Mwanamke Mshirika Katika Maisha
 

 

 


 


 
The .HTML version of this book is taken from
www.al-islam.org and ebooked by www.ShiaLibrary.com and www.islamkutuphanesi.com . May Allah be pleased with all.



MWANAMKE MSHIRIKI KATIKA MAISHA




 

Mwenyezi Mungu Mtukufu asema:

“Enyi watu! Hakika tumekuumbeni kutokana na mwanamume na mwanamke.  Na tumekufanyeni mataifa na makabila (mbali mbali) ili mjuane.  Hakika ahishimiwaye zaidi miongoni mwenu mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule am­cha­ye Mungu zaidi..”                 (49:13)

Je dini zimemdhulumu mwanamke?  Wako wasemao hivyo lakini kabla ya kujibu swali hili kwanza ni lazima tufafanue mambo mawili:

1.         Lazima tutofautishe kati ya dini zingine na dini ya Kiislam, kwa sababu katika dini zingine mwanamke huenda akawa na picha mbaya. Nami sina shaka kwamba dini iliyoteremshwa na Mwenyezi Mungu haiwezi kumdhulumu mwanamke au kumvunjia heshima.

Ama katika dini ya Kiislam, mwanamke ana heshima, na anatukuzwa zaidi ya mwanamume.

2.         Ni lazima tutofautishe kati ya mafunzo ya dini kwa mwanadamu na wanaadamu wenyewe wanaoifuata hiyo dini, kwani huenda ikawa hao wanaofuata dini wanamdhulumu mwanamke katika nyanja fulani, lakini hatuwezi kusema hivyo ndivyo dini inavyotaka, kwa sababu dini yenyewe haitaki uonevu, uwe umefanyiwa mwanamume au mwanamke au hata wanyama na mimea. Kwa hivyo mimi ninapozungumzia haki  za mwanamke, sizungumzii msimamo wa wafuasi wa dini, bali nazungumzia msimamo wa dini, basi nasema hivi; dini haiwezekani imdhu­lumu mwanamke, kwa sababu ndogo tu, nayo ni kwamba dini ni orodha ya maisha iliyoletwa na mwenyewe aliyeumba hayo maisha.  Na ikiwa Mwenyezi Mungu alimuumba mwanamke ili amtukuze, basi amemuumba ili amrehemu, ili amuingize peponi, kama alivyomuumba mwanamume kwa hayo; kwa hivyo haiwezekani amdhulumu, kwa sababu huyo mwanamke haku­chagua awe mwanamke au mwanamume.

Mwanamke huzaliwa mke, hana hiyari, na mwanamume pia huzaliwa mume pasi na hiyari.  Vipi tena dini imhukumu mwanamke kwa jambo ambalo hakulichagua yeye mwenyewe (la kuwa mwanamke)?

Kwa hakika dini ya Kiislamu yapinga vikali kila aina ya ubaguzi wa jinsi ya mtu alivyozaliwa bila ya kujia­mulia mwenyewe.  Mathalan ubaguzi wa rangi (mtu hakukhiyari awe mweupe au mweusi), ubaguzi wa lugha, n.k.  Dini haibagui mweusi wa Afrika wala mweupe wa Ulaya, wala haibagui kati ya anayezun­gumza lugha ya Kiingereza au Kijerumani au lugha nyengine.  Wala haibagui aliyezaliwa nchi fulani au nyengine, kwa sababu kuchagua rangi, jamii au nchi anayozaliwa mtu hakuko chini ya uwezo wa mtu huyo.   Aidha dini haibagui kati ya mume na mke kwa sababu kuchagua jinsi ya kuwa mume au mke hakuko kwenye uwezo wa mwanadamu. 

Ama kuhusu kutenda mema dini haibagui katu, hapa yafafanua:

“...Hakika sitapoteza amali ya mtendaji mema miongoni mwenu awe mwanamume au mwanamke.”             (3:195)

Aya nyengine yafafanua:

“Na watakaofanya mema wakiwa wanaume au wanawake hali wao ni wenye kuamini basi hao wataingia peponi.”

                                       (4:124)

Vilevile dini yakwambia kwamba, uwezo wa mtu kujichagulia awe mume au mke uko kwa Mwenyezi Mungu. 

“Yeye ameumba namna mbili mume na mke.”        (53:45)

Na yamkemea vikali anayebagua kati ya mume na mke:

“Na mmoja katika wao anapopewa khabari ya (kuzaliwa kwake) mtoto wa kike uso wake huwa mweusi akajaa sikitiko.  Akawa anajificha watu (wasimuone) kwa sababu ya khabari ile mbaya aliyoambiwa! (anawaza) Je akae naye juu ya fedheha hiyo au amfukie udongoni (kaburini akiwa hai)?  Sikilizeni!  Ni mbaya mno hukumu yao hiyo.”

                                                                             (16:58-59)

(Mambo haya yalikuwa yakifanywa wakati wa uja­hiliyya kabla ya Uislamu).

Hii ndiyo picha jumla ya mtazamo wa dini juu ya mwanamke.  Na sasa hebu tuangalie kwa ufafanuzi dini isemavyo:

Tukiuliza dini, je una maoni gani au kwa maelezo ya ndani zaidi, nini mtazamo wako juu ya mwanamke?  Tunaiona hapa dini ikijibu: Mwanamke yu hali tatu:

1.          Mwanamke anapokuwa mdogo na msimamo wa baba yake kwake.

2.          Mwanamke anapoolewa na msimamo wa mumewe kwake.

3.          Mwanamke anapokuwa mama na msimamo wa wanawe kwake.

Katika hali ya kwanza (anapokuwa mdogo) twaona kwamba Uislamu wamwambia babake kupitia kwa Mtume (saw) akisema: “Mtoto wa kike ni rehma na wa kiume ni neema.”  Mtume (saw) pia amesema: “Kumbusu binti yako ni jambo jema.”  Amesema pia:  “Bora ya watoto wenu ni mabinti.”  Amesema pia:  “Bora ya watoto ni mabinti wenye kujisitiri.”

Imepokewa Hadith nyingine kwamba:  Mtume (saw) alipopewa bishara ya kuzaliwa mtoto wa kike, ali­waangalia maswahaba nyusoni akawaona wamechu­kizwa, akawaambia:  “Mna nini nyinyi?  Hilo ni ua la rehani ninalolinusa na aliloniruzuku Mwenyezi Mungu.”

Vile vile twaona katika maisha ya Mtume (saw) kwamba yeye hajawahi kubusu mkono wowote ila mikono ya watu wawili tu:

1.          Mkono wa bintiye Fatima Zahra alipokuwa na miaka tisa, ilikuwa kila aingiapo kwa babake, alikuwa akisimamiwa na babake (Mtume (saw)) kumbusu mkono wake na akimketisha mahali pake; na hilo alilifanya hasa kwa ajili ya kuwa­zoezesha na kuwafundisha umma wake.

2.          Mkono wa mchapa kazi, aliyekwenda kwa Mtume (saw) akampa mkono, Mtume (saw) aka­hisi usugu wa mkono wa mtu yule, akamuuliza, “Mbona hivi?” Yule mtu akajibu: “Huu usugu ni kwa sababu ya kuchapa kazi ee Mtume wa Mwenyezi Mungu.”

Mtume (saw) akainama, akambusu mkono wake huo akasema: “Huu ndiyo mkono unaopendwa na Mwenyezi Mungu na Mtume wake!”

Vilevile unahimiza baba anaponunua zawadi za watoto wake, mtoto wa kike apate mbili na wakiume apate moja.  Au binti atangulie kupata kabla ya mvulana.

Imepokewa Hadith kutoka kwa Ibni Abbas; Mtume (saw) amesema:  “Atakayekwenda sokoni na kununua zawadi akenda nayo kwa familia yake (nyumbani) huyo ni kama aliyechukua sadaka na kuwapelekea wahitaji, basi na aanze kwa kuwapa watoto wa kike kabla ya watoto wa kiume, kwani atakayemfurahisha binti yake ni kama aliyemwacha huru mmoja mio­ngoni mwa wana wa Ismail (as).  Na mwenye kumfu­rahisha mtoto wa kiume, mtu huyo ni kama anayelia kwa kumcha Mwenyezi Mungu.”

Lakini jambo la kusikitisha ni kwamba watu wengi humtanguliza mtoto wa kiume kuliko mtoto wa kike katika maneno na vitendo vinavyohusu mambo yote ya nyumbani.  Mtu humnunulia mtoto wake wa kiume akamwacha wa kike au anaposhauri, kuhusu mambo ya ndani ya nyumbani kwake humshauri mtoto wake wa kiume na asimshauri wa kike.

Wazazi wengi wanawapa kipaumbele watoto wa kiume na kuwashughulikia sana kuliko watoto wa kike jambo linalowafanya watoto wa kike wajihisi kuwa wanadharauliwa na hilo huwafanya wakawa na chuki.  Kufanya hivi, licha ya kuwa haifai kisheria, vilevile huacha athari mbaya kwenye uhusiano wa wavulana na wasichana na hasa pale kila mmoja wao anapokuwa mwenye familia yake mwenyewe.  Jambo hilo twaweza kuligundua tunapochunguza zile fa­milia zenye aidha wasichana tu au wavulana pekee; ambapo utaona watoto wataishi wakiwa wameshi­kamana, ama wanapokuwa chini ya baba yao, ama kila mmoja anapokuwa tayari ana familia yake, kwa sababu watoto hao hawakubaguliwa kijinsiya.  Lakini kinyume nao, wale watoto walioonja ubaguzi wa kijin­siya utawaona hawana mshikamano pale wana­po­fikia kila mtu wakati wa kujitegemea.

Mtume (saw) asema:  “Mtu atakayekuwa na mtoto wa kike na hakumdhalilisha wala hakumtanguliza mwanawe wa kiume zaidi ya huyo wa kike, basi Mwenyezi Mungu atamwingiza peponi.”

Ama hali ya pili: Mwanamke anapokuwa mke wa mtu (rejea nyuma kidogo ili kufahamu zaidi) tutaona kwamba dini ya Kiislamu yamwambia mumewe hivi:  “Mcheni Mwenyezi Mungu juu ya wanawake kwani wao ni amana iliyoko kati ya mikono yenu, mmewachukua wao kuwa ni amana ya Mwenyezi Mungu, basi waoneeni huruma na zifurahisheni nyoyo zao mpaka wasimame pamoja nanyi.”   Mtume Muhammad (saw).

Vile vile amesema (saw):  “Mbora wenu, ni yule aliye mbora kwa mke wake, nami ni mbora kwa wake zangu.”

Anaendelea kusema Mtume (saw):  “Mja hatazidi kuwa na imani ila atazidi pia na kuwapenda wanawake.”

 Katika Hadith nyengine nyingi asema: 

·            “Mtu atakayemuoa mwanamke basi na amhe­shimu.”

·            “Dunia ni starehe, na bora ya starehe za dunia ni mke mwema.”

·            “Mambo matatu mtu akiyapata amefaulu: mke mtiifu, nyumba yenye nafasi na mnyama mwenye kasi.”

Katika Hadith nyingine! “Jibril hakuwacha kuniusia kuhusu wanawake mpaka nikadhani itakuwa haram kuwaacha.”

Imam Ali naye asema: “Ama haki za mkeo, ni wewe ujue ya kwamba Mwenyezi Mungu amemjaalia kuwa ni kitulizo na liwazo kwako, na ujue hiyo ni neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwako”.

Haki za Ndoa

Kwa mtazamo wa dini, mke ni mshirika katika maisha yeye ndiye anayemkamilisha mume na mume ndiye anayemkamilisha mke.  Wewe wamuhitajia, naye pia akuhitajia.  Mke si mtumishi, bali ni ‘mke’ kwa hivyo anafaa kutumikiwa.

Ama haki ambazo mwanamke lazima amtekelezee mumewe ni mbili tu.  Ya kwanza ni haki ya kita­ndani (tendo la ndoa),  yaani kuonana kimwili (ngono), kumpa mwili wake mumewe anapotaka.  Pia Uislamu hapo wasema mtu ajiandae kwa mkewe kama ambavyo mke ajiandae kwa mumewe (kabla ya kuonana).  Mume anapoomba hilo na hali zinaru­husu, basi mke ni lazima awe amejiandaa.  Sayyidna Ali (k.w.) amesema:  “Mke aliye muovu zaidi ni yule amnyimaye mumewe (tendo la ndoa).”

Haki ya pili ni mume kujua mke anapotoka nyu­mbani, yaani ajue mke anakokwenda.  Haifai katika Uislam  mke ajiendee tu popote au vyovyote atakavyo huku mumewe hataki.  Mtume (saw) amesema: “Mke yeyote atakayetoka nyumbani kwa mumewe bila ya idhini ya mumewe, basi huyo hulaaniwa na kila kitu kinacho chomozewa na jua na mwezi mpaka mumewe amridhie.”  Kwa kuwa ajua sababu iliyomfanya atoke ni nzuri hawezi kumficha mumewe.  Na ikiwa mume ni mtu muumini haamrishi wala hakatazi ila kwa sa­babu ya maana.  Basi mke anapotoka bila ya idhini yake kila kitu kitamlaani mpaka mume ajue sababu ya kutoka kwake na aridhike. Hizi ndizo haki mbili za mume kwa mkewe.

Ama haki za mke kwa mumewe ni nyingi:

1.          Mume amfurahishe mkewe ki-ngono, na kima­penzi na haifai mume aache kabisa kabisa kounana na mkewe kimwili. Haifai asionekane kwa muda mrefu bila ya udhuru wa maana.

2.          Ni juu ya mume amtimizie mkewe mahitaji ya lazima, nyumba inayofaa, mavazi yafaayo na chakula.

Mke si mali ya mume bali ni mshirika wake katika maisha anaingia mkataba na mume kwa ajili ya kuishi pamoja na kupendana pamoja na kubeba mzigo wa watoto pamoja.

Kwa hivyo, mke si katika majukumu yake kumtu­mikia mumewe bali kinyume chake.  Mume anakali­fiwa ki-sheria na kibinaadamu kutosheleza mahitaji yote yanayohitajika.

Ama kupika, kufagia, kufua au kuajiriwa ili kupata pesa, haya yote si wajibu wa mke. Anaweza asipike, asifagie, hata asimnyonyeshe mtoto. Kwani haki yake kwa mtazamo wa dini mume amlipe kwa kuwa maziwa anayompa mtoto ni sehemu ya maisha na mwili wake.  Baba ndiye mwenye jukumu la ulezi wa mtoto, kwa hivyo ni haki yake mke alipwe kwa kunyonyesha.

Mke ni “mke” wala si mtumishi, atakapojitolea kufagia, kupika, kunyonyesha na kulea si haki yake bali aweza kujizuia na hayo na haijuzu mume kwa vyovyote kumtenza nguvu apike, afagie afue au aoshe vyombo.

Akijitolea naye mume asimpatilize mathalan kwa kuzidi kutia chumvi  kwenye chakula au maji si baridi, nyumba chafu au haikusafishwa vizuri.  Kwa sababu hawajibiki na hayo yote, madhali amejitolea basi afanye  ni hisani kwa mume. Na kwa sababu hii ndipo tunakuta historia yasema kwamba Mtume (saw) ha­kulaumu katu mapishi ya chakula katika maisha yake.  Alikuwa akishirikiana na wakeze kupika na kufagia na akisema: “Wale wafanyao kazi nyumbani mwao ndio wa kweli katika umma wangu.”

Ama hali ya tatu ya mwanamke ni pale anapokuwa mama, uislamu unawalazimisha watoto kumheshimu, inasema Qur’an. 

“Wala usiwaambie Ah!…”                                       (17:23)

Kijana mmoja alikwenda kwa Mtume (saw) akasema:  “Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, ni yupi aliye bora zaidi kwangu nimtendee mama?” Mtume akamjibu: “mamako.”  Yule kijana akauliza  “kisha nani?” Mtume akajibu:  “kisha mamako.” Akuliza tena:  “Kisha nani?” Akajibu:  “Kisha mamako” akauliza (mara ya nne):  “Kisha nani?” Akamjibu:  ”Kisha babako”.

Yaani hii ni kuonyesha kwamba haki za mama ni nyingi zaidi kuliko za baba mara tatu zaidi.

