YALIYOMO
www.al-islam.org and ebooked by www.ShiaLibrary.com and www.islamkutuphanesi.com . May Allah be pleased with all. |
Lifuatalo ni toleo maalumu
la kitabu
kiitwacho
"Kumtukuza Mtume
Muhammad (s.a.w.w.)"
chenye mkusanyiko wa mada za kuadhimisha kuzaliwa kwa
Mtume Muhammad (s.a.w.w.)
Yaliyomo
ni:
-
Vidokezo juu ya maisha ya muasisi wa Uwahabi
-
Kuadhimisha kuzaliwa Mawalii wa Mwenyezi Mungu na kufa kwao
-
Qur'ani na kuwatukuza Manabii na Mawalii
-
Uzindushi
-
Maneno na matendo ya mawahabi yanapingana
Agiza nakala yako kutoka kwa:
Bilal Muslim
Sifa njema zote ni za
Mwenyezi Mungu, Bwana wa viumbe vyote. Na swala na salamu zimshukie Hashimu,
Mtume Wake muadhamu (s.a.w.w.), na aali zake kiramu, na wote wenye kufuata
nyayo zao.
Baina ya tarehe 4 Rabiiul
Awwal, 1423 / 17 Mei, 2002 na 7 Jamaadath Thaani, 1423 / 16 Agosti, 2002
nilitoa mfululizo wa makala kumi na tatu juu ya maulidi ya Mtume Muhammad
(s.a.w.w.). Katika makala hayo, kwa kujibu hujja zinazotolewa na wale
wanaopinga maulidi, nilijaribu kuonyesha kuwa maulidi si bid'a (uzushi) wala si haramu.
Ninamshukuru Mwenyezi Mungu
(s.w.t.) kwa makala hayo kupokewa vizuri na wote walioyasoma. Na kwa kuitika
maombi
Makala hayo na kitabu hiki
kisingetoka
ABDILAHI NASSIR
17 Jamaadath Thaani, 1423
26 Agosti, 2002
1
Maulidi ni Kiswahili cha
neno la Kiarabu, mawlid. Neno hili
lina maana ya "mazazi" au "kuzaliwa kwa
" (birthday). Kwa kawaida, linapotumiwa na
Waislamu, huwa na maana ya siku aliyozaliwa Mtume Muhammad (s.a.w.w.), au hafla
ya kuisherehekea siku hiyo.
Waislamu wa ulimwengu mzima,
ifikapo tarehe 12 ya Mfungo Sita (Rabiul
Awwal), husoma maulidi na kuisherehekea siku hiyo kwa furaha kubwa. Sherehe
hizo, kwa dasturi, haziishii tarehe hiyo tu, bali huendelea hata kwa miezi
miwili mitatu baada ya hapo. Hili huwa ni kwa sababu ya Waislamu wa kila
nyumba, kila mtaa, kila mji na kila nchi kutaka kushiriki katika sherehe hizo na
kupata baraka zake. Vile vile huwapa Waislamu nafasi ya kutembeleana na
kushirikiana katika sherehe hizo - jambo ambalo lisingewezekana lau watu wote
wangeliamua kuzifanya sherehe hizo siku hiyo hiyo moja tu.
Kwa
nini kusoma maulidi?
Waislamu husoma
maulidi kwa sababu mbalimbali. Kati ya hizo ni:
(i)
kuikumbuka na kuitukuza siku aliyozaliwa
mbora wa viumbe vyote, aliyetutoa vizani na kututia kwenye nuru;
(ii)
ni njia moja ya kutoa shukrani zetu kwa neema
hiyo;
(iii)
katika sherehe hizo, hupatikana fursa ya
kukumbushana maisha ya bwana mkubwa huyo na mafunzo yake;
(iv)
hupatikana fursa ya Waislamu wa madhihabi na
mataifa mbalimbali kushirikiana na kuziweka kando hitilafu zao; na
(v)
mikusanyiko hiyo huleta athari kwa wasio
Waislamu ya kuupenda Uislamu, na hata kusilimu.
Wanaopinga
na sababu zao
Lakini, hata
hivyo, kuna baadhi ya Waislamu -- japokuwa wao si wengi kama wanaoyasoma --
ambao hupinga kusomwa maulidi; na hutoa sababu zao. Kati ya sababu hizo ni:
(i)
maulidi hayakuwako zama za Mtume Muhammad
(s.a.w.w.). Basi kwa nini yazuliwe sasa?
