ni kiumbe pungufu, kama wanavyodai maadui wa Uislamu.

Katika moja ya kanuni muhimu za sheria ya kiislamu iliyotiliwa mkazo, na kumlazimisha mwanamke kutoachana nayo ni Hijabu. Kanuni ya Hijabu haikuja isipokuwa ni kwa ajili ya kuhifadhi na kulinda mafanikio ya mwanamke, bila kusahau heshima yake na utu wake. Kanuni hii inazingatiwa kuwa ni miongoni mwa kanuni muhimu sana ndani ya Uislamu.

Kutokana na umuhimu wake, Mwenyezi Mungu ameitaja katika Aya nyingi za Qur’an, na wala hakutosheka kuitaja katika Aya moja au nusu ya Aya, kama ambavyo kuna kanuni ambazo Mwenyezi Mungu amezitaja mara moja katika Aya moja au hata nusu ya Aya. Tutaonesha umuhimu wa kanuni hii ndani ya kitabu hiki kwa mujibu wa Aya nyingi za Qur’an zilizoitaja kanuni hii.

Mwenyezi Mungu amelikariri mara nyingi suala la Hijabu katika Qur’an ili kuonesha umuhimu wake ndani ya jamii na maisha ya wanadamu. Je ni kwa nini basi Waislamu inawapasa kuliangalia suala la Hijabu kwa makini, na pia kutumia muda mwingi kulitafakari na kuzinduana? Jawabu lake ni kwa sababu upinzani na uchochezi wa kutia dosari Hijabu, na kuitolea tafsiri

ambazo siyo maana halisi iliyokusudiwa katika vazi hili, umeongezeka na unazidi kuongezeka. Upinzani na uchochezi huu unakuja kutoka kwa maadui wa Uislamu na watu wapenda maovu.

Na kwa kutumia kalamu zao na kelele zao, siku zote wamekuwa wakijaribu kuonesha ubaya wa Hijabu, na kwamba eti inarudisha nyuma maendeleo. Pia hupata wakadai, “Ati Hijabu ni kumdhalilisha mwanamke na ni kumtesa.”Hayo ni pamoja na uzushi mwingineo wanaouona kuwa unaweza kuwasaidia katika kampeni yao hii dhidi ya Hijabu. Kwa masikitiko makubwa, ziko baadhi ya serikali zinaonesha msimamo wa wazi kabisa katika kupinga Hijabu, bali zinatumia kila aina ya uwezo walionao kusambaza upinzani huo kwa kuwataka wanawake wa kiislamu waache kujisitiri kwa mujibu wa sheria ya dini yao.[2]

Mambo haya hayafanyiki kwa siri, kwani mara kwa mara tunasoma magazetini na au kusikia kwenye vyombo vya habari vingine kwamba serikali fulani imetoa agizo kuwazuwia mabinti wa kiislamu wasiendelee na masomo ya sekondari au chuo kikuu kwa sababu tu ya wao kuvaa Hijabu. Na kuna baaadhi ya serikali zinatoa maagizo kuwa, miongoni mwa masharti ya kujiunga na vyuo vikuu vya nchi hizo, mwanamke anatakiwa asivaae Hijabu!!

Mpenzi msomaji, ukirejea nyuma kidogo tu katika historia ya nchi ya Iran utakuta kwamba, mwanzoni mwa utawala wa mfalme Shah aliyepinduliwa, lilipitishwa azimio rasmi la kuzuia kabisa uvaaji wa Hijabu kwa wanawake wa kiislamu nchi nzima. Askari walitawanywa njiani, sokoni mpaka katika njia za majangwani kwa ajili tu ya kuwazuia kuvaa na kuwavua wanawake wanaoonekana kuwa wamevaa Hijabu. Kutokana na unyama huu, wanawake wengi wa kiislamu waliona ni bora wabakie majumbani mwao kwa muda wa miaka mingi kutokana na hofu ya kunyanyaswa na askari wa serikali.