Alikwenda kijana mwingine kwa Imam Sadiq (A.S) akasema:  “Ee mjukuu wa Mtume, mimi nilimbeba mama yangu mgongoni kwangu na kuhiji naye mara nyingi akiwa mgongoni kutoka Madina hadi Makka, je nimetekeleza haki zake?”  Akatabasamu Imam Sadiq akamjibu:  “Wallahi bado hujatekeleza haki yake hata ya usiku mmoja alipoamka akakuwekea titi lake mdomoni ukanyonya.”

Hivi ndivyo ilivyo, utaona kwamba Uislamu unaanga­lia mwanamke kama mwanaadamu aliyeumbwa na Mungu kwa matakwa haswa ya muumba, kama ali­vyoumba mwanamume kwa kutoka kwake yeye muumba na ndio maana akaamrisha mwanamke ahishimiwe.

Anapokuwa msichana, dini yakwambia mheshimu.  Anapoolewa, dini yakwambia mheshimu, na anapo­kuwa mama, dini yakwambia mheshimu.

Dini inawatahadharisha wale wanaowapiga wake zao, inasema:  “Mwenye kunyoosha mkono wake ili amzabe kofi mwanamke huyo ni kama aliyeun­yoosha mkono wake motoni.”

Pili inasema:  “Mkeo asiwe ni mtu umchukiaye, kwa kuwa mwanamke ni ua la mrehani si mtumishi.  Na jiepusheni na wivu pasipo mahali pake, kwani ku­fanya hivyo humfanya yule mzima akapata maradhi, na asiye na hatia kumtia kwenye shaka.”

Masuala ya upande wa kike

Baadhi ya watu hujiuliza kuhusu Hijab, kwa nini dini ikawajibisha?  Wengine huuliza:  Je inafaa mwanamke afanye biashara, au ukulima?

Wengine wanataka kujua je mahari ni thamani (bei) ya mwanamke? Na wengine wanauliza kama inafaa mwanamke mmoja aolewe na waume wengi!

Ama kuhusu Hijab, kwa hakika mtazamo wa dini kwa mwanamke ni mtazamo wa kijumla, yaani ujumla mwanamke ni binaadamu na siyo wa kuji­starehesha naye tu.

Kwa hivyo inatubidi tumuangalie ki-upande huo, lakini kwa kuwa yeye ni kivutio kwa sababu ana maumbile mazuri ya kike yanayomvutia mwana­mume, ndipo dini ikafaradhisha Hijab ili kuzuia mwanamke asigeuzwe njia ya kujistarehesha, na hai­fai tumtazame mwanamke kama bidhaa ya kuuzwa au chombo cha starehe kama yanavyofanya maendeleo ya ki-magharibi ambayo yamemvua ubi­nadamu wake na kumbakishia  uanamke wake ndipo akafanywa ni kitu cha matangazo ya biashara ili kumvutia mteja.  Mwanamke anatumika kwenye biashara kiasi kwamba wanapotaka kuuza gari hum­si­ma­misha msichana mzuri kando ya gari hilo wa­kampiga picha nalo ili lipate kuuzwa.

Isitoshe hata wanapotaka kuuza farasi maalum, wa­tamsi­mamisha msichana mrembo kando ya ran­chi ya farasi ili awavutie wanunuzi wamnunue farasi huyo. Hata kwenye matangazo ya bustani ya kufugwa wanyama mwanamke amekuwa aki­tu­mika! Hivi ndivyo mwanamke anavyotumika kwa faida ya kibinadamu naye huhitajiwa tu pale anapo­kuwa mrembo wa kumezewa mate; ama akiwa mbaya au ameumbwa na uzuri wa kawaida tu, huwa hana thamani kwa sababu huyo hawezi ku­vutia wanaume.

Ama Uislamu haukubali mwanamke atupwe kwenye matamanio, kama alivyosema Imam Ali:  “Mwanamke ni rehani na si mtumishi.”  Mre­hani lazima uhifadhiwe.  Na mwanamke ni almasi lazima athaminiwe.  Tunaposema almasi lazima ifichwe ili isiibiwe, je huko utasema ni kuivunjia heshima almasi au kuichunga?  Basi vivyo hivyo mwanamke na Hijab!

Hapana.  Hijab si kumtweza mwanamke bali ni kum­chunga kutokana na wizi wa ngono.  Na  maadam mwanamke anatakiwa na mwanamume kwa mata­manio basi yampasa ajihifadhi maumbile yake ya kike kwa njia ifaayo, nayo ni kuficha vivutio vyake. Mwanamke mzuri ni yule anayejistiri mwili wake na  waume wengine na kujionyesha kwa mumewe tu.  Mtume (saw) asema: “Bora ya wanawake zenu ni yule mzazi, mwenye mapenzi, mwenye kujisitiri, mwenye kumtii mumewe, mwenye kujichunga na mwengine, anayemsikiza na kumtii amri zake na wanapokuwa faragha, humpa akitakacho.” 

Amesema pia:  “Mbora wa wanawake wenu ni yule anapokuwa faragha na mumewe huvua vazi la kuona haya.”        

Ama kuhusu wanaume ambao hawamtaki ila kwa ajili ya kufaidi tu, Uislamu umemzuia na hilo.  Kwa sababu kijana anayemchukulia msichana kama mpita njia tu kwa ukweli huwa hana haja naye ila hutaka kutimiza haja za matamanio yake tu wala hana penzi.  Kwa hivyo anachotaka ni kukidhi haja zake tu wala hajali mabaya wala mazuri ya mwanamke huyo.

Mara ngapi tumeona matukio kadha wa kadha katika nchi mbalimbali ambapo msichana amechukuliwa na kijana akatembea naye kisha akamwacha abebe mateso yake.

Kuhusu kufanya kazi, Uislamu haumkatazi mwanamke kufanya kazi yoyote.  Uislamu hausemi kwamba ni haramu kwa mwamanke awe mfanyi kazi au mkulima au mfanyi biashara, bali ni haki ya mwanamke afanye kama afanyavyo mwanamume katika kufanya kazi, kulima, biashara n.k. kwa sharti tu awe na “heshima” na kuulinda utu wake.

Uislamu unakataza kwenda tupu na mwanamke ku­jionyesha sehemu za mwili wake, haukatazi kufanya kazi.

Sote tunajua ya kwamba Bi Khadija bint Khuwailid (r.a.) alikuwa tajiri na mfanyi biashara mkubwa na ali­juana na Mtume (saw) kupitia biashara zake ambapo Mtume (saw) alikuwa akifanya kazi kwake.

Mwanamke anaweza kufanya kazi ikiwa atahifadhi Hijab yake kazini, au asichanganyike na wanaume wawezao kumuoa.  Kwa sababu bila ya kufanya hivyo atageuka kuwa ni burudani kwa wanaume.            

Ama kuhusu mahari, kwa mtazamo wa uislamu, ni alama ya kuonyesha kuwa msichana huyu anata­kiwa namvulana huyu.  Hutolewa mahari ili mwanamke ajihisi kuwa anahitajiwa na mwana­mume na si yeye anayemtaka mume, jambo linalo mtosheleza haya zake alizoumbwa nazo na heshima zake ambazo bila shaka zitavunjika pale yeye ataka­pom­taka mwanamume.

Mahari si thamani ya bei anayolipa mume kuununua mwili wa mwanamke, na ndipo ukaona uislamu haukupanga kiwango cha mahari na kitu chochote chaweza kuwa mahari (k.v. vyombo n.k.) hata kumfundisha hesabu au sura ya Qur’an kunaweza kuwa mahari, au chochote hata kiwe ki­dogo namna gani.

Isitoshe, uislamu unapenda mahari yawe kidogo.  Mtume (saw) anasema:  “Bora ya wanawake wa umma wangu ni wale wazuri wa uso wenye kutolewa mahari kidogo.” Na kila mahari yanapokuwa kidogo, inaamanisha kwamba huyo msichana (kwani ndiye anayetaja mahari) anamtaka huyo mume mwenyewe na si mali yake, na huyo mume anamtaka mke mwenyewe si kwa sababu amemnunua.

Kuhusu suala la mke na waume wengi, dini imekataza hilo kwa sababu hizi:

1.          Mwanamke hafai kushea ikiwa wewe hufai ku­shea hata kalamu yako, utaridhika kushirikana mkeo?

2.          Suala la kuona ni utangulizi wa kupata watoto, na kuwa na waume wengi ni kuchanganya watoto.

3.          Mwanamke ana hisia za ‘ulinzi’ yeye vyoyote ilivyo anatafuta mtu wa kumlinda.  Hebu uliza nchi gani inayotawaliwa na maraisi wawili? Au dola gani ya ndoa inayotawaliwa na waume wawili?

Hata upande wa mume kuoa wake wengi uliuhu­siwa na uislamu kwa sababu ya kutatua matatizo mengi, ikiwa ni pamoja na idadi ya wanawake kuwa kubwa zaidi ya wanaume.  Nchini Merekani pekee, kuna wajane milioni tisa waliofiwa na waume zao, na mamilioni ya washichana ambao hawajaolewa.

Vilevile sababu ya kuwa na wake wengi yaweza kuwa ni kwa ajili ya maslahi ya mwanamke kwa mfano; hebu tuchukulie mke ni tasa, hazai na mumewe anataka watoto na kisha mume tumzuie asiwe na wake wawili (asioe), hii ina maana kwamba tutamruhusu amuache yule mkewe ili aoe wa pili.  Hii kwa kweli itakuwa si kwa maslahi ya yule mkewe.

Hili ndilo suala la mwanamke, ambaye ana heshima yake katika uislamu, kwa sababu yeye ni kiumbe cha Mungu, na amejaaliwa hivyo na Mungu muumba kwa ajili ya kujuana kama isemavyo Qur’an:

“Enyi watu! Hakika tumekuumbeni kutokana na mwanamume na mwanamke.  Na tumekufanyeni mataifa na makabila (mbali mbali) ili mjuane.  Hakika ahishimiwaye zaidi miongoni mwenu mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule am­cha­ye Mungu zaidi..”                 (49:13)

Ama maendeleo ya kimagharibi (Ulaya) heshima ya mwanamke imevunjwa, amekuwa ni thamani tu ya kibiashara au burudani ya ki-ngono mambo yana­youtweza utu wake na hili sisi hatuliridhii wala hatutaki limpate mwanamke.

Wanamuua mwanamke siyo!

Siku moja Mtume (saw) alikuwa ameketi na baadhi ya maswahaba zake kwenye changarawe akachora kwa kidole chake ardhini mstari ulionyooka, kisha kando ya msitari huo akachora msitari ya mshazari, mmoja upande wa kulia na mmoja wa kushoto, akaashiria kwenye ule msitari wa kwanza ulionyooka akasema:  “Hii ni njia ya Mwenyezi Mungu, kisha akaashiria kwenye ile mistari mingine akisema:  “Na hizi ni njia zingine ambazo juu ya kila njia pana shetani anayewaita watu waifuate.  Kisha akafumba macho kwa muda mfupi kidogo, kisha akasema:  “Kwa hakika hii ndiyo njia yangu iliyonyooka, basi ifuateni.  Wala msifuate njia zingine mtafarikiana na njia ya Mwenyezi Mungu.”

Kwa hivyo hapa Mtume ameeleza upotofu wa kila njia isiyolingana na njia ya Mungu kama vile alivyoonyesha jinsi njia ya  Mungu inavyojitenga kimsingi na njia za shetani.  Sasa basi, tunapotaka kuigundua njia ya Mungu kuhusu masuala ya mwanamke tusiwaulize mashetani, na maana ya mashetani hapa ni wote walioanguka chini ya matamanio.  Yatupasa tuangalie kwenye maneno ya Mwenyezi Mungu na Mtume, kwa sababu mapenzi ya nafsi daima hufikiria lile jambo ilitakalo na haya­fikiri ukweli ulivyo.

Mtu akisema ‘Hijab hakuna katika uislamu’ wakati yeye anasoma jinsi Qur’an inavyosema:  “…na mnapowauliza kitu basi waulizeni nyuma ya pazia (hijab), mtu huyo hakusudii hijab kama ilivyo kwenye uislamu ila ni kwa kuwa hijab haiku­ridhisha matakwa yake, ya kimwili ndiyo maana akasema hakuna hijab.

Hivyo ndivyo ilivyo, na kwa hakika uislamu ndio unaopanga njia ya Mwenyezi Mungu na si watu wengine, na ndipo hapa tunakuta kwamba Mwenyezi Mungu anaweka orodha ndefu kuhusiana na maswala ya mwanamke:

1.          Maisha ya mwanamke ya kipekee

2.          Masuala ya mwanamke ya kijamii

3.          Masuala ya mwanamke ya kifamilia

4.          Masuala ya mwanamke ya ki-jinsiya.


Ufafanuzi wa masuala haya ni kama ifuatavyo:

1.          Kuhusu masuala ya muhusuyo ni kwamba yeye anapaswa kutenda yale yapasayo mwanamume kuyatenda kama kufanya ibada, kuwa na tabia nzuri  n.k.

2.          Mwanamke ana haki zote za kijamii na anaweza kufanya biashara kulima na kufanya kazi mradi tu ahifadhi heshima yake ya kike.

3.          kifamilia, mwanamke ni msimamizi wa utekelezaji ndani ya nyumba ambapo mume anakuwa ni kiongozi wa taasisi ya familia.  Aya isemayo:  “Wanaume ni wasimamizi wa wanawake” haimaanishi mwanamume atumie mabavu, na kulazimisha mambo; uislamu hau­mu­an­galii mwanamke kama mtumishi au si bandia wa anayefaa atishwe mizigo ili mwana­mume ajinufaishe.

Mwanamke ni mshirika wa wanaume, si mtumishi kwa hivyo yampasa mume kwa sa­babu mke ni bibi wa familia amuandalie mshirika wake huyo maisha mema ya ki-­binaadamu.

4.          Yampasa mke aishi vizuri na mumewe na amtosheleze nastarehe za jinsiya inavyotakiwa na kwa ndoa ya kisheria, na uislamu una orodha na miongozo mirefu juu ya suala hili linalofafanua kwa usawa kwa mume na mke njia za kuonana kimwili [1]  Nayo ni miongozo iliyofafanuliwa inayoeleza hata namna ya kufanya tendo la ndoa na wakati muwafaka wa hilo.

Kwenye orodha hizi zinazohusu masuala ya mwanamke katika uislamu tunagundua kwamba zinamuangalia mwanamke kuwa ni mwanaadamu, mwenye haki ya kuishi kwa usawa na mwanamume.

Lakini kuna zingine zisizokuwa za kiislamu ambazo zamuangalia mwanamke kama mwanaserere (kiji­sanamu) wa kujistareheshwa naye tu kamili.

Na kama tulivyoona, ni kwamba Uislamu unafanya juhudi kuona kwamba umedhibiti starehe za kimwili kwenye familia na maisha ya ndoa. Uislamu hauru­husu starehe hizo kutangazwa sokoni, barabarani, mabarazani au kwenye mikusanyiko. Pia hauruhusu kwenda uchi, kujionyesha mapambo, au kuchanga­nyika kuovu kwa wake na waume na kukaa faragha. Hayo yote yanaambatanishwa na adabu, desturi na hukmu maalum.

Hivi ndivyo Uislamu unavyolipa suala la mwanamke la jinsiya picha  yake halisi na kulipa umuhimu kama yalivyo masuala mengine yawe ya kijamii au ya ki­familia. Hivyo ndipo uzani wa usawa unapohifadhika na kuzuia mwanamke asitumiwe kama chombo cha madhambi au kisanamu cha ku­chezewa.

Ama mifano mingine (isiyo ya Kiislamu) yenye mi­singi na hukmu ambayo inaendelea hivi leo chini ya kivuli cha ‘maendeleo’(kompyuta na electroniki) inafanya juhudi za kufanya mwanamke awe ni ‘jinsi nyingine’. Asipotimiza wayatakayo basi hapana haja aweko.    Kwa msingi hii haya yote yamepangwa juu ya desturi za mambo hayo, ambapo baadaye hakuna kizuizi kwa mwanamke kuyafuata kama; kusam­baratika kwa familia, kuzaa nje ya ndoa, kuenea zi­naa n.k.

Kwa hivyo mwanaadamu leo yampasa achague moja kati ya njia mbili. Ama njia ya kujizuia, (maisha ya ki-familia ya ndoa) au njia ya zinaa (kuharibika kwa familia).