(ii)
hayakusomwa na maswahaba wala waandamizi wao.
Kama kweli yangelikuwa ni sawa kuyasoma, bila shaka mabwana wakubwa hao
wangelikuwa ni wa mbele kufanya hivyo;
(iii)
kuweka ada ya kusoma maulidi ni kuigiza
Wakristo walioweka siku ya Krismasi; na Mwislamu haruhusiwi kufanya hivyo;
(iv)
kwenye sherehe za maulidi hufanywa baadhi ya
mambo ambayo ni ya munkar
(yanayochukiza, bali ni haramu kamwe, katika sharia ya Kiislamu); na
(v)
hakuna ushahidi wowote, wa Qur'ani wala
Hadithi za Mtume Muhammad (s.a.w.w.), unaothubutisha usawa wa kuyasoma maulidi,
sikwambii kuyatilia nguvu.
Kwa nguvu ya hujja hizo,
mara nyingi viongozi wa wanaopinga maulidi huwaonyesha wafuasi wao kuwa wale
wanaosoma maulidi ni watu waliopotea kwa "kuzua" mambo yasiyo na
msingi katika dini yetu hii. Jambo hili limeleta mchafuko -- unaofufuka
aghalabu kila ifikiapo miezi ya kusoma maulidi -- ambao unahatarisha umoja na
masikizano, sio baina ya Waislamu wa madhihabi mbalimbali peke yao, bali hata
wale wa madhihabi mamoja!
Mchafuko huu huzidi kukua
kwa sababu ya lugha kali inayotumiwa na pande zote mbili -- za wanaounga na wanaopinga maulidi --
katika kutetea misimamo yao; na hilo haliwezi kusaidia katika kutatua usawa uko
wapi. Liwezalo kutatua hitilafu hii ni kuijadili ki-ilimu na kwa lugha nzuri ya
kuhishimiana. Na hilo ndilo nililokusudia kulifanya, kuanzia makala
yanayofuatia haya, Inshallah.
2
HUJJA
ZA WAPINZANI
Hujja
yao ya kwanza ni kwamba: maulidi hayakuwako zama za Mtume Muhammad (s.a.w.w.) Kwa
hivyo, kuyaleta baada ya yeye kufariki dunia, ni bid'a (uzushi). Na kila bid'a,
kwa maneno yake mwenyewe Bwana Mtume (s.a.w.w.), ni upotevu. Kwa hivyo, kila
anayesoma maulidi amepotea!
MAJIBU
YETU: Ni kweli kwamba maulidi,
hivi tunavyoyasoma, hayakuwako zama za Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Lakini si kweli kwamba, kulifanya kila ambalo halikuwako zama hizo, ni
upotevu. Kama ni hivyo, basi bila shaka Waislamu wote leo -- wakiwamo wanaopinga maulidi -- wangelikuwa wamepotea
kwa kuwa (katika zama zao mbalimbali) wamefanya, na wanaendelea kufanya, mambo
ambayo hayakuwako zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.)!
Kwa mfano, katika zama za
Bwana Mtume (s.a.w.w.), misikiti haikuwa ikitandikwa chochote (watu wakisujudu
juu ya mchanga); lakini leo inatandikwa majamvi, busati na mazulia! Kiwanja
kitakatifu cha Al-Kaaba kilikuwa ni mchanga mtupu na mawe; lakini leo
kimetandikwa marumaru! Watu walikuwa wakenda kuhiji kwa kupanda ngamia au
majahazi; lakini leo wanakwenda kwa ndege, meli za kisasa na mabasi ya anasa (luxury)! Watu, walipokuwa wengi
msikitini, walikikhutubu kwa kupaza sauti zao; lakini leo wanatumia vipaza
sauti (loud speakers)! Misahafu
ilikiandikwa kwa mkono, juu ya ngozi na mifupa, na kutolewa nakala chache;
lakini leo inachapwa kwa mashini, juu ya karatasi za fakhari, na kutolewa
nakala mamilioni kwa mamilioni!
