Maulidi, si Bida, si Haramu
Sh. Abdilahi Nassir


    YALIYOMO

 

 

 

 

 

The .HTML version of this book is taken from
www.al-islam.org and ebooked by www.ShiaLibrary.com and www.islamkutuphanesi.com . May Allah be pleased with all.

 

TOLEO MAALUMU

 

Lifuatalo ni toleo maalumu

 la kitabu kiitwacho

"Kumtukuza Mtume Muhammad (s.a.w.w.)"

chenye mkusanyiko wa mada za kuadhimisha kuzaliwa kwa Mtume Muhammad (s.a.w.w.)

 

Yaliyomo ni:

-      Vidokezo juu ya maisha ya muasisi wa Uwahabi

-      Kuadhimisha kuzaliwa Mawalii wa Mwenyezi Mungu na kufa kwao

-      Qur'ani na kuwatukuza Manabii na Mawalii

-      Uzindushi

-      Maneno na matendo ya mawahabi yanapingana

 

 

Agiza nakala yako kutoka kwa:

 

Bilal Muslim Mission of Kenya

P.O. Box 82508

Mombasa

Kenya

UTANGULIZI

 

Sifa njema zote ni za Mwenyezi Mungu, Bwana wa viumbe vyote. Na swala na salamu zimshukie Hashimu, Mtume Wake muadhamu (s.a.w.w.), na aali zake kiramu, na wote wenye kufuata nyayo zao.

 

Baina ya tarehe 4 Rabiiul Awwal, 1423 / 17 Mei, 2002 na 7 Jamaadath Thaani, 1423 / 16 Agosti, 2002 nilitoa mfululizo wa makala kumi na tatu juu ya maulidi ya Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Katika makala hayo, kwa kujibu hujja zinazotolewa na wale wanaopinga maulidi, nilijaribu kuonyesha kuwa maulidi si bid'a (uzushi) wala si haramu.

 

Ninamshukuru Mwenyezi Mungu (s.w.t.) kwa makala hayo kupokewa vizuri na wote walioyasoma. Na kwa kuitika maombi yao ya makala hayo kuchapishwa kitabu, nina furaha kubwa kuweza kuwatolea kitabu hicho kama walivyotaka.

 

Makala hayo na kitabu hiki kisingetoka kama si kwa msaada wa ndugu kadhaa wa kadhaa waliojitolea kunisaidia. Kwa upande wangu, sina la kuwalipa isipokuwa kuwaombea Mwenyezi Mungu awajazi kila lenye kheri na wao; amin.

 

ABDILAHI NASSIR

 

Mombasa, Kenya

17 Jamaadath Thaani, 1423

26 Agosti, 2002

 

 

1

 

SHEREHE ZA MAULIDI

 

Maulidi ni Kiswahili cha neno la Kiarabu, mawlid. Neno hili lina maana ya "mazazi" au "kuzaliwa kwa…" (birthday). Kwa kawaida, linapotumiwa na Waislamu, huwa na maana ya siku aliyozaliwa Mtume Muhammad (s.a.w.w.), au hafla ya kuisherehekea siku hiyo.

 

Waislamu wa ulimwengu mzima, ifikapo tarehe 12 ya Mfungo Sita (Rabiul Awwal), husoma maulidi na kuisherehekea siku hiyo kwa furaha kubwa. Sherehe hizo, kwa dasturi, haziishii tarehe hiyo tu, bali huendelea hata kwa miezi miwili mitatu baada ya hapo. Hili huwa ni kwa sababu ya Waislamu wa kila nyumba, kila mtaa, kila mji na kila nchi kutaka kushiriki katika sherehe hizo na kupata baraka zake. Vile vile huwapa Waislamu nafasi ya kutembeleana na kushirikiana katika sherehe hizo - jambo ambalo lisingewezekana lau watu wote wangeliamua kuzifanya sherehe hizo siku hiyo hiyo moja tu.

 

Kwa nini kusoma maulidi?

Waislamu husoma maulidi kwa sababu mbalimbali. Kati ya hizo ni:

(i)                 kuikumbuka na kuitukuza siku aliyozaliwa mbora wa viumbe vyote, aliyetutoa vizani na kututia kwenye nuru;

(ii)               ni njia moja ya kutoa shukrani zetu kwa neema hiyo;

(iii)             katika sherehe hizo, hupatikana fursa ya kukumbushana maisha ya bwana mkubwa huyo na mafunzo yake;

(iv)             hupatikana fursa ya Waislamu wa madhihabi na mataifa mbalimbali kushirikiana na kuziweka kando hitilafu zao; na

(v)               mikusanyiko hiyo huleta athari kwa wasio Waislamu ya kuupenda Uislamu, na hata kusilimu.

 

Wanaopinga na sababu zao

Lakini, hata hivyo, kuna baadhi ya Waislamu -- japokuwa wao si wengi kama wanaoyasoma -- ambao hupinga kusomwa maulidi; na hutoa sababu zao. Kati ya sababu hizo ni:

(i)                 maulidi hayakuwako zama za Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Basi kwa nini yazuliwe sasa?

(ii)               hayakusomwa na maswahaba wala waandamizi wao. Kama kweli yangelikuwa ni sawa kuyasoma, bila shaka mabwana wakubwa hao wangelikuwa ni wa mbele kufanya hivyo;

(iii)             kuweka ada ya kusoma maulidi ni kuigiza Wakristo walioweka siku ya Krismasi; na Mwislamu haruhusiwi kufanya hivyo;

(iv)             kwenye sherehe za maulidi hufanywa baadhi ya mambo ambayo ni ya munkar (yanayochukiza, bali ni haramu kamwe, katika sharia ya Kiislamu); na

(v)               hakuna ushahidi wowote, wa Qur'ani wala Hadithi za Mtume Muhammad (s.a.w.w.), unaothubutisha usawa wa kuyasoma maulidi, sikwambii kuyatilia nguvu.

 

Kwa nguvu ya hujja hizo, mara nyingi viongozi wa wanaopinga maulidi huwaonyesha wafuasi wao kuwa wale wanaosoma maulidi ni watu waliopotea kwa "kuzua" mambo yasiyo na msingi katika dini yetu hii. Jambo hili limeleta mchafuko -- unaofufuka aghalabu kila ifikiapo miezi ya kusoma maulidi -- ambao unahatarisha umoja na masikizano, sio baina ya Waislamu wa madhihabi mbalimbali peke yao, bali hata wale wa madhihabi mamoja!

 

Mchafuko huu huzidi kukua kwa sababu ya lugha kali inayotumiwa na pande zote mbili  -- za wanaounga na wanaopinga maulidi -- katika kutetea misimamo yao; na hilo haliwezi kusaidia katika kutatua usawa uko wapi. Liwezalo kutatua hitilafu hii ni kuijadili ki-ilimu na kwa lugha nzuri ya kuhishimiana. Na hilo ndilo nililokusudia kulifanya, kuanzia makala yanayofuatia haya, Inshallah.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

2

 

HUJJA ZA WAPINZANI NA MAJIBU YETU

 

Hujja yao ya kwanza ni kwamba: maulidi hayakuwako zama za Mtume Muhammad (s.a.w.w.) Kwa hivyo, kuyaleta baada ya yeye kufariki dunia, ni bid'a (uzushi). Na kila bid'a, kwa maneno yake mwenyewe Bwana Mtume (s.a.w.w.), ni upotevu. Kwa hivyo, kila anayesoma maulidi amepotea!

 

MAJIBU YETU: Ni kweli kwamba maulidi, hivi tunavyoyasoma, hayakuwako zama za Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Lakini si kweli kwamba, kulifanya kila ambalo halikuwako zama hizo, ni upotevu. Kama ni hivyo, basi bila shaka Waislamu wote leo -- wakiwamo wanaopinga maulidi -- wangelikuwa wamepotea kwa kuwa (katika zama zao mbalimbali) wamefanya, na wanaendelea kufanya, mambo ambayo hayakuwako zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.)!

 

Kwa mfano, katika zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.), misikiti haikuwa ikitandikwa chochote (watu wakisujudu juu ya mchanga); lakini leo inatandikwa majamvi, busati na mazulia! Kiwanja kitakatifu cha Al-Kaaba kilikuwa ni mchanga mtupu na mawe; lakini leo kimetandikwa marumaru! Watu walikuwa wakenda kuhiji kwa kupanda ngamia au majahazi; lakini leo wanakwenda kwa ndege, meli za kisasa na mabasi ya anasa (luxury)! Watu, walipokuwa wengi msikitini, walikikhutubu kwa kupaza sauti zao; lakini leo wanatumia vipaza sauti (loud speakers)! Misahafu ilikiandikwa kwa mkono, juu ya ngozi na mifupa, na kutolewa nakala chache; lakini leo inachapwa kwa mashini, juu ya karatasi za fakhari, na kutolewa nakala mamilioni kwa mamilioni!

 

Lakini hakuna anayesema -- hata hao wanaopinga maulidi hawasemi -- kwamba Waislamu waliobuni mambo hayo wametuletea bid'a au wamepotea. Kwa nini? Kwa sababu kwao wao, na kwa wanaosoma maulidi, uzushi wa aina hiyo si bid'a; sio alioukusudia Bwana Mtume (s.a.w.w.). Alioukusudia yeye ni ule wa kuzua jambo katika dini hii ambalo halitokani nayo (maa laysa minhu). Hilo ndilo lililo wazi kutokana na Hadithi mashuhuri ya Bwana Mtume (s.a.w.w.) inayosema: "Yoyote atakayezua, katika dini yetu hii, jambo ambalo halitokani nayo, litarudishwa (litakataliwa)."