Njia ya kwanza ni ya Mungu na ya pili ni ya shetani. Wale wanaochagua njia ya pili, yawapasa wafahamu kwamba jambo haliishi kwa wao kuifuata kando kando (bora wasifuate kabisa). Ama kujaribu ku­changanya baina ya njia mbili hakufai ila ufuate njia ya Mungu tu. Kwa sababu njia ya shetani  ni njia ya matamanio nayo hayana mwisho mwema. Kila mwanaadamu anapotopea humo, matamanio nayo humwambia; vipi nyongeza!

Suala: Je! yapasa kumpendelea mwanamume zaidi ya mwanamke kiasi cha kumnyima mwanamke haki nyingi za kisiasa na kijamii?

Jibu:  Lau kama mwanamke hatofautiana na mwanamume upande wa maumbile yake ya ki­mwili, kiakili na kifikra, hapa suala la kupendelewa lingeingia mahali pake.  Lakini kwa kuwa mwanamke kimsingi anatofautiana na mwanamume hapa suala si ‘kupendelewa’ bali suala ni ‘kuhu­sishwa’ na kuweka kila jambo pale panapofaa.  Hivi hasa ndivyo inavyoafikiana na maoni na mfumo wa Uislamu. Mwanamke kwenye Uislamu ana nafasi zake maalum, kwa sababu sehemu hizo zahitaji ahu­sishwe nazo yeye hasa.

Mathalan; kama ambavyo si sahihi daktari asomeshe mambo ya uhandisi (uinjinia), au kipofu achukuliwe kuwa muongozaji rada! Basi vile vile si sahihi mwanamke abebeshwe majukumu asiyoweza kuya­beba. Hata sayansi inatuonyesha kimsingi jinsi mwanamke alivyo tofauti na mwanamume.

Dkt. Casius Carel, mshindi wa tuzo la Nobel katika sayansi anasema: “Mambo yanayomtofautisha mwanamume na mwanamke hayaishii kwenye maumbile ya viungo vyao vya uzazi tu, au tofauti katika malezi yao tu, bali kuna mambo mengi. Tofauti hizo zina maumbile ya kimsingi zinazoanzia kwenye mpangilio wa kimwili, mwanamke katika kila kiungo cha mwili wake ana vitu vya maji maji vya kemikali vinavyorutubisha uzao.  Wale wanaodai kuwa na malezi sawa, elimu na kazi baina ya wanaume na wanawake hawazijui tofauti hizi kabisa; tofauti za kimsingi. Mwanamke alivyo hasa ana tofauti kubwa na mwanamume kwani kila chembe chembe (cell) katika mwili wake ina umbile la kike, hata mpangilio wa mishipa yake uko tofauti.”

Anaendelea Dkt Carel: “Utaratibu na kazi za vuingo vya mwili una mpangilio maalum kama vile elimu ya nyota na hesabu. Haiwezekani kufanya badiliko lolote kwa kuwa tu mwanaadamu anataka kubadilisha. Kwa hivyo letu sisi ni kukubali kama ilivyo. Na wanawake nao ni lazima wakuze vipawa vyao kulingana na maumbile yao, na waache kuwaiga wanaume kiholela. Nafasi yao katika maendeleo ni kubwa kuliko ya mwanamume na haifai kuiacha.”[2]

Maadam majaribio ya kisayansi yameonyesha tofauti hizo za kimaumbile, basi yapasa kutenganisha suala la mwanamume na la mwanamke. Kila mmoja wao apewe wadhifa ule utakaolingana na sifa zake. Mwanamke ana sifa za huruma basi ni  lazima kazi ya kulea watoto aachiwe yeye, kwa sababu kazi hiyo inahitajia huruma.  Na mwanamume kwa kuwa ana nguvu za kubeba majukumu mazito, basi hapana budi apewe  uongozi wa kusimamia nyumba na nchi.

Isitoshe, inapasa ratiba ya masomo ya mwanamke ibadilishwe ili iambatane na tabia, umbile na akili yake.

Vilevile hapana budi majukumu yake katika maisha ili yalingane na shakhsiya yake ya huruma.

Tutakapomweka mwanamke kwenye nafasi yake ifaayo basi tutaweza kuinua hali ya nchi iliyoporomoka.  Kwani kumpa kila mtu nafasi yake anayohusika nayo ndiko kumwezesha kupata fursa kwenye jamii ya kufikia maendeleo.          

Jamii ya mwanadamu ina mfumo wa “kutofau­tiana”. Ama jamii ya wanyama ina mfumo wa “kuwa sawa”. “Kutofautiana” ina maana ni kuto­fautiana watu na kila aliye na sifa fulani kumfanyia na kumkamilishia mwingine ambapo “kuwa sawa” maana yake ni kuwa sawa bila ya kushughulikiana. Kwa hivyo hapa, utaona kuwa mwanamume ana­muhitajia sana mwanamke na mwanamke anamu­hitajia sana mwanamume.  Lau ingelikuwa mwana­mume na mwanamke “wako sawa”, basi mmoja asingelimu­hitajia mwengine.

Dkt. Maranon anasema:  “Jambo linalothibiti ni kwamba, ukamilifu wa mwanadamu utatimia, na lazima utimie, kwa kuziainisha tofauti zao, yaani mwanamume ajione zaidi ni mwanamume, na mwanamke ajione zaidi kuwa ni mwanamke.”[3]

Kwa hivyo ni upumbavu wanawake wawaige wanaume, na wanaume nao kuwaiga wanawake.

Msichana aliye baleghe hapendezi mbele ya mwanamume pale anapovaa Mini au Kaptula (Short pants) kama vile mwanamume avae gauni, viatu vya mchuchumio (High heels) pochi kwapani na ajitie manukato ya kike ya ki-Faransa!

Takwimu zimeonyesha kwamba wanaume hupendelea sana wanawake wenye kujiheshimu kuliko wenye kujidhihirisha wazi wazi. Ndiyo, ni kweli mvulana (mhuni) mhuni hupata kumchezea msichana anayevaa Mini anapompitia mbele yake barabarani.

Lakini penzi liko mbali na suala la ndoa ya daima, kwani mwanamume katu hawezi kumuoa msichana mwenda-uchi. Anajua wanawe atakaozaa naye wa­taharibika kwa sababu mama atakayewalea ata­penda zaidi kujipamba kwa ajili ya wanaume wen­gine ili awavutie, kuliko kuwalea wanawe.

Na msichana apendaye kuangaliwa na maelfu ya ma­cho yenye njaa naye hajaolewa, basi hata atakapoolewa atapenda zaidi macho ya watu yamuangalie.  Haitai­shia hapo, mwisho itafikia kupokea wanaume!

Familia nyingi zimesambaratika kwa sababu mwanamke si mwenye kujistahi.  Kwa kweli ni ujinga wa mwisho mwanamke avunje heshima yake kwa sababu tu watu maarufu wa Ujerumani wanafanya hivyo, au vijana wajifanye kama watu washuhuri wa Marekani wafanyavyo.

Suala hapa si maendeleo kama wanavyodai bali suala ni uigaji wa kiholela.  Hebu niambie - kwa haki ya Mola wako - maendeleo yako wapi kulea watu wanaofanana na ramani ya Italia?

Maendeleo ya wapi, mvulana anapojitia rangi ya mdomo na kuvaa mikanda ya wacheza sinema wa zamani?

Maendeleo gani wanafunzi wa kike wakutane chooni wapeane tembe za kuzuia mimba?

Maendeleo gani mvulana amuazime dadake nguo ili aende kwenye tafrija fulani,  kama ilivyozoeleka hivi sasa Ulaya?

Watu wengi waliteleza wakaporomoka kwenye mashimo ya upotevu wa kijinsiya na matokeo ya kuteleza kwao yalionekana baada ya kupita muda.  Kwa nini basi nasi turudie makosa waliyofanya wengine?

Njia ya maendeleo haijapotea mwituni, watu wote wanajua kuwa ni njia ya kujistahi, amali njema na tabia nzuri.

Vilevile njia ya maangamivu haijapotea, na watu wote wanajua kuwa ni njia ya uovu, ulevi na tabia mbaya.

Ripoti zinasema:  “Vijana wamefuata njia mbaya inayopelekea kukata tamaa na kupotea na wanajiona kuwa hawana thamani wala maana, na wanahisi kupotea na chuki.” Ripoti za hivi karibuni zinasema kwamba paketi bilioni moja za madawa ya kulevya aina ya ‘L.S.D.’ hutumiwa na vijana kila mwaka mjini London. Vile vile zaidi ya watumiaji wa bangi laki moja nchini Merekani wameshikwa na wazimu, baadhi yao wamepelekwa kwenye mahospitalli ya wendawazimu au wengine wamefariki barabarani.[4]

Ikiwa mmoja wetu anahofia yasitokee haya basi inampasa aizibe njia ya kuelekea kwenye mkondo huo kabla haujaanza kwenda. Upepo unavuma kwa kasi sana katika zama zetu hizi. Wala si muda mrefu vijana wetu nao pia yatawapata yaliyowapata vijana wa Marekani na London iwapo wataendelea kuranda randa kwenye njia ya ngono na maovu.

Vilevile wasichana wetu yatawapata kama wakifuata njia hiyo hiyo, yaliyowapata wasichana wa Ulaya kiasi kwamba leo imekuwa huko Ulaya msichana amuoa msichana mwenzake yaani mmoja ni “mume” na mwingine ni “mkewe” na kisha ‘hulala’ naye. Madhambi haya yanafanywa hivi leo na wasichana Amerika na Urusi.  

Wasichana wawili wa Marekani mmoja akiwa na umri wa miaka ishirini na tano na mwengine wa miaka ishirini na tisa waliomba waruhusiwe kuoana, naye mkuu wa jimbo lao analichunguza ombi lao hilo.  Hata hivyo yule msichana mdogo ‘mke mtarajiwa’ (ambaye hucheza kwenye vilabu vya usiku) ameeleza kwamba yeye haogopi maneno ya watu, bali tatizo pekee anawaogopa wavulana wa ‘mchumba wake’ ambaye ana wavulana watatu mmoja wao mwanajeshi wa majini wa Amerika.[5]
 

Wanasema!!

·            Wanasema kwamba:  “Mwanamke lazima asome.”  Ndio, sawa lakini basi ndio aende uchi?  Kwa kawaida herufi zinaandikwa kwenye kurasa za vitabu, iweje vijana kwenye vyuo vikuu wazisome miguuni mwa wasichana? 

Mtume Muhammad (saw) amesema kabla ya zaidi ya miaka elfu kwamba; “kutafuta elimu ni lazima kwa kila Muislamu mwanamume na mwanamke.”  Ni wazi kwamba hilo laweza kuwa bila ya kwenda uchi, msisimko au matatizo yoyote.  Kwa nini basi shule mnazifanya za mchanganyiko?  Kwani msichana hawezi kufahamu kusoma mpaka akae pembeni mwa mvulana saa zote akimkonyeza?

Au barabara haifikiki nyumbani mpaka wakutane wanafunzi wa kike na wa kiume na mikono ya wasichana kutiwa kwapani mwa wavulana?

·            Wanasema:  “Hali imebadilika!  Hizi ni enzi za kwenda angani na Atomiki, hatuwezi kuishi kizamani, ambazo ilikuwa ukisafiri mpaka upande punda na kina baba kuwaficha mabinti zao wasijidhihirishe...!”

Lakini ee jamani huko kwenda angani ndiko kunakomfanya msichana aidhihirishe miguu?  Au mwanamke akivaa hijab, ndege haitaruka, hata mtu apande punda?

Na je Atomiki imegundua kwamba sasa mwanamke aonyeshe mwili wake mbele za watu?

Hebu ijaribuni heshima na kujistahi, mtaona kwamba hizi zama za kwenda angani hazitarudi kuwa za kwenda ardhini (ikiwa mwanamke atajiheshimu na akajichunga).  Na hiyo Atomiki pia haitageuka ikiwa mwanamke atarudi kuangalia anayekwenda uchi.

Jaribuni hivyo mtaona kuwa mwanadamu amekuwa na ubinaadamu sana pale anapofanya ngono kulingana na mipaka, vipimo na misingi yake bila ya kupetuka mipaka ya dini na akili.

·            Pia wanasema: “Sisi twampenda mwanamke, kwa hivyo twataka tumuone yeye na manukato yake kila mahali.”

Je kumpenda ndio kumtangaza barabarani?  Je! kumpenda ndio kulichukua ua liliochanua na kulianika kwenye madirisha yote?  ...Hapana... Nyinyi hamumpendi mwanamke, bali nafsi zenu!  Nyinyi mwamuua mwanamke, mwamuua!  Ama sivyo?

Mwanamke Wa Dini; Majukumu Na Wajibu Wake

“...Mwenyezi Mungu amewaumba kutokana na nafsi moja...”                                                                      (7:189)

Wajibu na majukumu ya mwanamke ni kama ya mwanamume,  na suala lake ni kama la mume yaani suala la haki, ujumbe na marejeo.  Isitoshe, mustakbali wa kazi yoyote ni dini kwa njia moja au nyengine mwanamke naye ana kazi yake.

Kuna kazi zingine ambazo hakuna awezaye kuzisimamia na kuzitekeleza ila yeye, kwa maana hiyo, huwezi kupata harakati zozote zenye kufaulu ila mwanamke atakuwa na fungu lake kubwa humo. 

Ushahidi wa hayo ni mapinduzi ya Iran.  Kuanzia hapa ndio pamekuwa na haja ya kuweka picha bora zaidi kwa mwanamke; vipi anapaswa awe, nini wajibu na majukumu yake, ndipo hapo tutajaribu kufafanua.

Majukumu Ya Mwanamke

“...Lau si waumini wanaume na waumini wanawake...”

 (48:25)

Kazi inayompasa kufanya mwanamke wa kidini siyo zawadi anayopewa na mwanamume (akikataa kumpa, basi) bali ni miongoni mwa haki zake na ni miongoni mwa majukumu yake kwa hiyo ni juu yake atekeleze majukumu yake.  Vinginevyo, hatakubaliwa atoe udhuru mbele ya Mwenyezi Mungu na Historia kwamba wanaume hawakumwachia atimize wajibu wake wala hawakumpa kazi ya kufanya kwenye utekelezaji huo.

Kwa hivyo ni lazima mwanamke huyo ajihisabu kuwa yumo kwenye kutekeleza wajibu wake kwa kujitolea nafsi yake kwenye upande wa mapambano kwa kuinua kiwango chake cha kifikra, kisiasa, kielimu, kidini na kikazi.

Inapasa achukue mfano wa wapiganaji jihadi wakubwa wa kike kama Bibi Khadija Al- Kubra, Bibi Fatima Zahra, Bibi Zainab Al-Kubra na wengineo.

Inapasa mwanamke atangulie na awe mbele ya mwanamume katika kubeba majukumu na wakati huo huo katika kuusimamisha Uislamu.  Kwa sababu mwanamke hutangulia hata katika kubaleghe ‘kisharia’ kabla ya mwanamume kwa miaka minne; vilevile katika kufanya kazi na kutekeleza wajibu atangulie.

Kama twajua kwamba miongoni mwa matawi ya dini ni kuamrisha mema na kukataza maovu, kuwapenda wanaopenda kizazi cha Mtume (saw) na kuwachukia maadui wa kizazi hicho, na jihadi, na kwamba hayo yote ni wajibu kwa mwanamke na mwanamume.  Basi; ni lazima tujue kwamba mwanamke ana kazi kubwa katika kufanya amali na jihadi kushinda  mwanamume.

Katika Historia ni dhahiri kwamba mwanamke alifanya kazi kubwa katika zile siku ambazo Uislamu ulipambana kujenga maisha mapya.  Lakini, hizi siku zote sasa za kutoendelea zimefanya mwanamke awe mbali na mapambano na zimempokonya majukumu yake ya kimapinduzi mpaka kufikia mwanamke kuwa ni mateka, mpishi tu au yaya wa kulea watoto.   

Na kwa kila mwanadamu anapendelea awe ametekeleza wajibu fulani katika maisha na nafsi yake inamsukuma kufanya hivyo.  Lakini, mwanamke wetu hajapata nafasi yake ila tu katika nafasi za wacheza sinema au waimbaji Na wale wanawake wetu wema wamekaa majumbani wakingojea mtu wa kumpa zawadi ya “kazi ya kufanya”; asipokuja wa kufanya hivyo basi huachwa nje.