Lakini hakuna anayesema --
hata hao wanaopinga maulidi hawasemi -- kwamba Waislamu waliobuni mambo hayo
wametuletea bid'a au wamepotea. Kwa
nini? Kwa sababu kwao wao, na kwa wanaosoma maulidi, uzushi wa aina hiyo si bid'a; sio alioukusudia Bwana Mtume
(s.a.w.w.). Alioukusudia yeye ni ule wa kuzua jambo katika dini hii ambalo halitokani
nayo (maa laysa minhu). Hilo ndilo lililo wazi kutokana na Hadithi
mashuhuri ya Bwana Mtume (s.a.w.w.) inayosema: "Yoyote atakayezua, katika dini yetu hii, jambo ambalo halitokani nayo, litarudishwa
(litakataliwa)."
Ukiitaamali vizuri Hadithi
hiyo, itakudhihirikia kwamba Bwana Mtume (s.a.w.w.) hakutuzuia kuzua (kubuni), katika dini hii, kila ambalo halikuwako zama zake. Kama angelitaka kutuzuia hivyo,
Hadithi hiyo isingelisema hivyo, bali ingelisema hivi: "Yoyoye atakayezua
jambo katika dini yetu hii, litakataliwa." Na lau ingelisema hivyo, basi
yote yale tuliyoyataja hapo juu yasingeliruhusiwa; yangelikuwa bid'a.
Lakini Hadithi haikusema
hivyo. Ilivyosema ni:
"Yoyote atakayezua
ambalo halitokani nayo,
litakataliwa." Kwa kuongeza kifungu cha maneno tulichokichapa kwa italiki (yaani "ambalo
halitokani nayo"), ni wazi kwamba Mtume Muhammad (s.a.w.w.) hakukusudia
kuwazuia Waislamu kufanya kila ambalo
halikuwako zama zake. Alilolikusudia ni kutuachia wazi mlango wa kubuni mambo
katika dini hii bora tu yawe
yanatokana nayo.
Sasa suali hapa ni: jee,
maulidi si katika mambo yanayotokana na "dini hii", hata kama
hayakuwako zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.)?
Majibu yetu ni: Maulidi, na
yaliyomo maulidini, si mageni na "dini hii", bali yanatokana nayo,
kama tutakavyobainisha kwa urefu zaidi katika majibu yetu ya hujja Na. (v) ya
wapinzani wake inshallah.
Kwa hivyo, kuwa tu jambo
halikuwako zama za Mtume Muhammad (s.a.w.w.) si hujja ya kuwazuia Waislamu
kulifanya. Wanalozuiliwa Waislamu kulifanya ni
kuzua jambo na kulifanya ni dini hali ya kuwa halina asili na dini. Na
maulidi si hivyo!
Katika hujja yao ya pili wanasema: Maulidi hayakusomwa na maswahaba wala
waandamizi wao (taabi'in). Kama kweli
yangelikuwa ni sawa kuyasoma, bila shaka mabwana wakubwa hao wangelikuwa ni wa
mbele kufanya hivyo.
MAJIBU
YETU: Hakuna Mwislamu yoyote anayekataa kuwa maswahaba ni watu watukufu. Wala
hakuna anayekataa kuwa wao ndio kiungo chetu sisi na Bwana Mtume (s.a.w.w.).
Lakini, pamoja na utukufu wote huo, wao walikuwa ni binadamu; hawakuwa ni ma'asumin. Walikiweza kufanya jambo,
wakaswibu (wakapata); kama ambavyo walikiweza kufanya jambo, wakakosea. Na
mifano ya yote mawili hayo ni mingi katika historia yao.
Kwa hivyo, kuwa tu jambo fulani halikufanywa na
maswahaba, haliwi ni hujja sahihi ya
kuwazuilia Waislamu kulifanya jambo hilo. Hujja ya pekee iliyo sahihi ni iwapo
lile ambalo hawakulifanya wao, waliacha kulifanya kwa sababu ndivyo
alivyoamrisha Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.), au waliacha kulifanya
kwa sababu linapingana na maamrisho ya Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.).
Ikiwa walifanya hivyo ndipo jambo hilo litakapokuwa ni hujja; lakini si kwa sababu
ya kuwa halikufanywa na maswahaba, bali ni kwa
sababu tu ya kuwa ndivyo alivyoamrisha Mwenyezi Mungu na Mtume Wake
(s.a.w.w.), au ni kwa sababu tu ya
kuwa linapingana na mafunzo ya Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.) -- na
hivyo ndivyo Kiislamu.