 

Ukiitaamali vizuri Hadithi hiyo, itakudhihirikia kwamba Bwana Mtume (s.a.w.w.) hakutuzuia kuzua (kubuni), katika dini hii, kila ambalo halikuwako zama zake. Kama angelitaka kutuzuia hivyo, Hadithi hiyo isingelisema hivyo, bali ingelisema hivi: "Yoyoye atakayezua jambo katika dini yetu hii, litakataliwa." Na lau ingelisema hivyo, basi yote yale tuliyoyataja hapo juu yasingeliruhusiwa; yangelikuwa bid'a.

 

Lakini Hadithi haikusema hivyo. Ilivyosema ni:

"Yoyote atakayezua … ambalo halitokani nayo, litakataliwa." Kwa kuongeza kifungu cha maneno tulichokichapa kwa italiki (yaani "ambalo halitokani nayo"), ni wazi kwamba Mtume Muhammad (s.a.w.w.) hakukusudia kuwazuia Waislamu kufanya kila ambalo halikuwako zama zake. Alilolikusudia ni kutuachia wazi mlango wa kubuni mambo katika dini hii bora tu yawe yanatokana nayo.

 

Sasa suali hapa ni: jee, maulidi si katika mambo yanayotokana na "dini hii", hata kama hayakuwako zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.)?

 

Majibu yetu ni: Maulidi, na yaliyomo maulidini, si mageni na "dini hii", bali yanatokana nayo, kama tutakavyobainisha kwa urefu zaidi katika majibu yetu ya hujja Na. (v) ya wapinzani wake inshallah.

 

Kwa hivyo, kuwa tu jambo halikuwako zama za Mtume Muhammad (s.a.w.w.) si hujja ya kuwazuia Waislamu kulifanya. Wanalozuiliwa Waislamu kulifanya ni kuzua jambo na kulifanya ni dini hali ya kuwa halina asili na dini. Na maulidi si hivyo!

 

Katika hujja yao ya pili wanasema: Maulidi hayakusomwa na maswahaba wala waandamizi wao (taabi'in). Kama kweli yangelikuwa ni sawa kuyasoma, bila shaka mabwana wakubwa hao wangelikuwa ni wa mbele kufanya hivyo.

 

MAJIBU YETU: Hakuna Mwislamu yoyote anayekataa kuwa maswahaba ni watu watukufu. Wala hakuna anayekataa kuwa wao ndio kiungo chetu sisi na Bwana Mtume (s.a.w.w.). Lakini, pamoja na utukufu wote huo, wao walikuwa ni binadamu; hawakuwa ni ma'asumin. Walikiweza kufanya jambo, wakaswibu (wakapata); kama ambavyo walikiweza kufanya jambo, wakakosea. Na mifano ya yote mawili hayo ni mingi katika historia yao.

 

Kwa hivyo, kuwa tu jambo fulani halikufanywa na maswahaba, haliwi ni hujja sahihi ya kuwazuilia Waislamu kulifanya jambo hilo. Hujja ya pekee iliyo sahihi ni iwapo lile ambalo hawakulifanya wao, waliacha kulifanya kwa sababu ndivyo alivyoamrisha Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.), au waliacha kulifanya kwa sababu linapingana na maamrisho ya Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.). Ikiwa walifanya hivyo ndipo jambo hilo litakapokuwa ni hujja; lakini si kwa sababu ya kuwa halikufanywa na maswahaba, bali ni kwa sababu tu ya kuwa ndivyo alivyoamrisha Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.), au ni kwa sababu tu ya kuwa linapingana na mafunzo ya Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.) -- na hivyo ndivyo Kiislamu.

 

Kwa hivyo si sawa kuyapinga maulidi kwa sababu tu hayakusomwa na maswahaba na waandamizi wao. La sawa ni kuyapinga kwa sababu tu yamekatazwa na Mwenyezi Mungu au Mtume Wake (s.a.w.w.), au yanapingana na maamrisho yao. Na hilo, mpaka hivi sasa, wapinzani wa maulidi hawajaweza kulithubutisha.

 

Tunasema hivyo kwa sababu, mmoja kati ya misingi muhimu ya sharia ya Kiislamu, inayokubaliwa na wanazuoni wa wanaosoma maulidi na wale wa wanaopinga maulidi, ni kwamba -- tunapokuja kwenye mambo kama ya maulidi, ujenzi wa msikiti, mavazi, na kadhaalika -- kila kitu ni halali mpaka kithubutishwe kuwa ni haramu. Kwa hivyo, kwa msingi huu, uharamu wa maulidi haitaki uthubutishwe na wanaoyasoma, bali inataka uthubutishwe na wanaoyapinga. Wala wasilithubutishe hilo kwa vichwa vyao (Sura 16:116), bali kwa kutoa ushahidi wa maneno ya Mwenyezi Mungu au Mtume Wake s.a.w.w. (Sura 4:59). Na hilo pia, mpaka dakika hii, wapinzani wa maulidi hawajaweza kulifanya.

 

Mwanzo mwanzo wa kuzuka madhihabi haya ya kupinga maulidi, wafuasi wake waliyapinga mambo mengi yaliyozuka katika zama zao. Kati ya mambo hayo ni kuvuta sigara, kupiga simu ya mdomo (telephone), kujiwekea kashida mbele ya mtu anaposwali, kumwamkia mtu kwa: "Umeamkaje?", kupana mikono baada ya swala, kutandika busati misikitini, na hata kuvaa nguo yenye thamani inayozidi dirhamu 100 (mia)!

 

Yote hayo waliyapinga kwa hujja ya kuwa hayakuwako zama za Mtume (s.a.w.w.), na kwamba hayakufanywa na maswahaba na waandamizi wao! Lakini, baada ya kutambua walikosea wapi, walirudi nyuma, wakayakubali yote hayo. Kwa maneno mengine, yakawa sio bid'a tena!

 

Leo, kwa hujja hizo hizo, waandamizi wao wameanza kusema vibula vivunjwe! Kesho watasema na minara nayo ivunjwe! Kesho kutwa watasema mimbari za mbao au za mawe, nazo pia ziondolewe, zirudishwe zile za vigogo vya mtende; hata vya mnazi havitafaa! Baada ya hapo ni nini kitakachowazuia wasitwambie tuondoe banka (panka) misikitini, turudi kujipepea kwa nguo zetu kama ilivyokuwa zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.)? Au twende hijja kwa ngamia au farasi badali ya ndege? Au ni lipi litakalowazuia kutuamrisha kuisoma Qur'ani katika ngozi na mbao, kama ilivyokuwa zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.) na maswahaba, badali ya hii miswahafu mizuri mizuri tuliyonayo?

 

Ni matumaini yetu kwamba, kama ambavyo watangulizi wao walirudi nyuma na kuyakubali yale waliyoyafanya ni bid'a mwanzo, wao nao watafuata nyayo zao, wayaone maulidi, na mengine kama maulidi, kuwa sio bid'a iliyokatazwa na Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Alhamdulillaah, baadhi yao wameanza kuona hivyo na kufanya sherehe za mazazi ya Bwana Mtume (s.a.w.w.). Lakini badali ya kuyaita maulidi, huyaita seera!

 

Hujja yao ya tatu ni kuwa: kuweka ada ya kusoma maulidi ni kuigiza Wakristo walioweka siku ya Krismasi; na Mwislamu haruhusiwi kufanya hivyo.

 

MAJIBU YETU: Mwislamu hazuiliwi kufanya jambo kwa sababu tu linafanywa na Mkristo au kafiri yoyote mwengine. Analozuiwa ni kufanya jambo kama linalofanywa na Mkristo, au kafiri yoyote mwengine, linapokuwa linakwenda kinyume na mafunzo ya Kiislamu; na hilo sio linapofanywa na Mkristo au kafiri yoyote tu, bali hata linapofanywa na Mwislamu mwenziwe; haruhusiwi kulifanya.

 

Tunaposoma historia, kwa mfano, tunaona jinsi Bwana Mtume (s.a.w.w.) -- katika Vita vya Handaki -- alivyokubali shauri la Salman Farisi la kuchimba handaki kama walivyokifanya Wafursi kwao. Na Wafursi, wakati huo, hawakuwa ni Waislamu, bali walikuwa ni makafiri waliokiabudu moto! Jee, kwa kuwaigiza makafiri hao katika uchimbaji wa handaki, Bwana Mtume (s.a.w.w.) alikosea?

 

Hali kadhaalika, tukija kwenye hijja mathalan, tunaona jinsi mahujaji wanavyokwenda baina ya Swafaa na Marwa, na jinsi wanavyochinja wanyama mwisho wa hijja yao. Lakini vitendo kama hivyo, kabla ya Uislamu, vilikuwa vikifanywa na makafiri! Basi kama kuigiza Wakristo hakuruhusiwi, kwa nini Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.) wakatuamrisha kufanya mambo ambayo dhahiri yake ni sawa na kuwaigiza makafiri?

 

Ukivizingatia vizuri vitendo hivyo utaona kwamba, japokuwa kwa dhahiri vinafanana na vile vya makafiri, kwa kweli huwezi kusema kuwa ni sawa na kuwaigiza makafiri. Kwa nini? Kwa sababu waliyokuwa wakiyafanya makafiri mwahali humo, walikuwa wakiyafanyia masanamu yao, waliyoyaweka humo. Kwa hivyo yao ilikuwa ni shirk (ushirikina). Lakini tunayoyafanya sisi Waislamu, baada ya kuondolewa mbali masanamu hayo, huwa tunamfanyia Mwenyezi Mungu Mmoja tu, asiye na mwenziwe (mshirika). Kwa hivyo yetu ni tawhid (kumpwekesha Mwenyezi Mungu).