Lazima mwanamke, ili kurekebisha hali hii, afanye kazi maradufu. Tunaamini kwamba anaweza.  Suala hapa la kujiuliza ni; Je! vielelezo vyenyewe ni vipi?

 

Mwanamke Katika Ujumbe Wa Mwenyezi Mungu

“Na waumini wanaume na waumini wanawake ni marafiki wao kwa wao”                                               (9:71)

Mwanamke muumin, katika ujumbe wa Mungu, siyo yule kiumbe dhaifu mwoga, mwenye kujitenga na uwanja wa mapambano, bali ni yule mwanamke aliyejitokeza mbele, jasiri, mwenye vitendo, mwenye kutengeza mustakbali wake na wa vizazi vijavyo, mwenye kakamio la muda mrefu kwenye njia ya haki, uadilifu, uhuru,na kuinua neno la Mungu.

Mwanamke anapokuwa katika ujumbe wa Mungu yeye ni mume, hapana tofauti kwani yeye amekuwa bega kwa bega na Manabii katika mapambano kama tutakavyoona katika Qur’an.  Mwenyezi Mungu anawapigia  kuwa ni ‘mifano’ na ‘walioamini’ tutataja hapa baadhi ya mifano:

 

Adam Na Hawa

Mtu na Mtume wa kwanza kabisa, Adam, tunaona kando yake kuna Mwanamke, Hawa.

Hawa huyu alikuwa na safari ya taabu na ndefu na mumewe Adam na Ibilisi, tangu peponi hadi kuteremshwa duniani.

Katika kuumbwa walikuwa pamoja, Mwenyezi Mungu akamuumba

“Na akamuumbia mkewe kutokana na nafsi ile ile…”( 4:1)

Walikuwa pamoja walipokutana na Ibilisi. Walibeba majukumu pamoja na wamepokea mwongozo pamoja.  Mwenyezi Mungu anasema katika Qur’an “Na tulisema:

“Ewe Adam!  Kaa wewe na mkeo katika bustani hii (peponi), na kuleni humo maridhawa popote mpendapo, lakini msiukaribie mti huu tu; msije kuwa miongoni mwa waliodhulumu (nafsi zao).  Shetani aliwatelezesha wote wawili, na akawatoa katika ile (hali) waliyokuwa nayo.  Tukawaambia “Nendeni hali ya kuwa maadui nyinyi kwa nyinyi, na makazi yenu (sasa) katika ardhi, na (mtapata) starehe humo kwa muda (mahsusi)                     (2: 35–36)

“Tukasema: Shukeni humo nyote; na kama ukikufikieni uongozi utokao kwangu, basi watakaofuata uongozi wangu huo haitakuwa khofu juu yao wala hawata­huzunika.”                                                                  (2:38)

Kwa hivyo msafara wa Adam na Hawa ulikuwa mmoja, na kubeba majukumu kulikuwa kumoja na matokeo pia yalikuwa mamoja.  Aidha, mapambano kati ya Ibilisi na ‘mtu’ awe mume au mke – ni mmoja. 

“…Tukasema, Ewe Adam! Huyu (Ibilisi) ni adui kwako na kwa mkeo.”                                                                       (20:117)

Hivi ndivyo Mwanamke aliyokuwapo kwa kujitokeza tangu mwanzo wa kuumbwa.

 

Mwanamke Hajar, na Ibrahim (a.s.)

Huyu ni Mwanamke jasiri, mwenye nia safi aliyeihama nyumba yake na nchi yake ili aende akaishi kando ya nyumba ya Mungu  katika ardhi kame isiyo na maji wake manyasi ili amwabudu Mungu pekee na ajitenge na kuabudu watu.  Nabii Ibrahim alisema:

Mola wetu!   Hakika mimi nimewaweka (Ismail na mamaye) katika bonde (hili, Makka) lisilokuwa na mimea yoyote, katika nyumba yake takatifu (Al-Kaaba) Mola wetu!  Wajaalie wasimamishe Swala.  Na ujaalie nyoyo za watu zielekee kwao na uwaruzuku ili wapate kushukuru”                                                               (14:37)

Bibi huyu Hajar alisumbuka na kwenda mbio kwa ajili ya kumtafutia maji mwanawe akienda mbio kati ya Swafa na Marwa; kukimbia huko kukawa ni kielelezo cha kufanya kazi kwa ajili ya kuwatafutia maisha wengine.  Naye alimlea Ismail (a.s.) malezi ya kidini yaliyomfanya anyenyekee na kukubali kukipokea kifo kwa mikono miwili pale alipoambiwa na babake.

“Mimi nimeota usingizini kuwa na kuchinja”.  Jibu la Ismail lilikuwa:  “Ewe baba! Fanya uliloamrishwa (na Mwenyezi Mungu) utanipata mimi Inshallah ni miongoni mwa wanaosubiri.”                                                     (37:102)

 

 

Musa pamoja na Asya

Miongoni mwa picha njema za mwanamke katika ujumbe wa Mungu ni picha ya Bi Asya bint Muzahim, mke wa Dikteta Firaun.

Mwanamke huyu mcha Mungu alikuwa ndiye ngome kuu ya Nabii Musa bin Imran (a.s.) tangu alipozaliwa; pale alipotiwa majini na mamake, akaokotwa na wafanya kazi wa Firaun naye akataka kumuuwa Asya akamzuia; kama Qur’an inayotuelezea: 

“Basi wakamwokota watu wa Firaun, ili awe adui kwao na huzuni; bila shaka Firaun na Hamana na majeshi yao walikuwa wenye uovu.”                                             (28:8)

Iliwezekana Firaun amuuwe Musa mara moja lakini kuingilia kati kwa mkewe (Asya) ndiko kuliko­muokoa Musa na kifo

Na mkewe Firaun alisema’ (Usimuuwe) atakuwa kibu­rudisho cha macho kwangu na kwako, na msimuuwe, huenda atatunufaisha au tumpange kuwa mtoto (wetu)”

    (28:9)

Msimamo huo wa Bi Asya haukuwa kwa Musa tu, bali alikuwa - kama mapokezi yasemavyo – ni mama wa Waislamu wote, akiwahurumia, akiwatetea na kuwakirimu kwa sadaka.

Ndio, alikuwa mke wa Firaun, lakini mapenzi yake yalikuwa ni kupenda haki na ibada zake ni kumwabudu Mungu pekee, na ujasiri wake ni kupigania dini, kwa hivyo alikuwa ni adui wa taghuti Firaun kutokea ndani.

Utukufu ulioje aliokuwa nao wa kuweza kutohadaika na anasa alizokuwa nazo mumewe na kushikamana na Mtume aliye adui wa mumewe?  Milki, na utajiri wa mito ipitayo kwenye ardhi ya nchi ya Misri ndivyo vilivyoiteka akili ya Firaun mtawala wa ki-imla hata akajifanya Mungu, akatangaza wazi wazi kuwa ‘Mimi ndiye Mungu wenu Mkuu”, lakini muangalie huyu mwanamke aliyekuwa akiishi naye na kulala naye kitanda kimoja na kuneemeka na neema alizo nazo mumewe na heshima anazopatiwa (za kuwa mke wa Firaun); pamoja na hayo yote yeye alikuwa muumin na mchaji, hata akaweza kusimama pamoja na haki na kukataa udikteta.

Aliyakataa maisha ya Firaun kwa sababu yalikuwa ni ya dhulma na ujuba, licha ya kuwa yeye ndiye angelikuwa wa kwanza kufaidika nayo! …Hebu mwangalie akiinua macho yake mbinguni akisema:  “Ewe Mola!  Nijengee nyumba peponi”.

Imepokewa kwenye Hadith kwamba kisha: “Firaun alimfunga mikono yake na miguu yake kwa vigingi vinne, akamlaza juani, kisha akaamrisha atupwe jabalini, hatimaye akafa.” Kwa hivyo alikufa shahid.

Kwa hatima yake hii, Asya amekuwa ni kielelezo cha mwanamke wa kidini, na kielelezo cha wote wanaofuata njia ya haki, uadilifu na uhuru.

Mwenyezi Mungu anatupigia mfano: 

“Na Mwenyezi Mungu amepiga mfano wa wale walioamini kweli, ni mkewe Firaun, aliposema: “Ee Mola wangu!  Nijengee nyumba peponi na uniokoe na Firaun na amali zake na uniokoe na watu madhalimu”       (66:11)

Bi Mariyam, mama yake Masih, Isa (a.s.)

Bi Maryam: mwanamke mtukufu aliye juu ya maisha haya ya dunia na anasa zake.

Bi Maryam, aliyekataa njia ya Waisraili, mtetezi wa mihrabu ya ibada …aliyejitenga na jamii ya kimaada yenye misingi ya kuabudu pato na chumo la pesa.

Bibi huyu ndiye aliyejitolea kuyalinda maadili ya dini.

Mariyam ni kielelezo kingine cha mwanamke mwanadini, kisa chake ni kipi?  Jihadi yake ni ipi?  Hebu tuangalie”

Mamake Maryam alipojihisi kuwa mja mzito alimwambia Mungu: 

“…Mola wangu! Nimeweka nadhiri kwako aliyomo tumboni mwangu kuwa wakfu, basi nikubalie.  Bila shaka wewe ndiye usikiaye na ujuaye.”                                (3:35)

“Basi Mola wake akampokea (yule mtoto) kwa kabuli njema na akamkuza makuzi mema na akamfanya Zakariya awe mlezi wake”                                                         (3:37)

Maryam alipokuwa, alishikamana na nadhiri ya mamake akaishi maisha ya utawa na ya kimapinduzi.

Alisimama imara na mwanawe mtukufu Isa (a.s.) na akavumilia kila aina ya mateso, maudhi na tuhuma.  Mwenyezi Mungu anasema:

“Na mtaje Mariyam kitabuni (humo).  Alipojitenga na jamaa zake, (akaenda) mahali upande wa Mashariki (wa msikiti).  Na akaweka pazia kujikinga nao.  Tukampeleka muhuisha sharia wetu (Jibril) akajimithilisha kwake (kwa sura ya) binadamu aliye kamili. Akasema (Maryam):  Hakika mimi najikinga kwa Mwenyezi Mungu aniepushe nawe, ikiwa unamuogopa Mwenyezi Mungu.  (Malaika) Akasema: “Hakika mimi ni mjumbe wa Mola wako ili nikupe mwana mtakatifu.  Akasema (Maryam) “nawezaje kupata mtoto hali sijaguswa na mwanamume (yeyote) na wala mimi si mzinifu?”  Akasema (Malaika ) “Ni kama hivyo (usemavyo) Mola wako amesema haya ni sahali kwangu. Na ili tumfanye muujiza kwa watu na rehma itokayo kwetu.  Na hili ni jambo lililokwisha hukumiwa.”                      

(19: 16 – 21)

Mwenyezi Mungu anaendelea kueleza kisa hiki;  baada ya Isa (a.s.) kuzaliwa:

 “Akenda kwa jamaa zake amembeba.  Wakasema:  Ewe Maryam!  Hakika umeleta jambo la ajabu!  (kuzaa hivi hivi tu), ewe dada yake Harun!  Baba yako hakuwa mtu mbaya wala mama yako hakuwa hasharati.  (Mariyam) akawaashiria kwake (yule mtoto).  Wakasema: “Tuzun­gumze na aliye bado mtoto kitandani?  (Yule mtoto) akasema: “Hakika mimi ni mja kwa Mwenyezi Mungu, amenipa kitabu na amenifanya Nabii.  Na amenifanya mbarikiwa popote nilipo.  Na ameniusia Swala na Zaka maadamu ni hai.  Na ameniusia kufanya mema mama yangu, wala hakunifanya niwe jeuri, mwovu.”  (19:27– 32)

Basi hivi ndivyo alivyokuwa Mariyam, nguzo ya Nabii Isa nanga ya mapinduzi yake.  Alisimama naye bega kwa bega mpaka dakika ya mwisho ya maisha yake; mpaka wawili hawa wamechukuliwa na Mwenyezi Mungu kuwa ni muujiza mkubwa pale aliposema:

“Na tulilofanya mwana wa maryam na mamake kuwa ishara na tukawapa makimbilio mahali palipoinuka…”                                                      

(23:50)

Kwa nini?  Kwa sababu Maryam alikataa kumnye­nyekea asiyekuwa Mungu akiwa katika mazingira magumu kwa ajili ya kuitikia mwito wa Mwenyezi Mungu kwake.

“Ewe Maryam!  Mnyenyekee Mola wako na usujudu na urukuu pamoja na wanaorukuu’                                (3:41)

Na hapa ndipo aliposifiwa 

“Na Maryam mtoto wa Imran aliyejihifadhi nafsi (tupu) yake na tukampulizia humo roho yetu (inayotokana na sisi) na akayasadikisha maneno ya Mola wake, na vitabu vyake, na alikuwa miongoni mwa wanyenyekevu.” (66:12)

Bi Khadija na Mtume

Bi Khadija alikuwa akiamini ujumbe wa Mtume na wa kumtetea.  Mtume alimuoa wakati bibi huyo akiwa na mali chungu nzima, alikuwa ni mmoja kati ya mamilionea wa Kiarabu.  Mtume alipoteremshiwa wahyi, bibi huyu alitoa mali zake zote katika njia ya Mwenyezi Mungu mpaka ilifikia kufa kwa njaa na kiu katika wangwa wa pango la Abu Talib.

Hivi ndivyo alivyokuwa Khadija, mwanamapi­nduzi wa kwanza katika jamii kafiri ya Makka na ndiye wa kwanza katika kabila la Makureish kuswali nyuma ya Mtume pamoja na Ali bin Abi Talib.

Hiyo ndiyo ilikuwa Swala ya kwanza kuswali katika Uislamu.  Ilikuwa ni Swala ya kimapinduzi.

Na ilikuwa Swala ya kweli ya ‘Lailaha illa llah

Bibi huyu alishikamana na Swala hiyo mpaka hatima ya maisha yake katika miaka kumi ya mwanzo ambayo Mtume alikuwa akieneza ujumbe, alistahmili matatizo mazito kuwahi kutokea katika historia ya Kiislamu.

Mtume naye, baada ya kufa Bi Khadija, hakuwacha kutaja wasifu wake kwa jinsi alivyojitolea, ushujaa wake na misimamo yake, hata siku moja Aisha akaona wivu akasema: “..lakini Mweneyzi Mungu amekupa bora zaidi yake (huyo Khadija) “Hapo picha ya ushujaa wa Bi Khadija ikamjia Mtume machoni kwake akamkemea Aisha: “We! Usiseme hivyo! Mwenyezi Mungu hajanibadilishia aliye bora kuliko yeye, kwani alinisadiki wakati watu walinikadhibisha; akanisapoti katika dini ya Mwenyezi Mungu na akanisaidia kwa mali zake, na Mweneyzi Mungu ameniamrisha nimbashirie Khadija nyumba huko peponi.”

 

Ali naye na  Bi Fatma

Fatma ndiye aliyeleta mapinduzi ndani ya mapinduzi pale wengine walipojaribu kuyabadilisha mapinduzi yawe dola.  Yeye alikuwa kiongozi wa mapinduzi ya mageuzi, mbele ya nyuso za matapeli wa kisiasa walioyaiba mapinduzi ili wayafanyie biashara.

Yeye alikataa, akabisha, akakatilia mbali utawala, akajadiliana na khalifa na akaweza kumshinda kwa nguvu za hoja.  Alipambana na kila aina ya mateso kwa ajili ya haki kama vile, kupigwa, kuharibika uja uzito wake na hata kuteketezwa nyumba yake.  Na hakuishi katika kupinga tu, bali mlango wake ulikuwa wazi kwa wanamapinduzi, ndipo akawa ni mwanamke wa kwanza katika uislamu kupinga wizi wa nembo za kiislamu.  Huyo ndiye Fatima.

 

 

Hussein naye pamoja na Zainab

Bi Zainab alikuwa mwenziwe Husein katika mapi­nduzi na mtetezi wake katika kupigana Jihad, vile­vile alikuwa ni tegemeo lake na sauti yake kwa ma­milioni ya watu baada yake.

Ikiwa kila mapinduzi yana umwagikaji wa damu na ujumbe, basi damu iliyomwagika ni ya Husein, na ujumbe ni ule aliokuwa nao Zainab.

Sasa tufanye nini?

Jibu, ni kuchukuwa hatua zifuatazo!

Kuwe na maandalizi ya kutosha.