Kwa hivyo si sawa kuyapinga
maulidi kwa sababu tu hayakusomwa na
maswahaba na waandamizi wao. La sawa ni kuyapinga kwa sababu tu yamekatazwa na Mwenyezi Mungu au Mtume Wake
(s.a.w.w.), au yanapingana na maamrisho yao. Na hilo, mpaka hivi sasa,
wapinzani wa maulidi hawajaweza kulithubutisha.
Tunasema hivyo kwa sababu,
mmoja kati ya misingi muhimu ya sharia ya Kiislamu, inayokubaliwa na wanazuoni
wa wanaosoma maulidi na wale wa wanaopinga maulidi, ni kwamba -- tunapokuja
kwenye mambo kama ya maulidi, ujenzi wa msikiti, mavazi, na kadhaalika -- kila kitu ni halali mpaka kithubutishwe kuwa
ni haramu. Kwa hivyo, kwa msingi huu, uharamu wa maulidi haitaki
uthubutishwe na wanaoyasoma, bali inataka uthubutishwe na wanaoyapinga. Wala
wasilithubutishe hilo kwa vichwa vyao (Sura 16:116), bali kwa kutoa ushahidi wa
maneno ya Mwenyezi Mungu au Mtume Wake s.a.w.w. (Sura 4:59). Na hilo pia, mpaka
dakika hii, wapinzani wa maulidi hawajaweza kulifanya.
Mwanzo mwanzo wa kuzuka
madhihabi haya ya kupinga maulidi, wafuasi wake waliyapinga mambo mengi
yaliyozuka katika zama zao. Kati ya mambo hayo ni kuvuta sigara, kupiga simu ya
mdomo (telephone), kujiwekea kashida
mbele ya mtu anaposwali, kumwamkia mtu kwa: "Umeamkaje?", kupana
mikono baada ya swala, kutandika busati misikitini, na hata kuvaa nguo yenye
thamani inayozidi dirhamu 100 (mia)!
Yote hayo waliyapinga kwa
hujja ya kuwa hayakuwako zama za Mtume (s.a.w.w.), na kwamba hayakufanywa na
maswahaba na waandamizi wao! Lakini, baada ya kutambua walikosea wapi, walirudi
nyuma, wakayakubali yote hayo. Kwa maneno mengine, yakawa sio bid'a tena!
Leo, kwa hujja hizo hizo,
waandamizi wao wameanza kusema vibula vivunjwe! Kesho watasema na minara nayo
ivunjwe! Kesho kutwa watasema mimbari za mbao au za mawe, nazo pia ziondolewe,
zirudishwe zile za vigogo vya mtende; hata vya mnazi havitafaa! Baada ya hapo
ni nini kitakachowazuia wasitwambie tuondoe banka (panka) misikitini, turudi
kujipepea kwa nguo zetu kama ilivyokuwa zama za Bwana Mtume (s.a.w.w.)? Au
twende hijja kwa ngamia au farasi badali ya ndege? Au ni lipi litakalowazuia
kutuamrisha kuisoma Qur'ani katika ngozi na mbao, kama ilivyokuwa zama za Bwana
Mtume (s.a.w.w.) na maswahaba, badali ya hii miswahafu mizuri mizuri
tuliyonayo?
Ni matumaini yetu kwamba,
kama ambavyo watangulizi wao walirudi nyuma na kuyakubali yale waliyoyafanya ni
bid'a mwanzo, wao nao watafuata nyayo
zao, wayaone maulidi, na mengine kama maulidi, kuwa sio bid'a iliyokatazwa na Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Alhamdulillaah,
baadhi yao wameanza kuona hivyo na kufanya sherehe za mazazi ya Bwana Mtume
(s.a.w.w.). Lakini badali ya kuyaita maulidi,
huyaita seera!
Hujja
yao ya tatu ni kuwa: kuweka ada ya kusoma maulidi ni kuigiza Wakristo walioweka
siku ya Krismasi; na Mwislamu haruhusiwi kufanya hivyo.