 

Hali kadhaalika tunapokuja kwenye Krismasi. Japokuwa Krismasi, kama maulidi, hufanywa kwa kusherehekea mazazi ya Mitume ya Mwenyezi Mungu (Nabii Muhammad s.a.w.w. na Nabii Isa a.s.), lakini sherehe mbili hizo -- kama ambavyo kila mtu anajua -- si sawa. Sherehe zinazofanywa Krismasi ni tafauti kabisa na zinazofanywa maulidini, kama ambavyo Wakristo wanavyomchukulia Nabii Isa a.s. (Yesu Kristo) ni tafauti kabisa na vile Waislamu wanavyomchukulia Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Kwa mfano, Waislamu hawamchukulii Mtume Muhammad (s.a.w.w.) kuwa ni Mungu, wala ni Mtoto wa Mungu, wala ni Roho Mtakatifu.

 

Kwa hivyo kuwa tu jambo fulani lilitangulia kufanywa na makafiri -- wawe ni Wakristo ama ni wengineo -- haiwi ni hujja ya kuwazuilia Waislamu kulifanya jambo hilo maadamu watayatoa yote ya ukafiri yaliyokuwamo humo. Na hivyo ndivyo maulidi yalivyo. Zaidi ya kuwa zote mbili -- Krismasi na maulidi -- ni sherehe za mazazi ya Mitume ya Mwenyezi Mungu, hakuna jengine linalofanana katika sherehe hizo.

 

Kama tutashikilia kuwa ni haramu Waislamu kuwaigiza Wakristo, au makafiri wowote kwa jumla, katika jambo lolote -- hata kama halipingani na dini yetu -- basi sio wanaosoma maulidi tu, bali hata wanaoyapinga pia watakuwa makosani. Kwani ni nani kati yao aliyeacha gari au ndege, akaendelea kupanda punda, farasi au ngamia? Ni nani, anayejimudu, aliyeacha kutumia umeme (spaki), akaendelea na kuni au mafuta ya taa? Ni nani anayeradhiwa kujipepea kwa kipepeo au nguo yake, akaacha -- ikiwa anayo nafasi -- kutumia banka au AC (Air Conditioner)? Ni nani anayepanda kwa miguu mpaka ghorofa ya 15, au ya 10, akaacha lifti? Kwa nini hawayaachi yote hayo ili wasiwe wanawaigiza Wakristo au makafiri wengine, maana yote hayo yameanzishwa na wao.

 

Kwa hivyo si sawa kuwazuilia Waislamu kusoma maulidi kwa sababu tu ya kuwa, kufanya hivyo, ni kuwaigiza Wakristo katika  sherehe zao za Krismasi.

 

 

Katika hujja yao ya nne wanasema: Kwenye sherehe za maulidi hufanywa baadhi ya mambo ambayo ni ya munkar (yanayochukiza, bali ni haramu kamwe, katika sharia ya Kiislamu).

 

MAJIBU YETU: Hiyo si hujja madhubuti. Kwa nini maulidi yote yatupwe kwa sababu tu ya kufanywa baadhi ya mambo ambayo ni ya munkar katika sherehe zake? Kwa nini hayaondolewi hayo ya munkar, kama yako, yakabakishwa yasiyo ya munkar? Kwani tunda likiwa limeoza kidogo hutupwa lote, au hukatwa pale palipooza likaliwa pale pazuri palipobaki?

 

Katika hili tuna funzo zuri kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Yeye aliondoa tawafu ya Al-Kaaba, na Swafaa na Marwa, kwa sababu mwahali humo mulikuwa na munkar (masanamu) au aliamrisha yaondolewe hayo masanamu na watu waendelee kutufu? Tutaona kuwa Mwenyezi Mungu hakutuzuia kufanya jambo zuri lililokuwako (kutufu na kusa'yi) kwa sababu tu katika ibada hizo palikuwa na munkar (masanamu). Alilolifanya ni kuondoa munkar uliokuwako, akatuacha tuendelee na mazuri yaliyobaki (tawafu).

 

Kwa hivyo, kama katika maulidi kuna munkar wowote, la sawa ni uondolewe munkar huo, na maulidi yaachwe yaendelee. Si kumtupa jongoo na ung'ongo (ujiti) wake.

 

Kidokezo

Baada ya kutoa makaratasi yetu kwa wiki tatu, makundi mawili ya wanaopinga maulidi yamejitokeza. La kwanza limejita "Ahlu-Tawheed"; na la pili linajita "Wakereketwa wa Sunna Malindi". Na yote mawili hayakutoa anwani zao!

 

Ahlu-Tawheed wametoa makaratasi yenye jina la "Uzushi na Shirk Ndani ya Barzanji na Vitabu Vyengine vya Maulid". Katika makaratasi hayo, wamenukuu baadhi ya madondoo ambayo -- kwa maoni yao -- ni shirki. Lakini hawakutueleza vipi kuwako madondoo hayo katika vitabu hivyo, hata kama yatakuwa ni shirki kweli, yanafanya maulidi yoyote mengine (yasiyo na hayo wanayoyaona wao kuwa ni shirki) hayafai kusomwa.

 

Wakereketwa wa Sunna Malindi, kwa upande wao, wametoa makaratasi yenye jina la "Chapa ya Kwanza (1): Majibu ya Abdillah Nassir". Katika makaratasi hayo, ambayo wameahidi kuendelea nayo, hawajazungumzia maulidi. Walilolifanya ni kunizungumza mimi binafsi -- kwa ya kweli na ya uwongo! Lakini na wao pia, kama wenzi wao, hawajatueleza vipi vyovyote vile vitakavyokuwa mimi binafsi -- iwe ni kwa wema ama kwa uovu -- ni hujja tosha ya kuyafanya maulidi yawe hayafai kusomwa! Pengine watalieleza hilo katika makala yao yatakayofuatia.

 

Hata hivyo si nia yangu, kwa sasa, kuyajibu makaratasi hayo kwa sababu kutatutoa nje ya mfululizo wetu huu. Nia yangu inshallah ni kuendelea kuzijibu hujja zao zote nilizozidondoa katika sura ya kwanza humu. Baada ya hapo ndipo nitakapojibu hayo yaliyomo katika makaratasi yao hayo.

 

Kwa hivi sasa, napenda kuwahakikishia wanaosoma maulidi kwamba yote waliyoyataja katika makaratasi yao mawili hayo tutayajibu kiilimu na kistaarabu, kama ilivyo dasturi yetu, na kama tulivyofanya mpaka sasa, pamoja na kuonyesha  kwamba hayana mashiko.

 

Kwa hivyo, tunawaomba wale walionayo makaratasi hayo wayaweke, wangojee majibu yetu inshallah.

 

Katika hujja yao ya tano wanasema: Hakuna ushahidi wowote, wa Qur'ani wala Hadithi za Mtume Muhammad (s.a.w.w.), unaothubutisha usawa wa kuyasoma maulidi, sikwambii kuyatilia nguvu.

 

MAJIBU YETU: Katika majibu yetu ya hujja yao ya pili, tulieleza kwamba -- kwa mujibu wa msingi mmoja kati ya misingi muhimu ya sharia ya Kiislamu -- anayetakikana kuthubutisha kuwa maulidi hayafai kusomwa si anayesema yasomwe; ni anayesema yasisomwe. Kwa hivyo ushahidi wa Qur'ani na Hadithi unaotakikana si wa kutolewa na sisi tunaosema ni sawa kusoma maulidi, bali ni wa kutolewa na wao wanaoyakataza. Jee, wanao ushahidi huo? Kama wanao, twaukaribisha.

 

Hata hivyo, kama ushahidi wanaoutaka wapinga maulidi, wa Qur'ani na Hadithi, ni unaosema kwa kutasua (nassun qat'iyy / categorically), "Enyi mlioamini! Someni maulidi"; basi ushahidi huo hakuna. Lakini tunauliza, kwa sharia ya Kiislamu, ni lazima jambo litasuliwe katika Qur'ani au Hadithi ya Bwana Mtume (s.a.w.w.) ndipo liruhusiwe kufanywa? Jee, hakuna mambo ambayo Waislamu -- wakiwamo wanaopinga maulidi -- huyafanya pamoja na kuwa hawana ushahidi wa Qur'ani wala Hadithi zilizoyataja mambo hayo?

 

Kwa mfano, ni nani kati ya wanaopinga maulidi anayeweza kututolea ushahidi wa kutasua -- wa Qur'ani au Hadithi ya Mtume Muhammad (s.a.w.w.) -- wa Waislamu kuruhusiwa kujenga vyuo (colleges) na vyuo vikuu? Au kutoa digrii? Au kujenga hospitali na zahanati? Au kujenga nyumba za mayatima (orphanages)? Au kuunda vyama vya ushirika? Au kuweka mashindano ya kusoma Qur'ani na kuyatolea zawadi, na mengine mengi kama hayo? Jibu ni: hakuna! Kama uko, tunaomba tutolewe. Jee, kwa kuwa hauko, ndio watakuwa Waislamu wote -- wakiwamo wanaosoma maulidi -- wanakosea kwa kuyafanya mambo hayo kwa sababu tu hakuna aya au Hadithi inayoyataja? Kama ni hivyo, basi kwa nini wao wanayafanya? Kama sio hivyo, basi kwa nini wanatukataza kuyasoma maulidi kwa sababu hiyo hiyo?

 

Katika Qur'ani na Hadithi kuna mambo ambayo uhalali wake umetasuliwa (specified). Mfano wa hayo ni kumpwekesha Mwenyezi Mungu, kuswali, kufunga (saumu), kutoa zaka, kuhiji, kuowa, kufanya biashara, kufanya uadilifu, na kadhaalika. Kuna na ambayo uharamu wake pia umetasuliwa; kama kumshirikisha Mwenyezi Mungu, kuzini, kula riba, kuiba, kudhulumu, kusema uwongo, kusengenya, na kadhaalika. Yote hayo ni mambo ambayo ushahidi wake -- wa kuyatasua khaswa -- unaweza kutolewa katika Qur'ani na / au Hadithi za Bwana Mtume (s.a.w.w.).