Yapasa mwanamke mwanadini ajiandae vya kutosha kutumia uwezo wake kwa kuwa Mwenyezi Mungu amempa kila mtu uwezo na vipaji vyake, lakini hivi kuna haja ya kuvigundua, kama Mwenyezi Mungu alivyoweka madini yenye thamani chini ya ardhi, lakini huwezi kufaidika nayo mpaka uyachimbe.

Ni kosa kubwa sana kwa watu au mtu kudharau kipaji na uwezo wake kwani Mwenyezi Mungu atatuuliza siku ya kiyama, kama alivyosema Mtume (saw):  “Hatapita yeyote kwenye sirat miongoni mwenu, mpaka aulizwe kwanza jinsi alivyoupitisha umri wake na alivyomaliza ujana wake.”

Kwa hivyo kwa mwanamke yampasa kwanza kukuza uwezo na kipaji chake na leo ni kukuza uwezo wake binafsi wa uongozi, na hivyo ni kuweza kuwa na sifa zinazostahiki, mathalan; ushujaa,  imani, na subira na uongofu maadili ya kimapinduzi na harakati.

Atakapokuwa na sifa hizi pia itampasa akuze uwezo na kipaji chake katika uongozi, usemaji utunzi, mbinu za ushujaa na ajifunze kuendesha gari na pikipiki.

 

 

Uhusiano wa kadiri na mume

“Ziokoeni nafsi zenu na watu wenu kutokana na moto”

(66:6)    

Mwanamke anapoingia kwenye maisha ya ndoa bado anakuwa na athari za maisha yake ya nyuma kabla hajaolewa ama kisaikolojia ama kitabia, kwa hivyo hapa itambidi abadilishe maisha yake, fikra zake na mazowea yake kulingana na mahitaji ya jambo analofanya na mumewe, na kwa tabia ya mwanamke iliyo, hawezi kuathirika haraka, kwa hivyo itampasa aanze safari ya kujibadilisha yeye mwenyewe kwanza subira na upole. 

Mwanamke asikate tamaa kwa uzito atakaopata wa­kati atakapokuwa akijirekebisha ili aende sambamba na maisha yake mapya.

Hapa kuna baadhi ya mambo muhimu ambayo yatamfaa mume na mke wakati wa maisha yao ya ndoa.

1.         Lazima pawe na lugha moja katika masuala mbali mbali na hivyo kuwe na majadiliano ya kifikra, kisiasa na kidini baina yao.  Na ikitokea mume akawa amemshinda mkewe katika mojawapo ya mambo haya, basi itambidi mke afanye bidii sana ili afikie kiwango cha mumewe, na vilevile mke akijiona anamshinda mumewe basi na amsaidie bila ya kujidai  ili mume afikie kiwango chake.

Ni lazima mke ajue kuwa uhusiano wa kitandani tu hautoshi, kuimarisha uhusiano wao bali yapasa kuwe na uhusiano wa kimapambano.

2.         Mwanamke mwanadini ajigeuze polepole kuwa sekretari wa kidini wa mumewe, amuandalie mazingira ya kumshujaisha mumewe atekeleze vizuri kazi na wajibu wake kama na kujisomea, kufanya kazi za huduma kwa jamii na nyinginezo, ampangie vizuri ofisi yake vile ipasavyo na akimkumbusha miadi yake na mtu, na mengineyo, lakini wakati huo huo asipekue na kuangalia vitu ambavyo mumewe hataki avione, kwani kuvumbua siri za mumewe ni haramu kisheria na lazima kutaleta madhara kwenye uhusiano wao.

Kuna msemo maarufu usemao “Nyuma ya kila mtu mashuhuri kuna mwanamke” kwa hivyo yapasa mwanamke mwanadini awe nyuma ya mumewe mwanadini ili awe mashuhuri mbele ya Mwenyezi Mungu na historia.

3.         Kuwe na kusaidiana baina ya mume na mke katika mambo yote yawe ni ya kidini, ya kinyumbani au ya kibinafsi, kiasi kwamba kuwe na raghba ya kila mmoja kumsaidia mwenzake.

4.         Mke apunguziwe mizigo ya kazi za nyumbani ili aweze kubeba vizuri kazi za kidini.

5.         Washirikishwe katika kazi za dini kama vile kutengeneza mafaili yanayohusu mambo maalum.

6.         Wafanye kikao rasmi juu ya kazi za dini na kila mtu maazimio yake yaheshimiwe.

Ewe Mola! Tupe katika wake zetu na watoto wetu viburudisho vya macho yetu na utujaalie tuwe viongozi wa wacha mungu.                                                     (25:74)

 

 

Wajibu wa kila mmoja (binafsi)

Kila mwanamke mwanadini inapasa pamoja na majukumu yake ya kijamii awe na majukumu yake binafsi akiyatekeleza kipekee nyumbani au mahali pengine.

Majukumu hayo ni kama ifuatayo:

1.         Upande wa uandishi, mathalan, utungaji, uandishi wa makala na barua kwenye magazeti au vilevile kukusanya habari za magazeti kwa kifupi na kuandika kanda zilizorekodiwa (khutba n.k).

2.         Kupiga chapa ya tapureta

3.         Kutayarisha mafaili ya kuhifadhia matukio muhimu yale atakayoyaona kuwa yana faida

4.         Kujisomea kila siku.

Wajibu wa pamoja

“Sema : “ Fanyeni (kwa pamoja) ”                           (9:105)

Kabla hatujazungumza chochote kwenye suala hili, ni lazima kwanza tusisitize kwamba kufanya kazi kwa pamoja ni jambo linalohitajika sana katika mkondo huu wa historia ya umma wetu, kwa sababu umoja huzidisha nguvu kutokana na uwingi na kwamba Mungu yu pamoja na wengi.

Mtume alikuwa akisema mara kwa mara!  “Wawili ni bora kuliko mmoja, na watatu ni bora kuliko wawili, na wanne ni bora kuliko watatu”.

Hapa, hata hivyo, kuna swali; hebu tufaradhie kuwa kuna wasichana wanadini ambao wapo tayari kushirikiana, lakini je majukumu gani watakayoweza kuyatekeleza?

Jibu ni kwamba, majukumu watakayohitajika ku­yatekeleza ni haya:

1.         Kuunda jumuia za kusimamia mambo ya dini, utafutaji pesa, muongozo na kuihamasisha jamii.

2.         Kuunda jumuiya za kujitolea kwenye mambo ya kheri, kukusanya michango, kutoa misada na mengineyo.

3.         Kuendesha mambo ya kielimu au ya kijamii k.v. kusimamia msikiti, kumbi za mikutano, maktaba, n.k. vilevile kutoa jarida maalum kwa mwanamke hata kama kwa kuanzia watoe vijinakala tu.

4.         Kuandaa safari zenye manufaa.

5.         Kushiriki kwenye harakati zote kwa ujumla, maandamano ya kidini n.k.

Haya ndiyo yapasayo kufanywa nao kwa ushirikiano katika  kutekeleza wajibu wa pamoja.

Na ni vizuri tueleze hapa ya kwamba kushirikiana pamoja kati ya mwanamume na mwanamke na huku wakichunga sheria – sio kuwa inafaa tu bali pia ni muhimu sana.

 

 

Ratiba kwa Vijana

Imam Ali amesema:  “Waangalieni sana vijana, na hasa wale wadogo…”

Amesema pia:  “Moyo wa kijana mdogo ni kama ardhi ambayo haijalimwa, kila utakachokipanda kitapokewa (kitamea).”

Kwa hivyo kuwashughulikia wavulana na wasichana ni muhimu sana kuliko kuwashughulikia watu wazima, haifai kuwatelekeza kwa sababu ya umri wao mdogo, huenda ikawa msichana aliyeshikamana na dini wakati wa udogo wake akawa ana nafasi kubwa na akaweza kutoa huduma kubwa sana kwenye njia ya Mwenyezi Mungu.

Kwa maana hiyo mwanamke mwanadini ni lazima awajibike katika kusimamia malezi mazuri na ya kimapinduzi kwa wasichana. Lakini je ratiba ya kazi hiyo ni ipi? Na itafanywaje?

Majibu yake ni kama ifuatayo.

1.         Suala zima la kuwaweka pamoja. Ni lazima kuwe na jumuiko litakalounganisha wanawake na wasichana; na hilo litapatikana kwa njia ya kuwafundisha Swala, au tafsiri ya Qur’an, au masomo mengine, vilevile kuwapa mafunzo ya ushonaji, upishi na mengineyo, bila ya kusahau jumuia za kila wiki za kujitolea.

2.         Kupanga nyakati. Ni lazima kupangwe njia maalum za kuzifuata, kwa kupanga vipindi maalum; mathalan, kipindi cha miezi minne ya kwanza kipangwe ni cha kuinua kiwango chao cha masomo kwa daraja maalum. Kisha miezi minne ya pili: kuwajenga wawe wana tabligh, lakini haipasi kuwafahamisha muda.

3.         Mbinu na mfumo mzima kwa ujumla.

Kinachotakiwa katika sehemu ya kwanza ni kujenga urafiki na wasichana na kujaribu kuwapa umuhimu zaidi katika mazungumzo nao ya ana kwa ana. Ni lazima kwanza vitayarishwe vitabu na kaseti  zifaazo kwa kila awamu; mathalan, wale wa awamu ya kwanza watayarishiwe vitabu vya Hadithi na kaseti zinazolingana na umri wao, na kuwafanya wawe na ushindani kati yao kwa kuwawekea zawadi kwa washindi.

Vilevile wazoezwe kutekeleza majukumu yao wanapokuwa majumbani mwao kama vile kuandika, kupeana kaseti, kusoma majarida na kurekodi kanda.

Vilevile kazi za nje, kama mihadhara, kutembelea wagonjwa na kupanga safari maalum za wanawake.

Huu ndio mfumo mzima anaopaswa mwanamke aufuate ili awe kama anavyomtaka Mwenyezi Mungu awe mwanzilishi na mbebaji wa ujumbe, lakini mfumo huu unahitajia ratiba maalum ya kuufuatilia, tunamshukuru Mwenyezi Mungu wa viumbe vyote.

 

 

Kuhusu mwanamke

Hao… wanataka kutokomeza familia…

Familia inapokuwa imejengeka kwa misingi ili­yowekwa na uislamu, basi inakuwa imara na yenye mshikamano na hivyo ni muhali kuisambaratisha.  Na familia inaposhikana kiasi hiki watoto hukua katika mazingira ya kidini wakiwa na pambo tukufu; na hii inafanya jamii kuwa ni yenye kuhifadhika na upotofu kusambaratika na kufanywa watumwa, na sote  tuna­jua kwamba kusambaratika ndiyo kipimo cha nguvu ya ukoloni.  Mason, ili kufikia hilo wanasema.:

“Ili kuleta mtafaruku baina ya mtu na ukoo wake, itawabidi muziondoe tabia nzuri zao tangu shinani, kwani kwa hio nafsi zinaelekea kwenye kuvunja udugu na kuingia kwenye mambo yaliyoharamishwa, na kwa sababu watu hao wanapenda sana domo kaya kwenye mikahawa na kuwacha kusimamia familia zao; watu kama hao  ni rahisi sana  kuwarubuni kwa kuwapa nyadhifa na mishahara kutoka kwa Mason kisha waonyeshwe ugumu wa maisha ya kila siku (ndipo mtawapata).  Na pia watengeni watu wa aina hiyo na watoto wao na wake zao na muwatupe kwenye anasa za maisha ya kinyama. [6]

Wazayuni nao (kwa lengo hilo hilo) wanasema:  “Lengo hupatikana kwa mbinu, kwa hivyo inatupasa tuangalie wakati tunapofanya njama zetu, tusi­wafuate wale watu wema wenye tabia nzuri watu wengi wamepotezwa na pombe na vijana kuwa ma­chizi. Hii ndiyo mbinu iliyotumiwa na maajenti wetu, waalimu na watumishi, vilevile wafunge kwenye nyumba za kitajiri, waandishi wetu, na hata wanawake wetu kwenye majumba yao ya starehe. [7]

Hata wana wa Nazi nao walikuwa na mwito wao; “sababisha chuki ndani ya ukoo ili uusambaratishe”

Kwa hivyo, utaona kwamba nadharia zote za kikoloni mwito wake ni ‘kuuteketeza ukoo na majivu yake kuyatupa baharini”.

Nchini Merekani, Wazayuni wanahimiza kila kinachoitwa ‘ndoa ya pamoja’. Yaani wakusanyike wanaume watano na wanawake watano, kisha waozwe wote pamoja kwa ‘tamko’ moja tu la ndoa, halafu inakuwa mwanamke mmoja ana waume watano, na mwanamume mmoja ana wake watano.

Ulaya ya mashariki nako (kwa walahidi) [8] wanadai kuondoa sheria zilizowekwa na dini kuhusu ndoa na kuchukua mfumo wa ‘ndoa ya pamoja’ uliopende­kezwa Uingereza. Na nadharia hizi hivi sasa zinae­nezwa kwetu; je kwa kiasi gani tutaweza kuzipinga?

Jibu: Uthabiti  wetu na upingaji wa nguvu dhidi ya nadharia hizi za kikoloni ni lazima ushikamane na dini na desturi zake.

 

 

Mwanamke huchinjwa vipi?

Huku akiwa amefanikiwa na shuka nzito yenye nembo za kijani na weupe, wamemchukua mwanamke, na kumpeleka kichinjioni ili asihisi maumivu ya kifo. Wametumia neno ‘uhuru’ wakampokonya mwanamke uhuru wake, na mwili wake wakaufanya bidhaa yenye kuvutia kwenye mashirika ya biashara ya ngono! Ndiyo ni kweli kwamba hawakumtungika msalabani, lakini wamemfungia njia ili afuate mwe­nyewe kwenye biashara ya utumwa na ajiuze mwe­nyewe kwa wateja.

Wametumia neno ‘penzi lisilo la kuingiliana’ wa­kamsukuma msichana mdogo kwenye makao ya haramu na kumfanya achukue tembe za kuzuia mimba ndani ya madaftari ya hesabu anapoingia chuo kikuu kusoma.

Wametumia neno ‘kufanya kazi’ wakawapeleka wake za watu kwenye mikono ya wanaume baki vichochoroni bure!

Na wametumia neno ‘mchanganyiko wa ki-heshima’ kwa kuunda kizazi lanisi, kisicho na mwenendo wala afya nzuri, na mamilioni ya wanaharamu kwa mwaka mmoja tu!

Lau ningeliambiwa nichague jina la enzi hizi zetu ningechagua ‘Enzi za upotofu na uchizi uliosindikwa ndani ya maneno matamu”.

Hebu angelieni huku na huko, hivi kweli kuna fikra iliyobaki bila ya kusindikwa (kutiwa) ndani ya maneno matamu?

Zamani neno ‘zinaa’ liliwaogyofiya wasichana kama makali ya kisu; wakalibadilisha neno hilo kwa neno ‘uhuru wa mapenzi’ ili asiogope!

Neno ‘msago’, wakalibadilisha kwa ‘penzi la penzi’ ili liwe tamu na lipendwalo!

Neno ‘mwanaharamu’ lilikuwa lina aibu kwenye jamii, hivi sasa limekuwa ‘mtoto wa kimaumbile’ ili asionewe haya na mtu yeyote!

Basi, kama yalivyobadilika maneno, na mtazamo wa jamii pia umebadilika. Mwanzo mtazamo wa jamii ulikuwa mzuri, wenye mshikamano kisha ukawa umepotea, umezama kwenye taabu na masumbufu.

Zamani msingi wa jamii ulisimamia kwenye imani, mapenzi na utangano, uchu na uhalifu.  Hivi ndivyo mwanaadamu walivyomuuwa kwa mwanadamu.

Ee chonde wanaadamu!

Safari ya ki-chizi inaelekea wapi?

Safari hiyo inayoanzia kwenye Mini inaishia wapi?

Jambo hili si gumu kama hesabu, tujumlishe, tutoe au tugawanye ndipo tupate majibu, la; majibu ni hali halisi kama tunavyoiona hivi sasa kwenye jamii ya kisasa inayoishi kwenye enzi hizi za upotofu wa kijinsiya na ufuska.

Kwa mtazamo wa haraka haraka tunapoangalia ndani ya jamii za kisasa tutagundua mambo yenye kuogofya yafuatayo:

Safari yenyewe hawaanzii kwenye Mini kama inavyodaiwa, bali inaanza pale mwanamke anapo­anza kujionyesha nywele na sehemu zingine.