MAJIBU
YETU: Mwislamu hazuiliwi kufanya jambo kwa
sababu tu linafanywa na Mkristo au kafiri yoyote mwengine. Analozuiwa ni
kufanya jambo kama linalofanywa na Mkristo, au kafiri yoyote mwengine,
linapokuwa linakwenda kinyume na mafunzo ya Kiislamu; na hilo sio linapofanywa
na Mkristo au kafiri yoyote tu, bali hata linapofanywa na Mwislamu mwenziwe;
haruhusiwi kulifanya.
Tunaposoma historia, kwa
mfano, tunaona jinsi Bwana Mtume (s.a.w.w.) -- katika Vita vya Handaki --
alivyokubali shauri la Salman Farisi la kuchimba handaki kama walivyokifanya
Wafursi kwao. Na Wafursi, wakati huo, hawakuwa ni Waislamu, bali walikuwa ni
makafiri waliokiabudu moto! Jee, kwa kuwaigiza makafiri hao katika uchimbaji wa
handaki, Bwana Mtume (s.a.w.w.) alikosea?
Hali kadhaalika, tukija
kwenye hijja mathalan, tunaona jinsi mahujaji wanavyokwenda baina ya Swafaa na
Marwa, na jinsi wanavyochinja wanyama mwisho wa hijja yao. Lakini vitendo kama
hivyo, kabla ya Uislamu, vilikuwa vikifanywa na makafiri! Basi kama kuigiza
Wakristo hakuruhusiwi, kwa nini Mwenyezi Mungu na Mtume Wake (s.a.w.w.)
wakatuamrisha kufanya mambo ambayo dhahiri yake ni sawa na kuwaigiza makafiri?
Ukivizingatia vizuri vitendo
hivyo utaona kwamba, japokuwa kwa dhahiri vinafanana na vile vya makafiri, kwa
kweli huwezi kusema kuwa ni sawa na kuwaigiza makafiri. Kwa nini? Kwa sababu
waliyokuwa wakiyafanya makafiri mwahali humo, walikuwa wakiyafanyia masanamu
yao, waliyoyaweka humo. Kwa hivyo yao ilikuwa ni shirk (ushirikina). Lakini tunayoyafanya sisi Waislamu, baada ya
kuondolewa mbali masanamu hayo, huwa tunamfanyia Mwenyezi Mungu Mmoja tu, asiye
na mwenziwe (mshirika). Kwa hivyo yetu ni tawhid
(kumpwekesha Mwenyezi Mungu).
Hali kadhaalika tunapokuja
kwenye Krismasi. Japokuwa Krismasi, kama maulidi, hufanywa kwa kusherehekea
mazazi ya Mitume ya Mwenyezi Mungu (Nabii Muhammad s.a.w.w. na Nabii Isa a.s.),
lakini sherehe mbili hizo -- kama ambavyo kila mtu anajua -- si sawa. Sherehe
zinazofanywa Krismasi ni tafauti kabisa na zinazofanywa maulidini, kama ambavyo
Wakristo wanavyomchukulia Nabii Isa a.s. (Yesu Kristo) ni tafauti kabisa na
vile Waislamu wanavyomchukulia Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Kwa mfano, Waislamu
hawamchukulii Mtume Muhammad (s.a.w.w.) kuwa ni Mungu, wala ni Mtoto wa Mungu,
wala ni Roho Mtakatifu.
Kwa hivyo kuwa tu jambo fulani lilitangulia
kufanywa na makafiri -- wawe ni Wakristo ama ni wengineo -- haiwi ni hujja ya kuwazuilia Waislamu
kulifanya jambo hilo maadamu watayatoa
yote ya ukafiri yaliyokuwamo humo. Na hivyo ndivyo maulidi yalivyo. Zaidi ya
kuwa zote mbili -- Krismasi na maulidi -- ni sherehe za mazazi ya Mitume ya
Mwenyezi Mungu, hakuna jengine linalofanana katika sherehe hizo.