Enyi watu nyie! Ni ya nini vita hii munayoineza dhidi ya Hijabu? Ni kwa nini hampambani na umalaya na maovu yaliyokithiri ndani ya jamii yetu na badala yake mnaelekeza mapambano yenu

kwa wanawake wanaolinda heshima ya mwanamke, heshima ya jamii bali pia wanalinda utu wetu?[3]

Ni kwa nini mapambano hayo msiyaelekeze kwenye madanguro ambayo tuna hakika kwamba

yanajulikana fika? Kwa nini hampambani na ulevi unaotishia familia zetu? Kwa nini hampambani na madawa ya kulevya yanayoziangamiza nchi zetu na kizazi chetu, bali pia yanaangusha uchumi wa nchi zetu? Kwa nini hampambani na umaskini uliokithiri ndani ya jamii yetu? Mbona hampambani na vibaka wanaotishia usalama wa raia kila kukicha? Mwenyezi Mungu anasema:

“Na anapotawala hujitahidi kufanya uharibifu katika nchi na kuteketeza mimea na viumbe. Na Mwenyezi Mungu hawapendi watu waharibifu.”[4]  

Siyo ajabu watu hawa kusema hayo wayasemayo hasa tunapozingatia kwamba, wao wanaelewa vizuri na kutambua hekima zilizomo ndani ya kanuni hii na falsafa zake, mambo ambayo yanakubalika kiakili na kimaumbile. Kwa upande mwingine wanakuta Hijabu ndiyo kizuizi kikubwa na madhubuti dhidi ya matendo yao machafu ndani ya jamii safi ya Waislamu. Ndiyo maana wakawa wanaipinga kanuni hii ya kiislamu kwa njia mbali mbali kupitia maonesho ya Television, Redio, Magazeti, Majarida, Sinema n.k. Nia yao ni kumuondeshea aibu na haya mwanamke wa kiislamu, pia kumvua vazi la utamaduni wake kama Mwislamu, na baadaye asiwe na haya wala aibu kisha wamtelekeze na kumsukumiza katika janga la maovu na uchafu mwingineo.

Maadamu mambo yako katika hali hii, yaani vita inaendeshwa dhidi ya mwanamke wa kiislamu, basi hana budi mwanamke huyu wa kiislamu ashikamane na vazi hili la Hijabu. Inampasa pia asimamie kwa uwezo wake wote kueneza mafunzo na hekima za Hijabu baina ya wanawake, wasichana walioko mashuleni na majumbani, na asisitize uvaaji wa vazi hili la Hijabu. Wajibu huu

ni kwa mwanamke kwa upande wake na pia kwa Waislamu wote.

Halikadhalika Waislamu wasikubali kutoa nafasi kwa maadui hawa kutekeleza malengo yao ya kishetani, ambayo yanaudhuru Uislamu na Waislamu. Nataraji kitabu hiki kitakuwa ni chenye kuongeza hamasa ya kuimarisha kanuni ya Hijabu na kuivaa. Mwenyezi Mungu ndiye mwenye kufanikisha na ndiye msaidizi.

Muhammad Ibrahim Muwahidi El-Qaz-wini.

1-5-1400/1979.

QUR-AN INASISITIZA KUVAA HIJABU.

Katika utangulizi tumetaja kwamba, Qur’an inahimiza sana sana kuvaa Hijabu, na katika Aya nyingi za Qur-an umetajwa mkazo wa jambo hili, nasi tutataja baadaye baadhi ya Aya nyingi zinazohusu suala hili na kuzifasiri kwa kifupi.

  1. Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema; “Ewe Nabii, waambie wake zako na binti zako na wake wa waaminio, wateremshe shungi zao. Kufanya hivyo kutapelekea wao kutambulikana (kwamba ni wanawake waungwana) hawatakerwa (na watu waovu), na Allah ni Mwingi wa kusamehe (tena) Mwenye huruma”.[5]

Katika Aya hii tukufu, Mwenyezi Mungu anamuamuru Nabii wake Muhammad (s.a.w), awaamrishe wanawake wa kiislamu wakiwemo wakeze, binti zake na wake wa waaminio, wajisitiri kwa kuvaa Hijabu iliyokamilika. Katika zama za mwanzo wa kuja Uislamu wanawake walikuwa wakitoka majumbani mwao bila kujisitiri miili yao kikamilifu, kama vile walivyokuwa wakitoka wanawake wa zama za Jahiliya (kabla kuja Uislamu). Hali ya kutokujisitiri kikamilifu kwa wanawake, haikuridhiwa na sheria ya kiislamu, ndipo Mwenyezi Mungu alipomuamuru Mtume