 

Kuna na ambayo hayakutasuliwa isipokuwa yametajwa kwa jumla (generally) tu. Hayo, kinyume na yale yaliyotasuliwa tuliyoyataja hapo juu, yana uwanja mkubwa wa jinsi ya kuyatekeleza maadamu hayatachanganywa na ya haramu. Hebu tuangalie mifano miwili mitatu:

 

1.      Mayatima: Tunaposoma Qur'ani na / au Hadithi, tunaona kwamba tunahimizwa kwa jumla tuwatizame, tusiwatupe; tuwahurumie, tusiwatese. Vipi? Hilo hatukutajiwa tafsili zake isipokuwa tumeachiwa sisi, bora tu tusitie la haramu. Kwa sababu hii ndio ukaona hakuna aliyezuia kujengwa nyumba za mayatima (orphanages) japokuwa hazikutajwa kwa jina katika Qur'ani wala Hadithi za Mtume Muhammad (s.a.w.w.)!

 

2.      Ilimu: Tunaposoma Qur'ani na / au Hadithi, tunaona jinsi tunavyohimizwa, bali kufaradhiwa, kusoma na kuitafuta ilimu popote ilipo. Hatukupawa tafsili ya namna ya kulitekeleza hilo. Kwa hivyo, maadamu hatulitii la haramu, tuko huru kusoma kwa ubao, kitabu, tepu, video, redio, runinga, mtandao, na kadhaalika; kama ambavyo tuko huru kusoma madrasa, nyumbani, msikitini, chuoni (college) au kwenye vyuo vikuu; na kama ambavyo tuko huru kukaa majamvini, vitini au madeskini. Hakuna hata mmoja wa mashekhe wa wanaopinga maulidi anayewazuia watu kuyafanya hayo, na tuliyoyataja hapo juu yanayohusu mayatima, kwa sababu tu hayakutajwa kwa jina katika Qur'ani wala Hadithi za Mtume Muhammad (s.a.w.w.)!

 

Basi kwa nini kuyapinga maulidi?

 

Inshallah, katika sura inayofuatia, tutazidondoa aya za Qur'ani na Hadithi za Bwana Mtume (s.a.w.w.) ambazo, japokuwa hazikutaja maulidi kwa jina, zinaunga kwa jumla yale yanayofanywa na yanayofanyika maulidini.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

3

 

MAULIDI  KATIKA  QUR'ANI  NA  HADITHI

 

Japokuwa -- kama tulivyoeleza katika sura iliyopita -- maulidi hayakutajwa kwa jina katika Qur'ani wala Hadithi, lakini yamekusanya mengi yaliyoamrishwa au yaliyopendekezwa na Qur'ani na / au Hadithi. Hapa chini tutayataja baadhi yake tu:

 

1.      Kusoma na kusikiliza Qur'ani:  Tunaposoma Qur'ani (k.m. Sura 73:4 na 20), tunaona jinsi Mwenyezi Mungu anavyotuamrisha tuisome. Na tunapokuja kwenye Hadithi zake, tunaelezwa kwamba Bwana Mtume (s.a.w.w.) alikuwa akipenda sana mtu amsomee yeye Qur'ani, na yeye akisikiliza.

 

Jee, pale tunapoyafungua maulidi yetu kwa mmoja wetu kuisoma Qur'ani, na wengine tukawa tunamsikiliza, huwa -- kama hatukufanya la sunna -- tumefanya lipi la bid'a?

 

2.      Kumswalia Mtume (s.a.w.w.): Katika Qur'ani Tukufu (Sura 33:56), Mwenyezi Mungu anatuamrisha tumswalie Mtume Wake (s.a.w.w.) baada ya kutwambia kuwa Yeye na Malaika Wake hufanya hivyo pia. Isitoshe! Na kila Ijumaa, khatibu hutukumbusha juu ya mimbari, kwa kututajia Hadithi ya Mtume (s.a.w.w.), kuwa yoyote atakayemswalia yeye mara moja, Mwenyezi Mungu atamswalia (atamrehemu) mtu huyo mara kumi!

 

Jee, katika kikao kimoja tu cha maulidi, waliohudhuria humswalia Mtume (s.a.w.w.) mara ngapi? Zidisha mara hizo kwa kumi ujue Mwenyezi Mungu hukurehemu wewe mara ngapi katika kikao hicho. Jee, ni lipi hapo -- kama halitakuwa sunna -- lililo bid'a?

 

3.      Kumhishimu na kumtukuza Bwana Mtume (s.a.w.w.): Katika Qur'ani Tukufu (Sura 7:157), Mwenyezi Mungu anawasifu, na kuweta "wenye kufaulu", wale ambao humtukuza na kumhishimu Mtume Wake (s.a.w.w.), wakamsaidia na kuyafuata yale aliyoyaleta. Lakini tutawezaje kuyafanya hayo kama mtu mwenyewe hatumjui vilivyo?

 

Waswahili husema: "Jambo usilolijua ni usiku wa kiza"; na "asiyekujua hakuthamini". Kwa hivyo, bila ya kumjua Mtume (s.a.w.w.) vilivyo -- historia yake, sifa zake, cheo chake, utukufu wake, na kadhaalika -- vipi tutaweza kumthamini na kumtukuza? Ndipo wanazuoni, kwa kuwa si kila mtu aweza kusoma vitabu, wakabuni maulidi ili yawe ni chombo cha kumjulisha Bwana Mtume (s.a.w.w.) apate kuhishimiwa na kutukuzwa. Hivyo katika maulidi, watu hupata fursa ya kuelezwa yote ya Mtume (s.a.w.w.). Na kwa kuyajua hayo, watu humpenda; na kama ilivyo dasturi ya kila apendaye kumfuata yule anayempenda, watu humfuata.

 

Jee, kama maulidi yanasaidia watu kumjua Mtume (s.a.w.w.), kumkumbuka na kumpenda, ni lipi hapo la bid'a?

 

4.      Kumsifu Bwana Mtume (s.a.w.w.): Tunaposoma maisha yake, tunaambiwa kwamba, miongoni mwa maswahaba, walikuwako waliotunga mashairi ya kumsifu Bwana Mtume (s.a.w.w.) ambayo walikwenda nayo mbele zake na kumsomea. Bwana Mtume (s.a.w.w.) hakuwafukuza watu hao wala hakuwakataza, bali aliwasikiliza na kuyafurahia yote waliyomsomea. Kwa kitendo hicho kwa hivyo, Bwana Mtume (s.a.w.w.) alitufungulia mlango wa kumsifu. Tafauti ya pekee iliyoko baina ya maswahaba na sisi ni kwamba wao walimsifu machoni mwake, hali sisi tunamsifu akiwa hayuko na sisi kimwili. Sasa, kwa kitendo hiki, tunafanya jambo gani ambalo halikufanywa na maswahaba na kukubaliwa na mwenyewe Bwana Mtume (s.a.w.w.)?

 

Kama kufanya hivyo ni bid'a, basi sunna ni ipi?

 

5.      Kutoleana waadhi: Katika Qur'ani Tukufu (Sura 16:125) Mwenyezi Mungu anatuamrisha tulinganiane kwa hikima na mawaidha mema. Na vivyo hivyo ndivyo Bwana Mtume (s.a.w.w.) anavyotuhimiza katika Hadithi zake nyingi.

 

Jee, maulidini hatutoleani mawaidha na kulinganiana mema? Hayo nayo kama ni bid'a, sunna ni ipi?

 

6.      Kumpenda Mtume (s.a.w.w.): Hadithi zake (s.a.w.w.) zatuhimiza tumpende, bali zinatueleza waziwazi kwamba hatuwi ni waumini mpaka tumpende yeye kuliko nafsi zetu, kuliko mali yetu na ahli zetu, bali kuliko watu wote.

 

Jee sifa zote zile anazosifiwa Mtume (s.a.w.w.) maulidini, furaha zote na nderemo zinazoonyeshwa maulidini, haziwi ni ushahidi wa mapenzi yetu kwa Mtume Muhammad (s.a.w.w.)? Mambo kama hayo hufanyiwa asiyependwa?

 

Kama kuonyesha mapenzi yetu kwa Mtume wetu ni bid'a, sunna ni ipi?

 

7.      Kujumuika na kushikamana: Qur'ani Tukufu (Sura 3:103) inatuhimiza tushikamane na tusifarikiane. Na Mtume naye (s.a.w.w.) anatuhakikishia, katika Hadithi zake, kwamba popote ambapo tutajumuika kwa kheri -- na sidhani kuwa maulidi ni shari -- basi Malaika watatuzunguka, rehema za Mwenyezi Mungu zitufinike, na utulivu wa nyoyo utushukie.

 

Jee, tunapokusanyika maulidini, hatuyaoni hayo? Ule umoja na mshikamano unaopatikana maulidini, wa wafuasi wa madhihabi mbalimbali kusahau hitilafu zao na kuwa kitu kimoja, ni rehema ndogo?

 

8.      Kutembeleana na kukirimiana: Bwana Mtume (s.a.w.w.), katika Hadithi zake, ametunasihi tuwe tukifanyiana hayo; na hayo huyapata kwa ukubwa siku za maulidi. Waislamu wa mtaa mmoja, au mji mmoja, au hata nchi moja -- kwa kuhudhuria sherehe za maulidi ya wenzi wao -- hupata fursa ya kutembeleana na kukirimiana. Kwa njia hii hujuana hali, wakasaidiana na kupanana (peana) moyo. Hilo huleta mapenzi na mshikamano baina yao. Na iwapo pale pasomwapo maulidi Waislamu ni wachache, kutembelewa kwao na ndugu zao wanaotoka sehemu nyengine huwatia moyo, na pia huwafanya wahishimiwe na wale jirani zao wasio Waislamu.