Kama tutashikilia kuwa ni
haramu Waislamu kuwaigiza Wakristo, au makafiri wowote kwa jumla, katika jambo
lolote -- hata kama halipingani na dini yetu -- basi sio wanaosoma maulidi tu,
bali hata wanaoyapinga pia watakuwa makosani. Kwani ni nani kati yao aliyeacha
gari au ndege, akaendelea kupanda punda, farasi au ngamia? Ni nani,
anayejimudu, aliyeacha kutumia umeme (spaki), akaendelea na kuni au mafuta ya
taa? Ni nani anayeradhiwa kujipepea kwa kipepeo au nguo yake, akaacha -- ikiwa
anayo nafasi -- kutumia banka au AC (Air
Conditioner)? Ni nani anayepanda kwa miguu mpaka ghorofa ya 15, au ya 10,
akaacha lifti? Kwa nini hawayaachi yote hayo ili wasiwe wanawaigiza Wakristo au
makafiri wengine, maana yote hayo yameanzishwa na wao.
Kwa hivyo si sawa kuwazuilia Waislamu kusoma
maulidi kwa sababu tu ya kuwa,
kufanya hivyo, ni kuwaigiza Wakristo katika
sherehe zao za Krismasi.
Katika hujja yao ya nne wanasema: Kwenye sherehe za maulidi hufanywa
baadhi ya mambo ambayo ni ya munkar
(yanayochukiza, bali ni haramu kamwe, katika sharia ya Kiislamu).
MAJIBU
YETU: Hiyo si hujja madhubuti. Kwa nini maulidi yote yatupwe kwa sababu tu
ya kufanywa baadhi ya mambo ambayo ni
ya munkar katika sherehe zake? Kwa nini hayaondolewi hayo ya munkar, kama yako,
yakabakishwa yasiyo ya munkar? Kwani tunda likiwa limeoza kidogo hutupwa lote,
au hukatwa pale palipooza likaliwa pale pazuri palipobaki?
Katika hili tuna funzo zuri
kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Yeye aliondoa tawafu ya Al-Kaaba, na Swafaa na
Marwa, kwa sababu mwahali humo mulikuwa na munkar
(masanamu) au aliamrisha yaondolewe hayo masanamu na watu waendelee kutufu?
Tutaona kuwa Mwenyezi Mungu hakutuzuia kufanya jambo zuri lililokuwako (kutufu
na kusa'yi) kwa sababu tu katika
ibada hizo palikuwa na munkar
(masanamu). Alilolifanya ni kuondoa munkar
uliokuwako, akatuacha tuendelee na mazuri yaliyobaki (tawafu).
Kwa hivyo, kama katika
maulidi kuna munkar wowote, la sawa
ni uondolewe munkar huo, na maulidi
yaachwe yaendelee. Si kumtupa jongoo na ung'ongo (ujiti) wake.
Kidokezo
Baada ya kutoa makaratasi
yetu kwa wiki tatu, makundi mawili ya wanaopinga maulidi yamejitokeza. La
kwanza limejita "Ahlu-Tawheed"; na la pili linajita "Wakereketwa
wa Sunna Malindi". Na yote mawili hayakutoa anwani zao!
Ahlu-Tawheed wametoa
makaratasi yenye jina la "Uzushi na Shirk Ndani ya Barzanji na Vitabu
Vyengine vya Maulid". Katika makaratasi hayo, wamenukuu baadhi ya madondoo
ambayo -- kwa maoni yao -- ni shirki. Lakini hawakutueleza vipi kuwako madondoo
hayo katika vitabu hivyo, hata kama yatakuwa ni shirki kweli, yanafanya maulidi
yoyote mengine (yasiyo na hayo
wanayoyaona wao kuwa ni shirki) hayafai kusomwa.
Wakereketwa wa Sunna Malindi,
kwa upande wao, wametoa makaratasi yenye jina la "Chapa ya Kwanza (1):
Majibu ya Abdillah Nassir". Katika makaratasi hayo, ambayo wameahidi
kuendelea nayo, hawajazungumzia maulidi. Walilolifanya ni kunizungumza mimi
binafsi -- kwa ya kweli na ya uwongo! Lakini na wao pia, kama wenzi wao,
hawajatueleza vipi vyovyote vile vitakavyokuwa mimi binafsi -- iwe ni kwa wema
ama kwa uovu -- ni hujja tosha ya kuyafanya maulidi yawe hayafai kusomwa!
Pengine watalieleza hilo katika makala yao yatakayofuatia.
Hata hivyo si nia yangu, kwa
sasa, kuyajibu makaratasi hayo kwa sababu kutatutoa nje ya mfululizo wetu huu.