wake Muhammad (s.a.w.w) awaambie wanawake waumini wajisitiri na wavae Hijabu, na awakataze kutoka majumbani mwao bila sitara iliyokamilika kisheria. Akasema Allah s.w.t kumwambia Mtume (s.a.w.w), “Ewe Nabii waambie wake zako na binti zako na wake wa waaminio wateremshe shungi zao.”Tamko (Jalabib) ambalo limetumika kwenye Aya ya hamsini na tisa, maana yake kilugha ni ushungi ambao hufunika kichwa cha mwanamke na uso wake na kumkinga asionekane kwa watu kwani kwa mujibu wa sheria haifai kuonesha mbele yao baadhi ya sehemu za mwili wake. Bali ilivyo ndivyo, ni mwanamke asitiri sawa maungo yake

kama sheria inavyomtaka kuyasitiri.

Ama maana inayopatikana katika kauli ya Mwenyezi Mungu aliposema; “Kufanya hivyo kutapelekea wao kueleweka (kwamba ni wanawake waungwana)”Kauli hii inalenga kufahamisha kuwa, Hijabu humfanya mwanamke atajwe kwa utajo wa wema, na katika jamii hupambika kwa sifa ya Uchamungu.

Ni mara chache Wachamungu kukumbwa na mikasa itokanayo na watu waovu, ndiyo maana Mwenyezi Mungu akaendelea kusema katika Aya hiyo ya hamsini na tisa kuwa; “Hawatakerwa

na watu waovu”.

Hii inamaanisha kwamba, macho ya watu waovu, wajeuri na wenye khiyana, hayamfikii mwanamke ambaye amejisitiri kikamilifu tena kisheria, kwa kuwa vazi la Hijabu humlinda dhidi

ya aina mbali mbali za uovu, hata kumfanyia maskhara (utani) huwa ni vigumu. Hijabu huwa inasitiri mwili wa mwanamke na kuufanya uzuri wake na mapambo yake kutoonekana, kwani (awapo ndani ya Hijabu) hakuna kinachoonekana katika mwili wake, na mwanamke huyo huwa amesalimika kutokana na shari za aina tofauti. Salama hii hupatikana kwa kuwa, muovu amuonapo na kumtambua kwamba mwanamke huyo ni Mchamungu, tena ni mwenye kujihifadhi barabara hushindwa kumtendea ubaya. Kwa hiyo katika Aya hii tukufu, tuna dalili iliyo wazi inayotujulisha kwamba, kuvaa Hijabu ni lazima, pia inatujulisha kwamba, Hijabu inamhifadhi mwanamke kutokana na ufisadi na aina nyinginezo za uchafu.

2. Mwenyezi Mungu anasema tena kwamba; “Na mnapowauliza (kitu wakeze Mtume), waulizeni nyuma ya pazia, kufanya hivyo kutatakasa nyoyo zenu na nyoyo zao”. (33:53)

Aya hii inawaamuru Waislamu wanapouliza au kuomba kitu kutoka kwa wake wa Mtume (s.a.w.w) waulize hali ya kuwa wako nyuma ya pazia. Hapa wametajwa wake wa Mtume, lakini matumizi ya amri hii ni kwa wanawake wote ambao sheria ya kiislamu hairuhusu kuonana nao bila ya kuwepo kizuizi kwa ujumla.

Maana inayojitokeza katika Aya hii, ni kupatikana wajibu wa kuwepo sitara, yaani Hijabu baina ya wanaume na wanawake.

Siyo sawa wanaume na wanawake kukosa mipaka ya mawasiliano, lazima papatikane muongozo utakaoeleza mipaka hiyo. Ndani ya Aya hii ya hamsini na tatu, Mwenyezi Mungu aliposema;

“Kufanya hivyo kutatakasa nyoyo zenu na nyoyo zao”. Kilichokusudiwa ni kwamba, suala la Hijabu kwa maana yake halisi ni jambo jema kwa pande zote mbili yaani wanaume na wanawake. Hapana shaka kwamba mwanaume anapomuangalia mwanamke, jambo hilo huamsha hisia za kijinsia, na kumpa shetani nafasi ya kumsukumiza mwanaume huyo katika mambo ya haramu na ufisadi. Na kwa upande wa mwanamke, pindi anapokosa kuwa ndani ya mazingira ya Hijabu, tayari huwaanaiweka heshima yake na utu wake katika hatari ambapo wakati wowote ule anaweza kuvunjiwa heshima yake. Hivyo basi vazi la Hijabu ni utakaso kwa wanaume na wanawake, na ikiwa kizuizi cha wanawake na wanaume kuchanganyika kitaondolewa,hali hiyo inaweza kusababisha ufisadi na fitna ndani ya jamii, mambo ambayo Mwenyezi Mungu ameyakataza nakuyaharamisha.