 

Katika hayo, ni lipi la bid'a, kama hapana la sunna?

 

9.      Kutangaza Uislamu na kusilimisha wengine: Katika Qur'ani Tukufu (Sura 5:67) Mwenyezi Mungu anamwamrisha Mtume Wake (s.a.w.w.) awafikishie watu Ujumbe aliompa. Na katika khutba yake ya mwisho, Bwana Mtume (s.a.w.w.) alituamrisha sisi wafuasi wake tuufikishe Ujumbe huo kwa yule ambaye haujamfikia. Na hilo limepatikana -- na linaendelea kupatikana -- maulidini kwa ushahidi wa rikodi ya wengi waliosilimu baada ya kuhudhuria maulidini na kusikiliza kaswida na khutba zinazotolewa huko.

 

Jee, bid'a ni ipi hapo?

 

10.  Kumkumbuka Mtume Muhammad (s.a.w.w.): Qur'ani Tukufu (Sura 41:34) inatwambia kuwa jema na ovu si sawa. Ukitaka kuliondoa ovu, liondoe kwa jema ndipo ovu litakapofutika. Na Mtume (s.a.w.w.) naye ametwambia vivyo hivyo. Hali kadhaalika wazee nao wanatwambia kwamba tukitaka kumpokonya mtoto wembe ili asijikate, tusimwache mikono mitupu maana ataurudia. Badali yake tumpe kitu chengine kisicho na madhara (k.m mpira) ashike. Kwa njia hii tutamwokoa na madhara.

 

Katika zama kama hizi zetu ambapo Waislamu kwa jumla, na watoto wao khaswa, wanayajua zaidi ya viongozi wasio Waislamu, bali hata ya walio maadui wa Uislamu, katika nyanja mbalimbali, na husherehekea mazazi yao -- ni lipi bora? Tuwaache waendelee vivyo hivyo? Au tuwaambie waache kufanya hivyo bila ya kuwawekea badali yake? Au tuwawekee badali iliyo nzuri (ya sherehe za mazazi ya Mtume (s.a.w.w.) na viongozi wengine wa Kiislamu) ili tuwaachishe hayo waliyoyashika? Jawabu hapo ninakuachia wewe, ndugu Mwislamu.

 

Mpaka hapa tumemaliza majibu yetu ya hujja zinazotolewa na wanaopinga maulidi; na kuwafikiwa ni kwa Mwenyezi Mungu. Sasa, kama tulivyoahidi katika sura ya pili humu, tutayajibu ya Ahlu-Tawheed waliyoyasema katika makaratasi yao, "Uzushi na Shirk Ndani ya Barzanji na Vitabu Vyengine vya Maulidi".

 

 

 

 

 

 

 

 

4

 

WALIYODAI  "AHLU - TAWHEED" NA  MAJIBU  YETU

 

Katika makaratasi yao hayo, ndugu zetu hao wamenukuu baadhi ya maneno yaliyomo katika Barzanji na Burdah (vitabu viwili vinavyoeleza sifa za Mtume Muhammad s.a.w.w.) na kujaribu, kadri ya ujuzi na uweza wao, kuonyesha kwamba kusema maneno hayo ni shirki. Lakini, kabla ya kutoa majibu yetu, tuanze kwa kuyanukuu maneno yenyewe. Nayo ni mane yaliyotolewa katika Barzanji, na mawili katika Burdah.

 

Katika Barzanji wameyatoa yanayofuata:

1.      "Na kama si yeye (Mtume s.a.w.) asingekuwa Alkhalilu (Ibrahim) na Adam. Na Musa (asingekuwepo) na Issa, bali hata Mulku Suleimani (usingekuwepo)."

 

2.      "Ilisemekana alipotaka Mwenyezi Mungu, Mwenye Ezzi na Alietukuka, kumdhihirisha Mbora wa viumbe vyake, Muhammad, Rehma na Amani za Mwenyezi Mungu zimfikie. Akamuamrisha Jibril achukue Udongo wake (wa kumuumbia nao) kwenye mahali pa kaburi lake karimu".

 

3.      "Alikuwa Mtume akikua mchana mmoja kama anavyokua mtoto mwengine kwa mwezi mzima kwa ajili ya kushughulikiwa na Mwenyezi Mungu".

 

4.      "Akamwonyesha kwa haya macho ya kichwani (ya usoni) aliyomwonyesha. Nayo ni yeye mwenyewe Mwenyezi Mungu."

 

Na katika Burdah wameyatoa yanayofuata:

 

5.      "Kama si yeye (Mtume s.a.w.w.) usingetoka ulimwengu (usingeumbwa)."

 

6.      "Haukupata kunipiga vita Ulimwengu, nikataka nusra kwa Mtume, ila huipata tu."

 

Hayo ndiyo maneno waliyoyanukuu ndugu zetu wa Ahlu-Tawheed kuthubutisha kwamba, katika vitabu hivyo, muna shirki. Wakayaandamiza, pia, na hujja zao za kuyabatilisha hayo.

 

MAJIBU YETU : Kwanza; tukumbuke kwamba tunalojadiliana si kuwa, katika vitabu vya maulidi, muna shirki au hamuna; la! Tunalojadiliana ni: maulidi ni bid'a au si bid'a; ni haramu au si haramu? Sisi, kwa upande wetu, katika makala yetu yaliyopita, kwa kujibu hujja zinazotolewa na wapinga maulidi, tumeonyesha kwamba maulidi si bid'a wala si haramu. Kwa hivyo sasa tunalolingojea kwa wapinga maulidi, wakiwamo Ahlu-Tawheed, ni majibu yao ya hujja tulizozitoa -- kiilimu na kimantiki, kama tulivyofanya sisi.

 

Pili; hata kama itakubaliwa kuwa hayo maneno waliyoyanukuu ni shirki -- na hilo hatulikubali kwa hujja tunayoitoa hapa chini -- hilo haliwi ni hujja ya kuharamishia maulidi au kuyasusia. La sawa kufanywa hapo ni kuyatoa hayo yanayoonekana ni shirki na / au kuyasahihisha; si kuzuia watu kuyasoma. Hivyo, kwa mfano, ndivyo alivyofanya marehemu Sheikh Abdulla Swaleh Farsy katika Wasila wa Nabahani. Yeye alipoona kwamba "Lawlaahu maa kunnaa walaa baaqiina" si sawa, hakuzuia watu, wala yeye hakuacha kuusoma. Alichofanya ni kukibadilisha kipande hicho na kukisoma alivyoona yeye ni sawa: "Lawlal ilaahu…" Hakuutupa wasila wote, wala hakuzuia watu kuusoma kwa sababu tu muna kipande cha maneno asiyoyakubali.

 

Tatu; tunapoyataamali yote madondoo sita waliyoyanukuu Ahlu-Tawheed, ambayo nasi tumeyanukuu hapo juu, hakuna hata moja liwezalo kusemwa ni shirki kwa hujja ifuatayo:

 

Shirki ni kusema / kuamini kuwa Mwenyezi Mungu ana mwenziwe, au ana aliye sawa naye, au ana mfanowe, au ana anayetokana naye. Pia kusema / kuamini kuwa yuko muumbaji mwengine wa ulimwengu asiyekuwa Yeye, au muendeshaji (mudabbir) ulimwengu asiyekuwa Yeye, au mwenye haki ya kuweka sharia asiyekuwa Yeye, au anayelazimika kutwiiwa asiyekuwa Yeye, au kuna mtawala (haakim) asiyekuwa Yeye, au kuna mwenye haki ya kuabudiwa asiyekuwa Yeye.

 

Kwa kuwa hakuna hata moja, ya madondoo sita waliyoyanukuu Ahlu-Tawheed kutoka katika Barzanji na Burdah, linalosema hivyo, vipi basi mutakuwa muna shirki? Kama lipo, tunaomba watwambie ni dondoo lipi kati ya hayo waliyotutajia, na linaingia wapi katika hiyo taarifa ya shirki tuliyoieleza sisi hapo juu. Kama taarifa yetu imeacha mengine yaliyo shirki, basi tunaomba tukumbushwe.

Kwa hakika haikuwa nia yangu kuingia katika masiala ya shirki kwa sababu hilo li nje ya maudhui yetu. Maudhui yetu ni maulidi ni bid'a au si bid'a; ni haramu au si haramu. Na hilo tushalijibu vya kutosha. Lakini, kwa kuwa wafuasi wa madhihabi ya wapinga maulidi hupenda kukibandika jina la bid'a au  shirki kila wanachokipinga wao, nimeona japo kwa ufupi niwaeleze wasomaji wangu jamaa zetu hao hupotelea wapi katika kuielewa shirki ni nini, na si nini!

 

 

 

 

 

5

 

SHIRKI  NI  NINI  NA  SI  NINI

 

Kwa taarifa tuliyoitoa (na tunaomba tuelezwe kama tumeacha kitu katika taarifa hiyo), kati ya madondoo sita yaliyonukuliwa na ndugu zetu hao, matano yametushinda kuelewa vipi yaweza yakawa ni shirki. Kwa hivyo hatutashughulika nayo kwa leo mpaka hapo tutakapofafanuliwa inshallah. Tutakaloshughulika nalo leo ni moja tu lililobaki ambalo, kwa hujja walizozitoa kulipingia, tumeweza kulifahamu lililowafikirisha wao kuwa ni shirki. Nalo ni lile la Buswiri kusema katika Burdah: "Haukupata kunipiga vita Ulimwengu nikataka nusra kwa Mtume ila huipata tu."