1.         Kisha safari hiyo huendelea mpaka kufikia kwenye Mini ambayo itaonyesha miguu.

2.         Kisha inaendelea mpaka kufikia kwenye Micro, ambayo  iko senti mita ishirini na nne juu ya magoti.

3.         Haishii hapo, kisha inaingia kwenye ‘stesheni’ ya Short (bukta) karibu na kwenda uchi

4.         Kutoka hapo inasimama kwenye ufuo wa bahari kwa kustarehe kijinsiya kufanya mapenzi na kuoga maji ya moto (k.v. Sauna n.k.)

5.         Kisha inafikia kwenye vilabu vya watembea uchi (Niudists) kama walivyozaliwa.

6.         Kisha wiki nzima kwenye vilabu vya ngono zisizo za kawaida na kwenye maandamano ya mashoga na wanawake wanaopenda jinsiya na wake wenzao wakidai haki zao za kufanya mapuuzi kwa uhuru!

7.         Kutoka hapo anafikia kwenye kujianika uchi na wenda-uchi wenzake kwa muda mrefu mabara­barani, viwanjani na hata kwenye mabwawa ya kuogelea.

8.         Kuishi hatua za mwisho mwisho ni uvutaji wa bangi , hashish na ‘unga’ (heroin)

9.         Mwisho wa safari ni kuharibika akili, wazimu na kujiua kwa pamoja .

Safari hii mbaya haichukui muda mrefu kufika, lakini kwa kweli inachukuwa maisha ya watu wengi mno katika jamii. Isitoshe ni safari moja lakini yenye vituo kumi ambavyo mtu lazima avipitie vyote kimoja baada ya kingine bila ya kuviacha vingine kwa sababu ‘orodha’ yake ni moja tu haiepukiki.

Wasomi wa elimu ya maadili wanasema:  “Ngono ina­pelekea mtu kufanya nyingine, tendo la haramu ni su­maku ya kuvutia lingine la haramu, na kuvama kwenye maAsya kuna sababisha kuvama zaidi kwenye maAsya”. Na kama wasomi hao hamuwaamini, macho yenu je?

Hebu njooni, kisha tuinue shingo zetu kidogo tuiangalie jamii hii ya kisasa ‘ya viwanda’ ambayo inatukuza mitambo tu bila ya kujali gharama ya utu wa binadamu ambao umezidi kuzorota siku baada ya siku mbele ya moshi wa viwanda. Hebu njooni tuangalie takwimu zinavyoonyesha.

Nchini Ufaransa kuingiliana ngono, kinyume na maumbile kunafanywa bila ya kuona haya.  Wana­sema wake nchini humo “Baada ya yote hayo, tuna wanaume wengi wa nje tunaowazalia watoto”[9]  Nchini humo, mtu haoni vibaya kujichua, kufanya ulawiti, kuingiliana na wanyama na midomoni amba­ko huko ndiko kunapendezwa.  Na huko Merekani, nako, mwanamke kwenda uchi ndiyo maendeleo na kunakubalika na kupigwa picha za jinsiya sehemu moja moja imekuwa pia ndio maendeleo.

Katika ripoti ya kila mwaka, imeelezwa kwenye mwaka 1965 ya manispaa ya mji wa San Fransisco, jimbo la Carlifornia kuzidi kwa makosa ya kijinsiya na kwamba, matoleo ya picha chafu za kijinsiya na watumishi wa nyumbani na wahudumu wa mahoteli walio vifua na mapaja wazi wanapohudumu wamezidi mno.  Vilevile pana wasichana wanaojionyesha mili yao uchi, mihadarati, na ulawiti kwa wanaume wamefikilia nusu milioni mwaka huu.”[10]

Safari hiyo ya wendawazimu inaendelea nchini Marekani, hebu angalia”

“Maofisi wa polisi walivamia ghafla jumba moja jipya liliopo mjini Atlanta, Georgia wakafanya msako, na wakapata mafaili ambayo inakisiwa kuwa ni ya kilabu cha kubadilishana wake! Msemaji wa polisi alinukuliwa akisema kwamba:  “Kuna jarida linalotolewa na kilabu hicho lisemalo kwamba mlango wa kilabu u wazi kwa makapera na walioowa, wake kwa waume, na kwamba kilabu hicho kina matawi yake mjini New York, Chicago, Dallas, Orlando na Florida”.

Polisi mwingine naye anasema:  “Kitendo cha ku­badilishana wake kinazidi kuongezeka siku baada ya siku katika kilabu hicho.

Huko Sovieti safari hiyo potofu inaishia kwenye talaka, kwenye gazeti litokalo nchini humo la Pravda kuna makala maalum iliyoandikwa na mtaalamu wa mambo ya jamii Dkt Kharshev isemayo:  “Katika kila watu kumi, watu tisa huwachana kwenye nchi za umoja wa kisovieti na sababu kubwa ni kuharibika kwa tabia na ulevi wa kupita kiasi. Na asilimia themanini ya uhalifu unaotendwa na vijana wadogo unatokana na kusambaratika kwa familia, vilevile wengi wanaoana hawaishi pamoja zaidi ya miaka mitatu au hata baadhi yao kwa miezi au wiki chache tu.”[11]

Nchini Uingereza, ripota moja wakike wa jarida moja la kiarabu, ameeleza kwamba siku moja alikwenda nchini humo na kupokewa uwanja wa ndege na rafiki yake wa siku nyingi: alipomuona tu kitu cha kwanza alichokigundua kwa rafiki yake huyo ni kubadilika kwa sura yake ambayo mwanzoni ilikuwa nzuri na kuonekana mzee! Akataka kujua sababu iliyomfanya azeeke mapema hivyo akiwa na umri wa miaka ishirini na mitano tu; alimjibu:  “Ah, kwa sababu ya matatizo mengi ya kisaikolojia”. Akamuuliza:  “kulikoni, mumeo kakuwacha na kuchukua mrembo mwingine nini?” Akajibu!  “Ndio kaniacha, lakini siyo kwa ajili kapata mrembo mwingine, la bali mwanamume kama yeye! Yule mwandishi alishangaa mno:  “Nini? Mwanamume kama yeye?“  Akajibu:  “Ndiyo, ame­kuwa mlawiti.”

Mwandishi huyo anaongeza:  “Wimbi linaloikumba jamii ya Uingereza ni hilo la mapenzi ya waume kwa waume, na utaweza kufahamu hilo kwa kuangalia matangazo yake kwenye majarida. Ikiwa zamani mwanamume alikuwa akitaja sifa anazotakiwa awe nazo mwanamke anayetaka kumuoa, ama hivi leo atatoa sifa za mvulana anayetaka kumuoa! Zamani msichana anapotafuta mchumba hujitaja sifa zake gazetini, mathalan, msichana, umri miaka kumi na nane rangi ya nywele: kahawia, elimu: chuo kikuu: angependa kuolewa na mume aliye chini ya miaka thelathini n.k leo hii mvulana ndiye anayejitangaza, mathalan, umri miaka ishirini rangi ya nywele; nyeusi, rangi ya macho; kijani.  Elimu: mwanafunzi wa mwaka wa tatu wa chuo kikuu, angelipenda ‘kuolewa’ na mume asiyezidi miaka hamsini… n.k.!

Je, si nilikwambia safari ya upotofu ni moja tu, mtu hawezi kufuata njia amoja akaacha nyingine!

 

 

Barua ya haraka kwa msichana wa karne ya ishirini na moja.

Kwako msichana wa karne ya ishirini na moja.

Wale wanaopigania uhuru hawakupiganii wewe, ati mwanamume fulani apigania uhuru wako kama unavyofahamu, sivyo, bali hao wenye njaa wanapi­gana wapate uhuru kwenye mwili wako wakuvutia, au ati mwanamke fulani atake uwe huru kwa sababu yeye yuhuru, la hasha, anachotaka ni kukuingiza wewe uwe pamoja naye katika pepo hiyo na mapo­chopocho, yeye anapotea na ataka wewe pia uanguke kwenye shimo la maovu kama yeye ili umuondolee hisia zake za kujiona yuko peke yake katika maovu hayo.

Hebu peleleza maisha yao hasa hao wanaopigania uhuru ugundue ukweli ulivyo: kwa hakika wote hao wana maovu yao wanataka kujificha uovu wao chini ya joho tukufu, na inaweza kuwa wana kasoro katika namna ya kufikiri au kwenye  mambo mengine.

Pengine mtu anaweza kuwa kama Bw. Sartre anaye­pigania ‘uhuru’ akiulizwa nini maana ya uhuru, anasema:  “Ni mwanamke awe na uhuru wa kufanya mapenzi na kila mtu.”  Anapoulizwa ‘hata mkeo’ Anajibu, ndiyo, hata mke wangu akipenda kufanya hivyo.”  Baadaye watu walipo yachunguza maisha yake ya utotoni waligundua kuwa alikuwa na kasoro.[12]

Au pia inawezekana mwanamume akiwa ni wa aina nyingine mathalan, aina ya wale ambao mkewe au mabinti zake wana kasoro, au anataka tu tustarehe na wanawake wengi kwa masaa tu na kuwapokonya maua ya maisha.

Au pia inaweza kuwa ni kwa sababu nyingine; almu­radi ni lazima utambue kuwa hakuna ‘anayekupi­gania’ uwe huru. Na jichunge sana usijaribu kuingia kwenye janga lolote, kwani utapotea.

Ukitawaliwa udhihirishe uso, nywele au mguu wako ‘kidogo’, usisadiki kwamba yataishia hapo tu bali yatafikia mahali ambapo hapana mwisho mwema.  Unataka nikupe dalili?

Hebu chukua jarida lolote dukani uliangalie, kwa haraka kitu utakachokiona ni wasichana wadogo ambao kila mmoja wao aweza kuwa ‘mama’ na akai­shi maisha matulivu ya ndoa, lakini wameufuata mwito wa kuonyesha nyuso, nywele na miguu ‘ki­dogo’ na wakaukubali mara tu baada  ya muda mfupi walipogundua, tayari wameshakuwa ‘wasi­chana wanaohitajika wakati wa haja’, Ee Mungu azirehemu enzi za utawa (za zamani)!

Na msichana anapokuwa chombo cha kutumiwa kwa matamanio ya wengine anapoteza thamani yake, hata wewe rafiki wajua vizuri hilo. Na hata mwanamume anayemtafuta msichana kama huyu humpenda kwa muda mchache tu unaoteketea mara moja tu na kuwacha moshi mzito unaompoteza msichana huyo, na anapokufa hakuna hata mtu mmoja atakayemlilia. Ndiyo, ni kweli kwamba pengine utajisikia hamu ya jinsiya na ikawa inaweza kupatikana lakini ole wako usikubali kujiingiza kwenye hiyo. Kwani njaa yako yaweza kuwa ya uwongo na kuukosa heshima yako ya kike ni ukweli kabisa. Na mwanamke anapoukosa uwanawali wake basi haupati tena, au sivyo!

Dada mpendwa, wakikuhadaa ufanye kazi kiwandani au ya safari na utapata mshahara mkubwa uweze kukidhi mahitaji yako na ya watoto usiwasadiki kwani nia yao si wewe uchume bali nia yao wakupate kum­buka ya kwamba asilimia themanini ya wanawake wafanyao kazi viwandani nchini Merekani wame­sinywa na kazi, kama ripoti zinavyoonyesha.

Na kumbuka pia ya kwamba mwandishi wa kike maarufu, Helen Michel amesema kwa uhuru, maendeleo ya ki uchumi na nafasi za kimataifa ali­zozipata mwanamke wa Ufaransa hazijamkwamua kutokana na matatizo yake mazito na wala haziku­badilisha hali yake na kuweza kupeleka jahazi la mai­sha.

Isitoshe, hakuna anayekupenda sana zaidi ya Mwenyezi Mungu aliyekuumba kwa hivyo usitende ila yale anayoyasema.

 

 

Kuiga:  Maafa ya Ulaya Mashariki

Watu wa Ulaya mashariki walipojitenga na dini tu, hadhi yao ikaporomoka wakawa ni wenye kuiga tu. Wengine nao walipofika mwezini, vijana wetu nao wakavutiwa sana na hilo wakasoma magazeti yao ili wapate ramani iliyowafikisha huko mwezini lakini hawakuipata, ila tu waliambulia bimbiriza – mavi, habari za vijana wa Pop Music na, fikra ya uhuru, wao wakadhani mambo haya ndiyo ramani ya kufika mwezini. Wakaacha kila kitu.  Wakavaa mavazi ya kike! Jee hii si aibu?

Hapana, maadam Waamerika wanafanya basi si aibu, si wao wamefika mwezini? Hayo ndiyo maneno yao.

Wengine wamefika kwenye safari ya Mars, vijana wetu pia wakavutiwa na lilo, wakasoma magazeti yao, wakapewa, wakipata “Sandwichi za kisaikolojia” zenye alama nyekundu na manjano wakadhani kula sandwich hizo ishirini kunatosha kumpeleka mtu kwenye Mars, wakamiminika madukani kuzinunua kwa fujo, mwishowe walicheza shere dini na maadili mema.

Walisikiliza idhaa zao wakasikia kwamba “kwa hakika hakuna misingi thabiti au ukweli unaopelekea kuwa na tabia njema, bali tabia zenyewe zinabadilika kutokana na jinsi hali za kijamii zinavyogeuka chini ya athari za kiuchumi, na kwamba fikra za  binaa­damu ni chombo kinachofuata maada tu (dunia) na vivyo hivyo mfumo wa kitabia ni chombo kingine cha ki-maada tu.”

Vijana wetu wakashikamana na fikra hizo kama wahyi ulioshuka, wakawa  wanaishi na familia na jamii zao kwa kutumia falsafa hiyo mbovu, wakaa­nguka kwenye mlizamu (mfereji wa maji ya mvua) badala ya kutua mwezini na kwenye Mars. Ikawa kisa  chao hiki kinafanana na kisa cha bwana mmoja aliyepata madaraka makubwa katika jamii, wenzake wakataka kujua sababu hasa iliyomfanya apate madaraka hayo, baada ya kipindi kidogo  cha uchunguzi wao, mmoja wao akadai kwamba ame­gundua sababu, akawaambia wenzake, “nimegu­ndua sababu iliyomfanya mwenzetu awe na mada­raka ni kuwa kila anapoketi mahali huchezesha ki­dole chake gumba cha mguu kwa vidole vyake vya mkono na kulia! wenzake hao wakaingilia kujichezeachezea vidole vyote vya miguu, wakiwa na ndoto ya kubeba wadhifa mkubwa kama mwenzao!”

 

 

Kupanga uzazi…  Kwa nini?

Mnamo mwaka 1965 huko Bombay, India, kulianzi­shwa shirikisho la kimataifa la kupanga uzazi (Fa­mily Planning), ambalo baadhi ya nchi za kiislamu zilijiunga.  Sababu walizozitoa za kuanzishwa kwa shirikisho hilo ni  kama ifuatayo.

1.         Tatizo la makazi

Ongezelo kubwa la watu duniani kila mwaka halilingani na uzalishaji mdogo wa chakula duniani, kwa hivyo ni lazima kupunguza ongezeko hilo ili kujiepusha na njaa.

2.         Umuhimu wa malezi ya watoto

Familia inayoweza kulea watoto watano mathalan katika hali ya kawaida , itaweza kulea watoto wawili kwa vizuri zaidi.

3.         Kuinua hali ya maisha

Familia yenye kipato cha chini haiwezi kukidhi mahitaji ya lazima kwa idadi kubwa ya watu iliyonayo.

4.         Kumkomboa mwanamke kutokana na maju­kumu ya ulezi katika kupanga uzazi kuna uhu­siano mkubwa baina ya mwanamke kuzaa sana kukombolewa kwa sababu mke mwenye mtoto mmoja anaepukika na ulezi wa mtoto kwa zaidi ya miaka mitano, hivyo anakuwa amepumzika na majukuma yake.

Hizi ndizo sababu kuu wanazozitoa hao wanao­pigania na kusimama upangaji uzazi. Nasi tunajibu hapa kwa ufafanuzi:

1.         Kuhusu tatizo la ongezeko la wakaazi, hilo halipo ila kwao hao wanaodai hivyo, dunia, kama tu­juavyo, ina uwezo wa kuzalisha chakula mara­dufu ya mahitaji ya wakaazi wake; kwa hiyo hakuna hoja ya kwamba ni dharura kupigana vita ku­maliza watu kwa ajili ya maisha yao!