Hali hii ya uovu ndani ya jamii inajitokeza kwa wingi mno ndani ya maeneo yasiyozingatia kanuni hii ya Hijabu.[6]

Wakati huo huo ni lazima tufahamu ya kwamba, Mwenyezi Mungu ameyakemea maovu na ufisadi kwa aina zake na vyanzo vyake vyote. Baada ya maelezo haya yatupasa tujiulize, je ni kwa nini Mwenyezi Mungu wakati akilielezea suala la Hijabu tamko lake akalielekeza kwa wakeze Bwana Mtume ((s.a.w))? Jawabu lake ni kwamba, wakeze Mtume wanayo daraja maalum ndani ya jamii ya kiislamu, kadhalika wao ni Mama wa Waumini wote, na kwa ajili hiyo wanatarajiwa mno kuwa na ziada katika utekelezaji wa sheria za Mwenyezi Mungu Mtukufu, na miongoni mwa sheria muhimu ni hii kanuni ya Hijabu. Kutokana na ukweli huu, mwanzoni tu mwa Aya hii Mwenyezi Mungu ameanza kwa kusema: “Enyi Wake wa Mtume, ninyi si kama yeyote miongoni

mwa wanawake”.[7]

Maana ya maneno haya ni sawa na kumwambia mtu mwenye elimu, “Wewe Bwana ni mwanachuoni usiseme uongo”. Sasa basi, maneno kama haya huwa hayamaanishi kuruhusu kusema uongo kwa asiyekuwa Mwanachuoni, bali maana yake ni kuwa sifa ya kuwa mkweli

inamsatahikia mno mtu huyo na uongo kwake ni jambo baya sana. Bali ukweli ulivyo ni kuwa, jambo lolote ambalo huwa ni sababu ya mwanaadamu kuingia ndani ya makosa, huwa ni haramu kwa mujibu wa sheria ya kiislamu. Ni wazi kabisa kwamba, wanawake wengi walikuwa wakienda kwa wake wa Mtume (s.a.w.w) na kujifunza mambo mengi waliyokuwa wakiyaona kwao.

3. Mwenyezi Mungu anatoa maelekezo zaidi anasema: “Na kaeni majumbani mwenu (enyi wanawake) wala msioneshe mapambo yenu kama walivyokuwa wakionesha (mapambo yao) wanawake wa zama za Jahiliyya (kabla kuja Uislamu).[8]

Ndani ya Aya hii mnapatikana amri ya Mwenyezi Mungu inayomtaka mwanamke kutulizana nyumbani mwake, ili ashughulikie masuala ya ndani miongoni mwake ni kuhusu ndoa yake na familia, ikiwa ni pamoja na kuwalea wanawe kwa malezi ya kidini na tabia nzuri. Hii ndiyo maana sahihi ya wanawake kutulizana majumbani mwao. Na iliposemwa katika Aya hii ya 33; “Na wala msioneshe mapambo yenu kama walivyokuwa wakionesha mapambo yao wanawake wa zama za kijahiliya.”Maana yake ni kuwataka wanawake wa kiislamu wasitoke majumbani mwao kila inapobidi kutoka, bila ya kujisitiri sawa sawa kama walivyokuwa na tabia hiyo wanawake wa zama za jahiliya. Si sawa mwanamke kuonesha mapambo yake hadharani. Na inapotajwa mapambo, lazima ieleweke wazi kwamba mapambo ni kama vile hereni, bangili, mikufu n.k. Istoshe kwa vitu hivyo kuwa ni mapambo, bali mwanamke yeye mwenyewe bila kuongeza hereni au mkufu ni pambo. Kwa hiyo basi mwili wake asiuache wazi na kuufanya uonekane kwa kila mtu.

  Index Next