 

Kulikosoa hilo, Ahlu-Tawheed wameitaja Sura 3:126 ambayo wameifasiri hivi: "Na msaada hautoki (kwa mwengine yoyote) isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu, Mwenye Nguvu na Mwenye hikima". Kwa kuitaja aya hii, kwa hivyo, tumeelewa kwamba ndugu zetu hao wameyaelewa maneno ya Buswiri hivi: "Kwa kuwa msaada (nasr) hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu, kuuomba kwa mtu mwengine yoyote asiyekuwa Mwenyezi Mungu, hata awe ni Mtume (s.a.w.w.), ni sawa na kumfanya mtu huyo ni Mwenyezi Mungu! Na kufanya hivyo ni shirki; kwa hivyo katika Burdah muna shirki!"

 

MAJIBU YETU : Kwanza; katika tafsiri yao ya hiyo Sura 3:126 wameongeza maneno katika pinde, tuliyoyachapa kwa italiki, ambayo hayamo katika aya hiyo, wala hayaipunguzii maana lau yasingeongezwa.

 

Pili; kama maana ya "msaada hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu" ni kwamba haturuhusiwi kutafuta msaada kwa asiyekuwa Yeye, au asiyekuwa Yeye hana msaada wa kuutoa, basi ilikuwaje watu wa Madina wakaitwa answaar (wasaidizi)? Walimsaidia nani? Huyo aliyesaidiwa, aliukosa msaada wa Mwenyezi Mungu hata wakaingia kati wao? Na sisi Waislamu, pamoja na Mtume wetu (s.a.w.w.), tunamshirikisha Mwenyezi Mungu kwa kuwaita answaar watu wa Madina?

 

Tunaposoma Sura 3:81 tunaona jinsi Mwenyezi Mungu alivyochukua ahadi kwa Mitume Yake kwamba itamsaidia / itamnusuru (latansurunnahuu) Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Jee, kama "msaada hautoki (kwa mwengine yoyote) isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu," ilikuwaje hapo, Yeye Mwenyewe, akautaka kwa asiyekuwa Yeye? Jee, kwa kitendo hicho, Mwenyezi Mungu -- Mwenyezi Mungu apishe mbali! -- alikusudia kuifanya Mitume Yake ni miungu?

 

Katika Sura 7:157, kati ya sifa za waumini ambao "ndio wenye kufaulu", ni wale ambao wamemsaidia / wamemnusuru (wanaswaruuhu) Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Jee, kama "msaada hautoki (kwa mwengine yoyote) isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu", kwa nini akawaagiza waumini wamsaidie Mtume Wake? Kwa sifa hiyo hapo, ndio Mwenyezi Mungu amewafanya waumini kuwa ni miungu? Mwenyezi Mungu -- Mwenyezi Mungu apishe mbali -- hapo amefanya shirki?

 

Hali kadhaalika; tunaposoma Sura 28:15 tunaona jinsi jamaa yake Nabii Musa (a.s) "alivyomuomba msaada" (fastaghaathahuu) juu ya adui yake. Jee, Nabii Musa (a.s) alimrukia jamaa yake huyo, na kumwambia asilete shirki kwa kumuomba yeye msaada badali ya Mwenyezi Mungu? La! Alimsaidia; na siku ya pili (Sura 28:18) yule aliyeomba msaada jana (istanswarahuu) akamuomba tena! Jee, kama "msaada hautoki (kwa mwengine yoyote) isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu", kwa kutoa msaada wake huo, Nabii Musa (a.s) alikuwa Mwenyezi Mungu, au hakujua kuwa "msaada hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu"?

 

Kwa kutaja mifano hiyo hapo juu, sisi tusomao maulidi hatukusudii kukanusha yaliyomo katika aya iliyotajwa na wapinga maulidi, kuwa "msaada hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu"; hasha! Tunalokusudia ni kufahamisha kwamba: maneno yanapofanana, si lazima na  maana yafanane (yawe mamoja). Kwa hivyo, msaada ambao Buswiri aliuomba kwa Bwana Mtume (s.a.w.w.), na sisi huukariri tunapoisoma hiyo Burdah, sio msaada ambao huombwa kwa Mwenyezi Mungu. Ni majina tu kufanana -- kama ulivyokuwa ule ambao Mwenyezi Mungu alimtakia Mtume Wake kwa Mitume mengine, na aliotutaka sisi waumini tumpatie Mtume Muhammad (s.a.w.w.), na ambao watu wa Madina walimpatia Bwana Mtume (s.a.w.w.) hata wakaitwa answaar (wasaidizi wake), na ule ambao Nabii Musa (a.s) alimpatia jamaa yake.

 

Msaada wa Mwenyezi Mungu unatokana na Yeye Mwenyewe; hakupawa na yoyote uweza huo wa kusaidia. Lakini wa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, akiwamo Mtume Muhammad (s.a.w.w.), si wake mwenyewe; ni wa kupawa (kuwezeshwa na Mwenyezi Mungu). Na hapo ndipo palipo na tafauti baina ya shirki ni nini, na si nini.

 

Ukiamini kwamba Mtume (s.a.w.w.) -- yeye mwenyewe,  bila ya kupawa uweza huo na Mwenyezi Mungu -- aweza kusaidia; hiyo ni shirki. Na hilo silo alilokuwa akiliamini Buswiri, wala silo tunaloliamini sisi tusomao maulidi. Lakini ukiamini kuwa msaada uwezao kupawa na Mtume (s.a.w.w.) ni ule aliowezeshwa yeye na Mwenyezi Mungu; hiyo si shirki. Na hilo ndilo alilokusudia Buswiri katika Burdah, na ndilo tunaloliamini sisi tunaosoma maulidi. Kwa hivyo kubwa ambalo wapinga maulidi waweza kutwambia sisi ni kuwa Mtume (s.a.w.w.) hakuwa / hana uweza huo; kwa hivyo ni kazi bure kumuomba hivyo -- jambo ambalo hatulikubali kwa sababu ya hujja tulizonazo. Lakini hawawezi kutwambia ni shirki, kwa mifano mingi tuwezayo kuwatolea katika Qur'ani Tukufu.

 

Wapinga maulidi hupotea wapi

Wapinga maulidi, wanaposoma vitabu vya maulidi, wakaona kuwa Mtume (s.a.w.w.) amesifiwa kwa neno alilosifiwa Mwenyezi Mungu, au kitendo chake kimetajwa kwa neno ambalo, kwa kawaida, hunasibishwa nalo Mwenyezi Mungu -- wanapoona hayo, moja kwa moja husema ni shirki, kwa sababu hivyo ndivyo wanavyoielewa wao shirki, na hali hivyo sivyo.

 

Neno lililotumiwa kumsifia Mwenyezi Mungu, linapotumiwa kumsifia Mtume (s.a.w.w.), halimfanyi Mtume kuwa ni Mungu (kwa hivyo si shirki) kama ambavyo, vile vile, neno lililotumiwa kuelezea kitendo cha Mtume (s.a.w.w.), halimfanyi Mtume kuwa ni Mungu. Kwa kutolielewa hili ndipo wapinga maulidi -- wao na viongozi wao -- walipokosea na kudai kuwa vitabu vya maulidi vina shirki!

 

Kuthubutisha kosa lao hilo, hapa chini tunayataja mifano michache tu (sio yote) kutoka katika Qur'ani Tukufu:

 

1.      Tunaposoma Sura 2:143, tunamuona Mwenyezi Mungu anavyojisifu kuwa Yeye ni rauufun (Mpole) na rahiimun (Mwenye kurehemu). Na tunaposoma Sura 9:128, tunamuona Mwenyezi Mungu, Yeye Mwenyewe, anamsifu Mtume Wake (s.a.w.w.) kwa sifa zizo hizo za rauufun rahiimun! Jee, kwa kufanana matamko ya sifa hizo, Mwenyezi Mungu alikusudia kumfanya Mtume Wake ni Mungu kama Yeye? Jee,  sisi tunapomsifu Mtume kwa sifa hizo, huwa tumefanya shirki kwa sababu tu matamko yaliyotumiwa yanafanana?

 

Jawabu ni: La! Isipokuwa kama tutaamini kuwa uraufu na urahimu wa Mtume (s.a.w.w.) ni sawa na ule wa Mwenyezi Mungu! Na hilo, sisi watu wa maulidi, hatulisemi wala hatuliamini. Tunaloliamini sisi ni kwamba uraufu na urahimu wa Mwenyezi Mungu ni Wake Mwenyewe kwa asili (bil aswaala / independently); wa Mtume (s.a.w.w.) ni wa kupawa na Yeye, Mola wake. Kama kumsifu Mtume kwa sifa hizo ni shirki kwa sababu tu zimefanana na za Mwenyezi Mungu, basi na wapinga maulidi nao pia ni mushrikina kwa sababu hatuamini kwamba wanapoifikia aya hiyo (Sura 9:128), kama Waislamu, huiruka wakaacha kuisoma, au huibadilisha maneno yake.

 

2.      Tunaposoma Sura 16:70, tunaona kwamba Mwenyezi Mungu ndiye aliyetuumba na ndiye anayetufisha / anayetuuwa (yatawaffaakum); na tunapoisoma Sura 32:11, tunaona kwamba atakayetufisha (yatawaffaakum) sisi ni "malaika wa mauti". Sasa tushike lipi hapo, maana neno lililotumiwa kuelezea kitendo hicho cha kutoa roho ni lilo hilo moja: yatawaffaakum? Afishaye ni Mwenyezi Mungu, au ni huyo malaika?