2.         Kuhusu malezi ya watoto, haya ni madai ya fitna tu kwani malezi ya watoto hayana uhu­siano wowote na kuzaa watoto wengi au wachache kwani familia ikiwa nzuri inaweza kulea idadi yoyote ya watoto, na ikiwa mbaya haiwezi kulea hata mtoto mmoja. Isitoshe, ku­kata kizazi ni kosa kubwa kwa jamii ya watu, kwani inawezekana, pengine yule mtoto, aliye­zuiliwa na mamake asijaliwe, angelikuwa mtu mkubwa sana katika jamii kama angeachiliwa aishi.  Angalia, lau Abu Talib, babaye Ali bin Abi Talib angefunga kizazi chake baada ya ku­zaliwa Aqil (kakake Ali) je ni kosa kubwa kiasi gani angeliifanyia jamii ya watu.

3.         Ama kuhusu kuinua hali ya maisha, inaweza kuwa hoja sahihi kama watu kuangalia kwa makini na kwamba mikutano ya kimataifa iweze baada ya kulipa umuhimu suala la ‘kupanga uzazi’ wangelipa kipaumbele suala la kuongeza makao ili yalingane na jinsi watu wanavyoongezeka.

4.         Na kuhusu suala la kuhusisha upangaji wa uzazi na ‘kumkomboa’ mwanamke ni kweli lakini nani kasema kwamba inapasa mwanamke ajikomboe na majukumu na wajibu wake? Kuzaa kwa mpango si jambo lililo chini ya uwezo wa mwanamke tu, bali ni jambo lilio chini ya uwezo wa jamii, na jaribio lolote la kuzuia wasizaliwe watu wema kwa jamii ni kwenda kinyume na ubinaadamu wote ambapo huko kumkomboa mwanamke kwa maneno mengine, tayari anakombolewa kwa kuwaweka vifaa ili kumrahisishia kazi.

Hizi ndio sababu wanazozitoa, (tulizozijua) kwa ajili ya kupanga uzazi.  Na maadam sababu hizi hazina hoja ya nguvu, basi nasi ni haki yetu kuuliza swali hili: hawa wanaofanya kampeni  ya kupanga uzazi wanakusudia nini? Je kweli wanataka mwanamke aende kulingana na ratiba iliyopangwa ya malezi mazuri zaidi ili aweze kutoa huduma nzuri zaidi?

Mmoja kati ya viongozi wao, katika nchi moja ya Kiarabu anajibu “kwa hakika kazi ya kufanya kam­peni ya upangaji uzazi lengo lake kubwa ni kuondoa desturi walizonazo watu; na ili tuweze kufanya kazi hii barabara ni lazima tuondoe zile fikra zinazo­kwamisha mpango huu”

Lakini bwana huyu hayaweki wazi maneno yake juu ya hizo anazoziita ‘fikra’ hizo ni fikra za kiislamu, na desturi hizo ni yale maadili na tabia za familia za kiislamu.

Ama njia ya kuziondoa ni kujaribu kutia shaka ndani ya Uislamu na kuileta misingi ya mambo ki­maada (kidunia), ya kilahidi badala ya maadili ya kiislamu. Jambo la kushangaza ni kwamba wale wanaoshadidia mambo ya kupanga uzazi hawaoni umuhimu wowote wa kuenea ukahaba, kama ambavyo zile nchi zinazokampenia upangaji uzazi hazijaribu hata mara moja kuzuia ukahaba.

Je nini maoni ya uislamu katika kupanga uzazi?

Bila shaka uislamu haukubali kupanga uzazi kwa ‘mwito’ wowote ule.  Kuna wale wanaopotosha hadith ya Mtume (s.a.w) isemayo:  “Oaneni mzaane ili mpate kuwa wengi, kwani mimi nitajifaharisha kwa watu wa umma zingine siku ya kiyama hata kwa mimba iliyoharibika.”  Watu hawa wanadai kuwa makusudio ya Mtume kusema ‘mpate kuwa wengi’ siyo wengi wa idadi bali wa aina fulani.  Ndiyo, ni kweli uislamu unataka kupanga, lakini nani aliyesema uislamu unataka kupunguza kwa mpango, na si kuongeza lakini kimpango?

Ama ile hadith ya Mtume makusudio yake si ‘aina’ (kama wanavyodai) itakuwa na uhusiano gani basi juu ya kujifaharisha Mtume na aliposema mpate kuwa wengi na aliposema hata mimba iliyoharibika?

Kuhusu suala la ongezeko la wakaazi, uislamu umekuja na masuluhisho ya aina mbili

1.         Ufafanuzi wa ki-ujumla

2.         Ufumbuzi maalum wa hali halisi

Kabla hatujafafanua juu ya ufumbuzi wa kwanza ni lazima tukubali kwamba Uislamu umeruhusu baadhi ya familia kupanga uzazi.

Katika maoni ya Uislamu, Mwenyezi Mungu ameumba ardhi kulingana na wanadamu walivyo na daima kuna uhusiano baina ya mwili wa ardhi na mwili wa binaadamu kiasi kwamba haijatokea na wala haitatokea siku ambayo ardhi haitamtosha mwanaadamu vilevile, mazao ya dunia daima yana­zidi mahitaji ya mwanaadamu hata kama watazaana kwa wingi.  Qur’an inasema: 

“Na Mwenyezi Mungu amekuumbieni wake kwa jinsi yenu, na akakujaalieni kutoka kwa wake zenu watoto na wajukuu, na akakuruzukuni vitu vizuri vizuri.  Basi je, wanaamini yasiyokuwa ya haki na kuzikataa neema za Mwenyezi Mungu?”                                                (16:72)

Neema za ardhi hazitakuwa chache kuliko mahitaji ya binaadamu isipokuwa ugawaji mbaya na mpango mbaya wa miji kisiasa ndiyo mambo yaliyosababisha ugumu wa maisha ya baadhi ya watu.  Kuna baadhi ya nchi tajiri zenye ardhi zenye rutuba, madini na utajiri wa mali asili, na hali watu wake wanaishi maisha ya dhiki na mfumko mkubwa wa bei.

Pia kuna nchi zingine maskini zenye ardhi kame zinapatana na nchi tajiri lakini watu wake wana­taabika na ukosefu wa chakula, njaa na vifo.

Ufumbuzi wake ni mdogo tu, zile nchi tajiri zi­funguwe milango yake kwa nchi masikini na mipaka ya kisiasa iondolewe na mashirikisho ya kimataifa yasimamie chakula, hilo litafanya watu wote waishi kwenye ardhi moja wakistarehe na kuneemeka.

Nani aliyesema Amerika lazima kila mwaka iteke­teze tani chungu nzima za ngano ya zaidi; ambapo kuna watu duniani kiasi cha milioni moja wanaokufa kwa njaa na ukata?

Nani aliyesema mataifa dunia yatumie milioni ya mapesa katika mashindano ya kujilimbikizia silaha bila ya kujua hatima yake, na hali kuna watu wana­shindwa kupata mkate na tone la maji.

Takwimu za uchumi wa kijeshi na mashindano ya silaha duniani zinaonyesha kwamba gharama za matumizi ya kijeshi duniani zinazidi, kwa kiwango kikubwa, kuliko gharama za maisha katika sekta za kiafya, kielimu, chakula na kijamii.  Tarakimu hizo zinafafanua kwamba matumizi ya kijeshi duniani katika mwaka 1966 na 1967 yalifikia dola milioni mia moja na themanini na mbili ($182) kila mwaka, na kwamba kiwango hiki kitapanda hadi kufikia dola milioni mia nne na tisini na tisa ($499) kabla ya kufikia mwaka 1977.

Na kulingana na takrimu za shirika la UNESCO, Gemini News Service, England, matumizi ya kijeshi ya dunia yanazidi matunzo ya kielimu dunia kwa wastani wa asilimia arubaini (40%)

Miongoni mwa mambo yaliyofichuliwa na UNESCO ni kama ifuatayo:

1.         Gharama za kumsomesha shuleni mtoto mmoja kwa mwaka  hazizidi dola mia moja ($100) ambapo gharama zinazotumika kwa mwanajeshi mmoja tu praveti zinafika dola elfu saba na mia nane ($7800)

2.         Msaada (huo) anaotoa mtu katika nchi tajiri kuzi­patia nchi masikini hauzidi hata dola nane ($8), ambapo kwa wastani anagharamika zaidi ya dola mia moja na sabiini ($170) kwa matu­mizi ya kijeshi!

3.         Misaada ya kijeshi inayopokea nchi maskini ku­toka nchi tajiri imeongezeka.

Hii ni kuongezea kwamba bado kuna utajiri mwingi sana wa mali asili ambazo haujavumbuliwa au hauja­tumika, utajiri ambao wataalamu wanakisia kwamba utakapogunduliwa utaweza kumuongezea mahitaji zaidi ishirini elfu ya wakaazi duniani kwa kila wana­chokihitaji.

Hebu tuangalie utajiri ulioko baharini:

Kadri idadi ya watu inavyoongezeka duniani ndiyo matumizi ya nchi asili yanavyozidi kuongezeka kwa kasi na kwa wingi mno na watu wanaelekea zaidi ba­harini ambamo mna hazina kubwa sana ambayo bado haijatumika. Hivi sasa zaidi ya tani milioni hamsini za samaki huvuliwa kila mwaka na hiyo ni sehemu ndogo tu kama tone la utajiri ulioko baharini ambao kwa ujumla unaweza kufikia tani bilioni ishirini, mbali na mimea ipatikanayo baharini.  Bidhaa zina­zopatikana baharini zikitumiwa vizuri unaweza kuondoa tatizo la ukosefu wa Vitamin, Protini na ma­futa katika chakula cha binaadamu.

Isitoshe, baharini mna hazina isiyokwisha ya madini mbalimbali wachilia mbali hazina za meli na maja­hazi yaliyozama ambazo ni kidogo sana kulingani­sha na hazina zilizomo humo.

Chini ya bahari kunapatikana mabilioni ya tani za chuma na manganese, Nicel (madini kama fedha), shaba na madini nyingi mbalimbali.  Uvumbuzi wa hivi karibuni umeonyesha kwamba kuna hazina ya kutosha ya mafuta baharini, na dhahabu iliyomo chini ya bahari ikiwa itagawanywa itatosheleza kila mtu duniani ku­pata tani tatu.

Isitoshe, maji ya bahari yanaweza kuzalisha umeme katika siku zijazo

Ikiwa utajiri wa dunia ni mkubwa kiasi hiki kwa nini basi kuwe na kutaka kukata kizazi?  Uislamu una­posema ‘la’ hakuna kupanga uzazi hautegemei hoja tasa, bali ukweli ulivyo kwa dunia na watu we­nyewe.

Ah!  Mangapi mazuri yatapatikana lau uislamu uta­rudi?

Kuna mamia ya watu wanaokufa njaa nchini ya ki­vuli cha ulahidi.  Mamia wengine wananyimwa ki­bali cha kuingia kwenye maisha kwa ajili ya kile wanachokiita ‘kupanga uzazi’

Lakini, kwa sababu uislamu hauamini kama wanavyoamini watu wa ki-maada wa kisasa kwamba, mwanaadamu ni manyasi ya jangwani anayetoka tumboni kwa mama yake, si muhimu, awe na njaa, kiu, au hata afe..!

Kwa matazamo ya uislamu, mwanaadamu ana heshima yake maalum kubwa zaidi ya heshima ya dunia, hata kilenge kilicho tumboni kina heshima yake.  Kwa hivyo utaratibu wa kiislamu umetoshe­l­eza kila mtu maisha mazuri vyovyote itakavyo­kuwa.

Uislamu, kwa kiasi kikubwa, unafanya juhudi ku­muandalia kila mtu shughuli njema ili aweze kuitosheleza familia yake, na asipopata kazi basi mtu aliye karibu naye amsaidie kimaisha, si kwa hu­ruma na hisani, la, bali ni wajibu uliofaradhiwa na uislamu

Na kukiwa na familia maskini isiyo na uwezo na haina jamaa zakusaidia basi dola ya kiislamu ndiyo itakayowasimamia mahitaji yao ya kimalezi, kiafya na kijamii.

Maadam uislamu hautambui mipaka ya kikoloni baina ya dola za kiislamu, au hata mipaka ya duniani, na maadam mwanaadamu kwa mtazamo wa kiislamu ni ‘mwanaadamu’ basi nchi haziwezi kuwa na matatizo kwa wingi wa makazi.  Hebu tu­pige mfano, mathalan nchi ya Misri imezidiwa na watu kisha nchi ishindwe kuwatosheleza mahitaji ya lazima ya watu wake, hakuna tatizo, wafungulieni wamisri mipaka ya Sudan ambayo ina ardhi kubwa na hali nzuri ya hewa kisha muwagawanyie pesa za mafuta za Libya kisha muwaache wajiendeleze…!

Hii ni kwa upande wa kutatua matatizo ya kiislamu ki-ujumla.

Ama kuhusu kutatua matatizo yaliyopo hivi sasa, kile kinachotoa uislamu ni rahisi kupatikana.  Ardhi ya Kiislamu kama tujuavyo si ndogo bali ni kubwa na masafa yake yanatosha kwa kuishi na kuwaajiri watu wote duniani, isitoshe, ardhi hiyo si maskini kwa sa­babu ina madini, maji na rutuba.  Mwenyezi Mungu ameumba petroli sehemu nyingine na nchi nyingine hakuweka, vilevile kwingine ameweka mito na kwingine hakuweka; naye alipoumba hivi hakuweka mipaka bali alimwambia ‘hii ardhi ni kwa ajili yenu, shikaneni na muishi kwa amani’ bali watu ndio walioweka mipaka umma mmoja wakaufanya ziwe ishirini, na taifa moja wameligawanya kwenye mataifa ishirini.

Nasi si wajinga kiasi kwamba tupendekeze ufum­buzi wa tatizo la wingi wa watu kwa njia ya kuo­ndoa mipaka ghafla katika nchi za kiislamu, kwa sa­babu zoezi hilo si rahisi hivi sasa, kama si muhali.  Lakini pia sisi si wajinga kiasi kwamba tuamini kwamba haiwezekani kukusanya pesa za Kiislamu zinazotumika mahotelini kwa ufuska kwa ajili ya kufungua viwanda vikubwa ambavyo vitawaajiri mamilioni ya watu kwenye mji wa Kiislamu wanaotafuta chochote na hawakipati!

Kwa hivyo basi sisi tunapinga ‘kupanga kizazi’ kwa maana ya kuzuia watu wazaane kwa sababu hizo, upingaji huu unaukosea umma wa kiislamu ambao unabeba majukumu mazito ya ulimwengu, ya kuutoa kwenye udhalili na kuweka kwenye uadilifu, uhuru na amani, na kisha kumtoa mwanaadamu kumpeleka kwenye anga ambao hajaijua upeo wake, na hatuamini kama watu milioni mia nane wanatosha kutekeleza majukumu haya. 

Jambo la kushangaza ni kwamba propaganda za ‘upangaji uzazi zinaonge­zeka upande wa mashariki ya nchi za kiislamu kila kunapokuwa na mapambano kati ya nguvu za kiko­loni, kilahidi na waislamu, na hasa wanapohisi kuwa nguvu hizo zinashindwa kutokana nguvu za watu za wais­lamu.

Na jambo jingine la kushangaza utafiti juu ya ongezeko la wakazi katika nchi za kiislamu kwanza huonekana kwenye magazeti ya kikoloni nchi za mashariki na magharibi kisha unaonekana katika magazeti ya nchi za kiislamu na watu wakavalia ujinga?

Lakini msisahau kwamba Ulaya mashariki na uli­mwengu wa kiyahudi wanafanya juhudi kubwa ya kuongeza uzazi badala ya kupanga!

 
WAsya kwa mwanamke mu’min

Katika historia yetu adhimu, mwanamke ana sehemu kubwa na ya kijasiri, ambayo mara nyingine yamu­onyesha akiwa kwenye uwanja wa mapambano, na wakati mwingine kwenye medani ya kupambana na ubatili, kuanzia bibi Maryam, bibi Khadija, bibi Fatima, bibi Zainab, Ummu Ammar na wengineo.