 

Tukisema ni Mwenyezi Mungu peke Yake, tutakuwa tunaikanusha Qur'ani kwa sababu Qur'ani yiyo hiyo imetwambia kuwa na malaika huyo naye huifanya kazi hiyo. Na tukisema ni malaika peke yake, tutakuwa vile vile tunaikanusha Qur'ani kwa sababu Qur'ani yiyo hiyo imetwambia kuwa Mwenyezi Mungu naye huifanya kazi hiyo. Sasa ni nani basi? Ni wote wawili?

 

Jawabu ni: Ndiyo! Ni wote wawili; lakini pana tafauti. Japokuwa maneno (yatawaffaakum) yaliyotumiwa yanafanana, tawaffaa ya Mwenyezi Mungu si sawa na ya malaika. Ya Mwenyezi Mungu ni ya uweza Wake alionao Yeye Mwenyewe kwa asili. Ile ya malaika si hivyo. Yake ni ya "kuwakilishwa" (alladhii wukkila bikum) na Mwenyezi Mungu, kama aya yake (Sura 32:11) inavyofafanua. Kwa hivyo, ukiamini hivyo; hiyo si shirki. Lakini ukiamini kuwa uweza wa kufisha alionao malaika ni sawa na ule alionao Mwenyezi Mungu; hiyo, bila shaka yoyote, itakuwa ni shirki. Na ni Mwislamu gani anayeamini hivyo?

 

3.      Tunaposoma Sura 22:6, tunaona kwamba Mwenyezi Mungu ndiye anayefufua (yuhyii) wafu; na tunaposoma Sura 3:49, tunamuona Nabii Isa (a.s), mtume wa Mwenyezi Mungu, anasema kuwa yeye naye anafufua (uhyii) wafu! Sasa basi, kwa kusema hivyo, Nabii Isa hapo alijifanya ni Mungu? Au sisi, tunapoisoma aya hiyo katika Qur'ani, huwa tunamshirikisha Nabii Isa na Mwenyezi Mungu?

 

Jawabu ni: Ndiyo, kama tutaamini kuwa Nabii Isa (a.s) alikuwa nao uweza huo yeye mwenyewe. Lakini kama tutaamini, kama alivyoeleza yeye mwenyewe Nabii Isa katika aya yiyo hiyo, kuwa aliweza kufanya hilo "kwa idhini ya Mwenyezi Mungu" (bi idhnillaahi), hapo hatutakuwa tumemshirkisha na Mwenyezi Mungu japokuwa neno lililotumiwa kwa wote wawili -- yuhyii na uhyii -- ni lilo hilo moja.

 

4.      Tunaposoma Sura 25:2, tunaona kuwa Mwenyezi Mungu ndiye aliyeumba kila kitu. Sisi binadamu (Sura 32:7) alituumba (khalaqa) kwa udongo, kisha (Sura 32:9) akatuvivia / akatupulizia (nafakha fiihi) roho Yake, tukawa. Hali kadhaalika Nabii Isa (a.s); kwa mujibu wa Sura 3:49 anasema, "…Ninawaumbia nyinyi (akhluqu lakum) kwa udongo, kama sura ya ndege, kisha nampuliza (anfukhu fiihi), mara anakuwa ndege …"

 

Jee, Nabii Isa hapo alikuwa Mungu? Au sisi Waislamu -- tunaosoma maulidi na tunaoyapinga -- tunapoisoma aya hiyo, pamoja na kuwa ametumia maneno yale yale (akhluqu lakum na anfukhu fiihi) yaliyotumiwa na Mwenyezi Mungu, humfikiria Nabii Isa (a.s) kuwa ni Mungu? Hasha! Kwa nini? Kwa sababu, katika aya hiyo hiyo, amesema kuwa ameweza kulifanya hilo "kwa idhini ya Mwenyezi Mungu" (bi idhnillaahi); si kwa uweza wake yeye mwenyewe.

 

Kwa mifano mine hiyo tuliyoitaja hapo juu, tumeona kwamba linalozingatiwa katika kuhukumu jambo kuwa ni shirki au la, si maneno yanayotumiliwa Mwenyezi Mungu na Mtume Wake kufanana; hasha! Linalozingatiwa ni hilo tunalomnasibisha nalo Mtume, au kiumbe yoyote, linatokana na uweza alionao yeye mwenyewe kwa asili au aliopawa na Mwenyezi Mungu? Tukiamini hilo la kwanza,, itakuwa ni shirki. Tukiamini hilo la pili, itakuwa si shirki. Na hili ndilo aliloliamini Buswiri na wanaoyakubali ya Burdah: kwamba uweza alionao Mtume (s.a.w.w.) wa kutoa msaada ni wa kupawa na Mwenyezi Mungu; si wake mwenyewe kwa asili.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

6

 

WALIYODAI "WAKEREKETWA"

 

Sasa tuyajibu yaliyochapishwa na "Wakereketwa wa Sunnah Malindi" kwa jina la "Majibu ya Abdillah Nassir". Makala tunayoyajibu humu ni yale ya "chapa ya kwanza". Sijui kama, baada ya hiyo, wametoa chapa nyengine kwa sababu mimi sijaziona.

 

Katika makala yao hayo, walianza kwa kusema: "Tunashindwa kukuelewa tukueke wapi …"

 

MAJIBU:  Tunalolijadili ni maulidi ni bid'a au ni haramu, au si bid'a wala si haramu? Sijadiliwi mimi niwekwe wapi. Kwani "wakereketwa" wakishajua pa kuniweka, ndio watajua hukumu ya maulidi ni ipi; ni bid'a / haramu au si bid'a / haramu?

 

Kisha wakasema: "… Sifa za mwanzo ilikuwa sunna, ukawa mstari wa mbele kwa kuamrisha, kufanya, kukataza lolote la uzushi au haliambatani na sheria ya Mwenyezi Mungu na Sunna ya Mtume S.A.W."

 

MAJIBU:  Hilo ni kweli; na mpaka hii leo msimamo wangu ungali huo huo. Tafauti iliyoko hapa, baina ya "wakereketwa" na mimi, ni kwamba baadhi ya mambo wanayoyaona wao kuwa ni "uzushi", mimi siyaoni hivyo kwa sababu bid'a wanavyoielewa wao sivyo ninavyoielewa mimi. Kwa ajili hii, katika uhai wangu wote mpaka hapa nilipofika, sijapata kupinga maulidi hata siku moja. Kinyume cha  hilo, nimekuwa nikihudhuria maulidini, na wakati mwengine kutoa khutba -- si hapa Mombasa tu, bali Afrika ya Mashariki nzima na hata ng'ambo, kuanzia 1955 (nilipoanza kutoa khutba hadharani) hadi hii leo. Kama uko ushahidi wa mimi kupinga maulidi, nawaomba "wakereketwa" watutolee.

 

Wakasema tena:  "PILI: Ukawa kadiani ukapinga kwamba Mtume S.A.W  siyo Mtume wa mwisho ikawa Gulam Ahmed ndiye wa mwisho kuambatana na safari yako isiyoeleweka, ukapinga kabisa thibitisho la Kuran Mtume Muhammad S.A.W  kwamba ndiyo wa mwisho".

 

MAJIBU:  Astaghfirullah! Watu hawa hawamchi Mola wao? Hayo yote ni uwongo! Kama "wakereketwa" wadai hivyo, ninawaomba wawatolee Waislamu ushahidi wao. Wangu mimi, mbali na ninayoyasema katika darasa zangu, ni kijitabu changu kiitwacho Hakika ya Ukadiani ambacho, miaka isiyopungua thalathini iliyopita, kilichapishwa na kuenezwa na National Union of Kenya Muslims wakishirikiana na Ansaar Muslim Mission ya Mombasa. Humo nilieleza uwongo wa Mirza Ghulam Ahmad na ukafiri wa Ukadiani.

 

Vile vile, miezi michache inayokuja inshallah, nina azma ya kuchapisha tafsiri ya Kiswahili ya Sura Al-Ahzaab ambamo ndani yake nimetoa ushahidi mwingi sana, ambao haujapatapo kuchapishwa kwa urefu hivyo kwa lugha ya Kiswahili hadi hii sasa, kuthubutisha kuwa Muhammad (s.a.w.w.) ni Mtume wa Mwisho, na kuwa hakuna mtume mwengine baada yake. Pia nimejibu kwa tafsili upotofu wote ambao Makadiani wameuandika katika maelezo yao ya Sura 33:40 katika tafsiri yao ya Kiswahili ya Qur'ani Tukufu.

 

Wakaendelea kusema: "TATU: Ukawa Shia, ukamkadhibisha Mwenyezi Mungu pamoja na Mtume wake S.A.W.  na kwamba Jibril alifanya hiana, kwamba Kuran ina kasoro ukawatukana wake za Mtume S.A.W. pamoja na maswahaba zake radhia allahu anhum …"

 

MAJIBU:  Ni kweli mimi ni Shia Ithnaashari. Hilo silifichi wala silionei aibu kwa sababu ninaamini kwamba kuwa Shia si kuwa kafiri. Nguzo tano zinazokubaliwa na Waislamu wote, mashia vile vile wanazikubali. Hali kadhaalika nguzo za imani.

 

Kuwa Shia "wanamkadhibisha Mwenyezi Mungu pamoja na Mtume wake S.A.W."; huo ni uwongo ulio wazi. Kwa Shia, yoyote anayefanya hivyo huwa ni kafiri wa kutiwa Motoni. Hilo ndilo lililomo katika vitabu vyao.

 

"Kwamba Jibril alifanya hiana"; hilo nalo pia ni uwongo. Ukisoma vitabu vya fiqhi vya madhihabi ya Shia utaona kwamba anayeamini hivyo si kafiri tu, bali ni najisi kamwe! Ngozi ya mwili wako ikigusana na ngozi ya mwili wake lazima yako uioshe. Haya! Ikiwa hiyo ndiyo imani yao, vipi watu hao watarudi waseme wao kuwa "Jibril alifanya hiana"?!

 

"Kwamba Kuran ina kasoro"; hilo pia ni uwongo. Imani ya Shia ni kama ile ya Waislamu wote: kuwa hii Qur'ani tuliyonayo sasa ndiyo ile ile iliyokuwako wakati wa Mtume Muhammad (s.a.w.w.) shilingi kwa ya pili. Haikubadilika hata kitone. Kwa maelezo zaidi juu ya jambo hili, kwa anayetaka kujua msimamo wa Shia, ninamshauri asome kitabu changu kiitwacho Shia na Qur'ani : Majibu na Maelezo, kinachoweza kupatikana bure kutoka ofisi yoyote ya Bilal Muslim Mission ya Mombasa (S.L.P. 82508) au ya Dar es Salaam (S.L.P. 20033). Humo utaona majibu ya Shia juu ya tuhuma zote juu ya Qur'ani Tukufu zinazotolewa na watu kama kina "wakereketwa".

 

Kuwa nimewatukana "wake za Mtume (s.a.w.w.) pamoja na maswahaba zake radhia allahu anhum"; hilo pia ni uwongo. Nimewatukana wapi? Ninawaomba "wakereketwa" watoe ushahidi wa nilipofanya hivyo.

 

Imani yangu mimi, na imani ya Shia wote, juu ya maswahaba nimeieleza katika kitabu changu chengine kiitwacho Shia na Sahaba : Majibu na Maelezo ambacho, vile vile, unaweza kukipata kutoka Bilal Muslim Mission. Humo nimechapisha kwa Kiarabu, pamoja na tafsiri yake ya Kiswahili, dua ya kuwaombea Mwenyezi Mungu maswahaba ambayo Shia huisoma. Kwa wale wasiolijua hilo, dua kama hiyo haipatikani katika madhihabi yoyote mengine ya Kiislamu isipokuwa ya Shia. Basi vipi watawaombea Mungu na hapo hapo wawatukane?

 

"Wakereketwa wa sunnah Malindi" wameendelea kusema: "NNE: Safari yako ya "Transit" haijaeleweka itatokomea wapi katika dini, kwa sababu hoja unazotupatiya bado hatujazielewa rasmi…"

 

MAJIBU: Safari yangu ya transit (mpito) waliyoikusudia ndugu zetu hao ni hili la mimi kuwa Shia baada ya kuwa mfuasi wa Imam Shaafi'i (Sunni). Na hayo wameyaandika kwa namna ya kumfikirisha yoyote anayeyasoma makala yao hayo kuwa nimefanya kosa kubwa -- la kutoka madhihabi mamoja na kuingia madhihabi mengine. Wala hilo si kweli -- si kosa wala si ila -- kwa ushahidi wa yaliyofanywa na wanazuoni kadhaa wa kadhaa ambao mimi siwi hata viatu vyao!

 

Kwa mfano, tunaposoma historia tunaona wanazuoni kadhaa wa kadhaa waliobadilisha madhihabi kwa kutoka yale waliyozaliwa nayo wakaingia mengine, na mara nyengine wakarudi tena katika yale yale yao ya kwanza!

 

Katika karne za nyuma, tunasoma ya Sheikh Muhammad bin Abdalla aliyefariki mwaka wa 268 Hijria. Huyu kwanza alikuwa akifuata madhihabi ya Imam Maalik. Imam Shaafi'i alipohamia Misri, mwanachuoni huyo aliwacha madhihabi ya Maalik, akaingia ya Shaafi'i; kisha akarejea tena kwa Maalik. Mwengine ni Abu Ja'far bin Nasr at-Tirmidhi aliyefariki mwaka 295 Hijria. Huyu alikuwa mkubwa wa Mashaafi'i huko Iraq. Lakini mwanzo alikuwa Hanafi; alipokwenda hijja ndipo alipotoka, akawa Shaafi'i. Wa tatu ni al-Khatib al-Bughdadi al-Hafidh, aliyefariki mwaka wa 493 Hijria. Huyu alikuwa Hambali, kisha akawa Shaafi'i. Wane ni Abuu Said aliyefariki mwaka wa 562 Hijria. Yeye alikuwa Hanafi mwanzo; kisha akawa Shaafi'i. Wa tano ni Sayf al-Aamadi, mwanachuoni mashuhuri wa ilimu ya Usuli aliyefariki mwaka wa 631 Hijria. Yeye alikuwa Hambali mwanzo; halafu akawa Shaafi'i. Wa sita ni Sheikh Muhammad bin Dahhaan aliyekuwa bingwa wa ilimu ya Nahau (Sarufi). Huyu alikuwa Hambali mwanzo; kisha akawa Shaafi'i. Khalifa wa zama zake alipotaka mwanachuoni wa Nahau ili amfundishe mwanawe fani hiyo, akawa Hanafi. Kisha akarudi akawa Shaafi'i tena!

 

Kuna na Sheikh Taqiyyud Diin bin Daqiiq. Huyu mwanzo alikuwa Maaliki, kisha akawa Shaafi'i. Na Sheikh Abdulaziz bin al-Khuzaa'i aliyekuwa kati ya wakubwa wa madhihabi ya Maalik. Lakini Imam Shaafi'i alipokwenda Baghdad, aliyawacha ya Maalik akamfuata Shaafi'i. Kuna na Abu Ja'far at-Twahaawi aliyekuwa Shaafi'i, akasoma kwa mjombake (al-Muzani). Baadaye akawa Hanafi. Mbali Ibn Faaris. Huyu alikuwa Shaafi'i kwa kumfuata babake. Kisha akawa Maaliki.

 

Hayo ni ya karne nyingi zilizopita, na ya nchi za mbali. Hebu sasa tuangalie ya hii karne yetu, na ya nchi zetu za Afrika ya Mashariki.

 

Wa kwanza ni Sheikh Aly bin Abdalla Mazrui, babake Sheikh Al-Amin bin Aly Mazrui, aliyekuwa Kadhi Mkuu wa Kenya. Huyu mwanzo alikuwa Ibadhi; kisha akawa Shaafi'i. Wa pili ni Sheikh Muhsin bin Ali Barwani, babake Sheikh Ali Muhsin Barwani aliyekuwa kiongozi wa Chama cha Hizbu, Zanzibar na mwandishi wa Tafsiri ya Qur'ani Tukufu kwa Kiswahili. Huyu naye alikuwa Ibadhi vile vile; lakini kisha akawa Shaafi'i. Wa tatu ni Sayyid Alwy Ahmad Badawy (Mzee Mwenye) wa Lamu aliyekuwa Shaafi'i; lakini sasa ni Shia Ja'fari kama mimi. Wane ni Sayyid Hassan Ahmad Badawy wa Lamu vile vile, aliyekuwa Shaafi'i mwanzo; kisha akawa Shia Ja'fari. Lakini sasa amerudi kuwa Shaafi'i!

 

Wala si hao tu, bali hata wao "wakereketwa wa sunnah Malindi", pamoja na mashekhe wao na viongozi wao, ni hali kadhaalika. Kabla ya wao kuingia haya madhihabi wayafuatayo sasa, walikuwa wakifuata madhihabi ya Shaafi'i ambayo ndimo walimozaliwa.

 

Sasa ni lipi la kioja nililolifanya mimi? Naomba nielezwe.

 

Kwa kuwa Shia, mimi sijatoka katika Uislamu. Yote ya msingi yanayokubaliwa na Waislamu, na sisi Shia tunayakubali. Kama ndugu zetu "wakereketwa" waamini kuwa sisi Shia tuna mambo yoyote ya kikafiri, basi watoe makaratasi yao kuyaeleza hayo moja moja -- kiilimu na kwa lugha ya adabu, bila ya matusi -- ili tupate kuyajadili kama tulivyofanya haya ya maulidi.

 

Kwa faida ya ndugu wasomaji wa makala haya, kama vile ambavyo kuna mambo ambayo madhihabi ya Kishia hukhitalifiana na madhihabi mane ya Kisunni, hali kadhaalika kuna  mambo ambayo kila madhihabi matatu ya Kisunni hukubaliana na ya Kishia, na moja tu la Kisunni likawa peke yake. Pia kuna na mengine ambayo madhihabi ya Kisunni na ya Kishia hukubaliana, na ya kina "wakereketwa" peke yao yakawa tafauti!. Kama wanataka tuyajadili hayo, ahlan wasahlan.

 

Mpaka hapa, tumekoma mjadala wetu kuhusu maulidi. Twataraji wasomaji wetu -- wa maulidi na wapinzani wao -- wamestafidi.

 

Ifikapo Rajab ya mwaka huu tulionao inshallah, tutaanza mfululizo mpya wa makala ya kueleza: hawa wapinga maulidi, khitma, tawasuli, wakavunja makaburi na mihrabu, na kama hayo, ni kina nani? Wanafuata madhihabi gani? Madhihabi hayo yalianza wapi? Lini? Yalianzishwa na nani? Yaliingia lini huku kwetu Afrika ya Mashariki? Vipi? Yameeneaje? Jee, wanaamini kuwa Waislamu wasiokuwa na itikadi kama zao -- wakiwamo masunni -- ni Waislamu? Na mengi mengine.

 

Wassaalaamu alaykum.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

… basi wale waliomwamini yeye

(Mtume Muhammad)

na kumhishimu na kumsaidia,

na kuifuata nuru iliyoteremshwa pamoja naye;

hao ndio wenye kufaulu.

 

(Surah 7:157)

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Kimechapishwa na kutolewa na

 

BILAL MUSLIM MISSION OF KENYA

P.O. BOX 82508 MOMBASA TEL: 229641 FAX 230909

e-mail : tableegh@kenbilal.org