Kwa kweli mwanamke, pamoja na kazi zake za kawaida bado ana kazi kubwa ya kupambana na kubeba mas’uliya (majukumu).  Wanawake wangapi walioviporomosha viti vya enzi vya mataghuti? Wanawake wangapi wameshinda madhalimu? Na kwa sababu hiyo, si ajabu kuwa katika Qur’an, neno kali dhidi ya ufalme na utaghuti lilitamkwa na mwanamke pale aliposema:

“(Malkia) akasema: 

“Hakika wafalme wanapoingia mji (wa watu) huuharibu na wanawafanya watukufu wake kuwa dhalili; hivi ndivyo wanavyofanya (daima).”                                           (27:34) 

 

 

Ewe mwanamke mu’min!

Daima kumbuka kuwa Mungu wako na Mungu wa mwanamume ni mmoja, na uwezo aliokupa wewe ndio aliompa mwanamume.  Majukumu mamoja, haki moja na marejeo yenu mwishowe ni mamoja tu.

Ama tofauti za ki-maumbile zilizoko kati yenu, hazimaanishi kwamba wewe ni madini ya feruzi (isiyo na thamani) na yeye ni almasi.  Nyote mwato­kana na Adam na Adam atokana na udongo.

“Enyi watu! Hakika tumekuumbeni kutokana na mwanamume na mwanamke.  Na tumekufanyeni mataifa na makabila (mbali mbali) ili mjuane.  Hakika ahishimiwaye zaidi miongoni mwenu mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule am­cha­ye Mungu zaidi..”                 (49:13)

Kuwa mume siyo fahari na ubora kama vile ambavyo kuwa mke si udhalili na aibu, bali kuwa hivyo ni njia tu ya kujuana na hivyo kuweza kushirikiana katika kubeba majukumu.  Kama vile ambavyo haifai kwa mtu wa kabila fulani ajione bora kuliko mtu wa kabila nyingine kwa ajili ya nasaba na ukoo wake, au watu wa nchi fulani wajiona bora kuliko watu wengine kijografia au kilugha, basi hata kwa mwanamke si haki ajione bora kuliko mwanamke mwingine au kinyume chake, ila kwa kumcha Mungu tu. 

“…Kwa hakika aliye mbora zaidi kwa Mwenyezi Mungu ni yule amchaye Mungu zaidi.”                               (49:13)

Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) pia amesema mara nyingi:  “Nawausia juu ya wanawake.”  Kwa hivyo basi, ni lazima kwa mwanamume mtilie manani sana mwanamke, kwani kuwapenda wanawake ni katika imani, na kadri mtu anavyozidi kuwa na imani kama asemavyo Mtume (saw) ndivyo anavyozidi kuwapenda wanawake.  Siyo penzi dhaifu la kimwili basli penzi tukufu la kidini!

Ewe mwanamke mu’umin!

1.         Ewe Mtetezi wa Mwenyezi Mungu, usiwe na kipenzi ila Mwenyezi Mungu, kwani yeye humpenda yule ajipendekezaye kwake.  Na ufunge milango yako ya duniani ili Mwenyezi Mungu akufungulie milango ya mbinguni! Wacha maneno ya kipuuzi, wacha matamanio na ujue ya kwamba hakuna uokovu mwingine ila wa Mwenyezi Mungu tu na Mugu hana khiyana yeye ndiye mbora, mwenye kunusuru, kata uhusiano wako wa upuuzi na ufanye uhusiano na jihadi na kina dada wana-dini.

2.         Heshimika na hijab yako na uifanye kuwa ndiyo silaha ya kuwapinga mataghuti wanao kutaka uwe kama mwanaserere (kijisanamu).  Ukiwa na hijab yako, geuka uwe mwangaza wa ucha­gamfu, kwani hijab siyo jela na kaburi la kuzikia uwezo wako, bali ni njia ya kuwa huru na ku­tenda.  Usitosheke na kuwa mtumwa mwenye thamani tu, bali uwe mwenye nafasi yenye tha­mani.

3.         Zielewe mbinu za mataghuti za kusaga shaksiya ya mwanamke, kwani mbinu zake ni chafu na zenye mizunguko mingi, mara nyingi hutumiwa mbinu zitakazofurahisha kuliko zitakazochukiza.  Taghuti ni bidhaa isiyochoka ya Iblis.  Taghuti hutumia vitimbi, mizunguko na udanganyifu, yeye huyachochoea matamanino ili azivunje heshima, na anasa ili kuivua heshima na hutumia ngoma na muziki ili kuiba imani za ucha Mungu.  Na ili uihifadhi heshima yako, basi ni lazima upambane na njia potofu ambayo ni nafsi inayoamrisha maovu na utahadhari na mata­manio yako.  Kisha jiulize: ni mwanamke gani anayeogopewa na taghuti?  Je! Ni yule ambaye  asubuhi akitafuta virembesho, marinda mazuri na hutoka akiwaonyesha watu wenye “Kiu” ma­pambo yake? Au ni yuke anayekwenda kwenye duka la vitabu akatafuta magazeti yenye fedheha na visa vya uongo vya mapenzi? Au je ni yule anapokuwa kwenye sherehe ataka awe mithili ya tausi akiringia nakshi za nguo zake na alivyo­tengeza nywele na mipaka ya muhimu kwake ni Jiografia ya mwili wake tu (alivyoumbika)? Au mwanamke anayeogopewa na Taghuti ni yule mpiganaji jihadi anayetafuta medani ya mapa­mbano, kama kipepeo atafutaye ngome ili awe kama askari mwenye tahadhari.

4.         Usiabudu virembesho na mapambo, kwani wewe ni mkuu kuliko chupa ya manukato au mti wa kupakia wanja, au kitambaa cha rinda, na fahamu ya kuwa uzuri wa roho ndio wanaowaunganisha watu na si uzuri wa mwili.  Jipambe na tafakuri na hisia zako zitie huruma kwa familia maskini, kwani moyo ni kama mmea, mtu asipouangalia kwa huruma na upole utakufa.

5.         Tahadhari sana na kushindwa, kwa sababu silaha kubwa ya mkoloni ni kushindwa kwa watu, yaani ndiko kushindwa kwa mwanamke; na ikiwa mwanamke ameshindwa, ni kizazi gani basi kitakacholelewa ila kitakuwa ni kizazi cha walioshindwa tu?

6.         Kuwa ni mwenye kutengeza mustakbali, na uingie kwenye mapambano ya kishujaa, kwani jihadi ni wajibu wako wa kimsingi  na zama hizi tunazoishi ni zama za hujuma za kikafiri dhidi ya uislamu, kwa hivyo kujilinda hakuhitaji ruhusa!

7.         Shiriki kwenye mipango na wanaume, kwani si haramu kuzungumza na wanaume na kukaa nao maadam muko katika njia ya Mwenyezi Mungu na uchunge heshima ya kisharia.

8.         Mbele ya mataghuti:  toa hoja ya nguvu, kataa, piga kelele.  Kumbuka kuwa mataghuti wengi wameanguka kutokana na upinzani wa kina Zainab na mikono yao ya chuma.

9.         Toka kwenye upenu wa khofu uliotiwa na vibaraka wa wakoloni, au kulala na kuzunguka jikoni tu kama wanavyokutaka uwe.

 

 

Ewe mwanamke mu’min!

Wakati tunaposoma Qur’an tukufu kuhusu mwanamke tunapata ukweli ufuatao:

·            Mwanamke na mwanamume kwa pamoja wana jukumu la kuchunga nafsi na watu.  Mwenyezi Mungu amesema:

“Waambie waislamu wanaume wainamishe macho yao na wazilinde tupu zao, hili ni takaso kwao, bila shaka Mwenyezi Mungu anazo habari za (yote) wayafanyayo.  Na waambie waislamu wanawake wainamishe macho yao na wazilinde tupu zao.”

                 (24:  30-31)

·            Kwa hakika mwanamke na mwanamume ni vipenzi wao kwa wao, mwanamume yampasa amthamini mwanamke na kumtakia mema, na mwanamke pia afanye hivyo hivyo.

“Na waumini wanaume na waumini wanawake ni marafiki (vipenzi) wao kwa wao.  Huamrisha mema na hukataza mabaya, na husimamisha Swala na kutoa Zaka na humtii Mwenyezi Mungu na Mtume wake; hao ndio Mwenyezi Mungu ataware­hemu.  Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye nguvu mwenye hekima.”                                               (9:71)

·            Mwanamke na mwanamume wana haki ya ku­pata sawa kulingana na wajibu wao watakao­utekeleza, na Mwenyezi Mungu anahifadhi haki ya mwanamke kama anavyohifadhi ya mwanamume, kama alivyosema katika Qur’an:

“Na watakaofanya vitendo vizuri wakiwa ni wanaume au wanawake hali wao ni wenye kuamini, basi hao wataingia peponi wala hawatadhulumiwa hata kokwa (konde) ya tende.”                          (4:124)

Amesema tena Mwenyezi Mungu: 

“Mola wao akawakubalia (kwa kusema): “Hakika mimi sitapoteza amali ya mfanya juhudi miongoni mwenu awe mwanamume au mwanamke”      (3:195)

“Wafanya wema wanaume au wanawake hali ya kuwa ni waislamu, mtawahuisha maisha mema, na tutawapa ujira wao (akhera) mkubwa kabisa kwa sababu ya yale mema alilyokuwa waliyatenda.”

  (16:97)

“Siku utakapowaona waislamu wanaume na wais­lamu wanawake, nuru zao zitakwenda mbele yao na kuliani kwao (wanaambiwa): “Furaha yenu leo (mnapewa) mabustani yapitayo mito mbele yake ku­kaa humo daima, huku ndiko kufaulu kukubwa”                   

(57:12)

·            Hapana tofauti kati ya mwanamume na mwanamke katika uharamu wa kuingilia haki zao.  Mwenyezi Mungu amesema:

“Na wale wanaowaudhi waislamu wanaume na waisalmu wanawake pasipo kosa lolote, bila shaka wamebeba adhabu ya Jahannam na watapata adhabu ya kuungua.”                                                    (85:10)

“Hakika wale waliowaadhibu (kuwaudhi) waislamu wanaume na waislamu wanawake, kisha wasitubie, basi watapata adhabu ya Jahannam na watapata adhabu ya kuugua.”                                          (85:10)

Na kuna Aya nyingi ambazo kwanza Mwenyezi Mungu anazungumza na Mtume wake juu ya mwanamke mwislamu, akimtaka Mtume aku­bali kuahidi kwao kubeba majukumu, amesema (s.w.t.): 

“Ewe Nabii! Watakapokuja wanawake walioamini wanaokuahidi ya kwamba hawatamshirikisha Mwenyezi Mungu na chochote, wala hawataiba wala hawatazini, wala hawataua watoto wao, wala hawa­taleta uzushi wanaozusha tu wenyewe baina ya mi­kono yao na miguu yao wala hawatakuasi katika jambo jema, basi peana ahadi nao na uwatakie maghfira kwa Mwenyezi Mungu.  Hakika Mwenyezi Mungu ni mwingi wa maghfira, mwingi wa rehma.”

                (60:12)

10.       Ingia kwenye sehemu yako aliyoitaka kwako Mwenyezi Mungu ya ukhalifa wa dunia na ku­jenga maisha na usingoje wanaume wakwambie la kufanya katika kutetea na ujipatie nguvu za wanaume kwa uthabiti wao.  Na uizuwie dhulma ya wanaume kwa matakwa yao; na ujue ya kwamba mwanamke anaweza kufanya mambo mengi na kutoa mchango wake katika mambo mema.  Na mwanamke ni mtukufu pale anapojuwa kuwa yeye ni mtukufu.

11.       Pambana na ada na desturi potofu za kijamii ambazo Mwenyezi Mungu hakuteremsha uhalali wake hasa zifanywazo katika nyanja za kijamii k.v. kwenye harusi ambapo mwanamke hukubali bei rahisi au kujiuza kwa vitu vya anasa tu.  Fikiri sana juu ya mali ya mumeo, ibadilishe hali yake, mwenendo wake, badili washirika wake wasiofaa, na katika mali yake badilisha mfumo wake.

12.       Kazi yako si kulea watoto tu, kama wasemavyo, bali kazi hiyo ni jukumu lako na mumeo, wajibu wako ni kama ule wa mwanamume katika nyanja zote.  Usikubali kuchukua nafasi ya pili kuwekwa pembeni; ondoa fikra za kufuata.  Jivishe vazi la uongozi usijiweke nyuma katika njia ya uongofu.

13.       Muige mwanamke mtukufu katika Historia, muige bibi Maryam bint Imran, mamake Masih (Isa (a.s.)) mtetezi, mpambanaji aliyawakemea Waisrael.   Au muige bibi Asya bint Muzahim, mke wa dikteta Fir’aun, mwanamke aliye muamini Musa (a.s.) na kufa shahid katika njia ya haki akikataa maisha ya anasa duni.  Au  uwe mfano wa bibi Khadija ambaye alimcha Mungu ali­mpa Mungu na cha kaizari pia alimpa Mungu!  Aliyejitolea kwa hali na mali kwa ajili ya waka­ndamizwaji.  Au pia uwe mithili ya bibi Fatima ali­yehama (Hijra) akapambana kwa jihad, akake­mea, akatoa hoja za nguvu na kuwanyima usi­ngizi matapeli.  Au pia jifanye kama bibi Zainab, sauti ya kimapinduzi iliyokata kusalimu amri kwenye huzuni, kukata tamaa na kutishwa.

14.       Usikubali kuvunjwa moyo na nduguzo, jamaa zako au marafiki juu ya kufuata njia ya jihadi na kupambana na taghuti, kwani kumridhisha Mwenyezi Mungu ndilo jambo la kwanza kabla ya viumbe, na watu wako hawana mamlaka ya kupigana na hukmu ya Allah.

15.       Jiweke kwenye kushiriki na wanaume na wanawake, na uwe na nafasi muhimu kwani lau kama Mwenyezi Mungu hakutaka mwanamke awe na nafasi muhimu asingemuumba mwanamume kwa njia ya mwanamke.

16.       Uwe mume, pale panapokosekana mwana­mume, kwani uume si mwili bali ni wa mwamko na msimamo.  Wanawake wangapi wana nguvu kushinda wanaume elfu, na kuna wanaume wangapi walio madhaifu kuliko wanawake.

17.       Kuwa mwana mapinduzi.  Kuwa mpiganaji.  Kuwa kila kitu lakini usiwe pambo la jikoni au godoro la kitandani au sahani iliyoangikwa ukutani, au sauti katika nyimbo, au picha ya kupamba ukurasa wa jarida.

18.       Jisome sana, fikiri sana, kwani  “Kufikiri saa moja ni bora kuliko ibada sabiini.”

19.       Ukuze mwamko wa leo wa kisiasa kwa kusoma vitabu vya siasa, na kufuatilia matukio ya kila siku, kwani yule anayezijua zama zake na hali zilivyo, hawezi kuvamiwa na majanga na kushtuliwa na matukio.

20.       Jizoeze mbinu za mapambano, kwani mwanamke mwislamu mwenye nguvu ni bora kuliko mwanamke mwislamu dhaifu, na hivyo hivyo mwanamume mwislamu mwenye nguvu ni bora kuliko asiye na nguvu.



[1] Soma mlango wa Nikah (ndoa) katika vitabu vyote vya Fiqh

[2] Man the Unknown.  Page.98

[3] Presence le Corps et I’Ane R.Beit

[4] Jar ida la  “Assuruuq”  Toleo No.4 mwaka wa 1

[5] Jar ida la  “Assuruuq”  Toleo No.1 mwaka wa 1

[6] Sehemu ya hotuba iliyotolewa na mwanachama mashuhuri wa Free Mason Bw. Beckrator, mnamo 1921.

[7] Yamenukuliwa kutoka kwenye Protocal 1 za Wazayun (Wayahudi).

[8] Walahidi:  Watu wasioamini Mungu.

[9] Dr. Melene Michele – Wolfromm. Cetle chose - La.

[10] Gazeti la Herald Tribure. Toleo la Ulaya, 10 Mach 1996.

[11] Gazeti la Al-Ihram la Misri 26 April 1966 lilinuko kutoka gazeti la Pravda la Sovieti la tarehe 25 April 1966.

[12] Jean Paul Sartre mwandishi na mwanafalsafa wa kifaransa aliyezaliwa mwaka 1905 (A.D.)