Nia yangu inshallah ni kuendelea kuzijibu hujja zao zote nilizozidondoa katika
sura ya kwanza humu. Baada ya hapo ndipo nitakapojibu hayo yaliyomo katika
makaratasi yao hayo.
Kwa hivi sasa, napenda
kuwahakikishia wanaosoma maulidi kwamba yote waliyoyataja katika makaratasi yao
mawili hayo tutayajibu kiilimu na kistaarabu, kama ilivyo dasturi yetu, na kama
tulivyofanya mpaka sasa, pamoja na kuonyesha
kwamba hayana mashiko.
Kwa hivyo, tunawaomba wale
walionayo makaratasi hayo wayaweke, wangojee majibu yetu inshallah.
Katika hujja yao ya tano wanasema: Hakuna ushahidi wowote, wa Qur'ani wala
Hadithi za Mtume Muhammad (s.a.w.w.), unaothubutisha usawa wa kuyasoma maulidi,
sikwambii kuyatilia nguvu.
MAJIBU
YETU: Katika majibu yetu ya hujja yao ya pili, tulieleza kwamba -- kwa mujibu
wa msingi mmoja kati ya misingi muhimu ya sharia ya Kiislamu -- anayetakikana
kuthubutisha kuwa maulidi hayafai kusomwa si
anayesema yasomwe; ni anayesema
yasisomwe. Kwa hivyo ushahidi wa Qur'ani na Hadithi unaotakikana si wa kutolewa
na sisi tunaosema ni sawa kusoma maulidi, bali ni wa kutolewa na wao
wanaoyakataza. Jee, wanao ushahidi huo? Kama wanao, twaukaribisha.
Hata hivyo, kama ushahidi
wanaoutaka wapinga maulidi, wa Qur'ani na Hadithi, ni unaosema kwa kutasua (nassun qat'iyy / categorically),
"Enyi mlioamini! Someni maulidi"; basi ushahidi huo hakuna. Lakini
tunauliza, kwa sharia ya Kiislamu, ni lazima jambo litasuliwe katika Qur'ani au
Hadithi ya Bwana Mtume (s.a.w.w.) ndipo liruhusiwe kufanywa? Jee, hakuna mambo
ambayo Waislamu -- wakiwamo wanaopinga maulidi -- huyafanya pamoja na kuwa hawana ushahidi wa
Qur'ani wala Hadithi zilizoyataja mambo hayo?
Kwa mfano, ni nani kati ya
wanaopinga maulidi anayeweza kututolea ushahidi wa kutasua -- wa Qur'ani au
Hadithi ya Mtume Muhammad (s.a.w.w.) -- wa Waislamu kuruhusiwa kujenga vyuo (colleges) na vyuo vikuu? Au kutoa
digrii? Au kujenga hospitali na zahanati? Au kujenga nyumba za mayatima (orphanages)? Au kuunda vyama vya
ushirika? Au kuweka mashindano ya kusoma Qur'ani na kuyatolea zawadi, na
mengine mengi kama hayo? Jibu ni: hakuna!
Kama uko, tunaomba tutolewe. Jee, kwa kuwa hauko, ndio watakuwa Waislamu wote -- wakiwamo wanaosoma maulidi --
wanakosea kwa kuyafanya mambo hayo kwa
sababu tu hakuna aya au Hadithi inayoyataja? Kama ni hivyo, basi kwa nini
wao wanayafanya? Kama sio hivyo, basi kwa nini wanatukataza kuyasoma maulidi
kwa sababu hiyo hiyo?
Katika Qur'ani na Hadithi
kuna mambo ambayo uhalali wake umetasuliwa (specified).
Mfano wa hayo ni kumpwekesha Mwenyezi Mungu, kuswali, kufunga (saumu), kutoa
zaka, kuhiji, kuowa, kufanya biashara, kufanya uadilifu, na kadhaalika. Kuna na
ambayo uharamu wake pia umetasuliwa; kama kumshirikisha Mwenyezi Mungu, kuzini,
kula riba, kuiba, kudhulumu, kusema uwongo, kusengenya, na kadhaalika. Yote
hayo ni mambo ambayo ushahidi wake -- wa kuyatasua khaswa -- unaweza kutolewa
katika Qur'ani na / au Hadithi za Bwana Mtume (s.a.w.w.).
Kuna na ambayo
hayakutasuliwa isipokuwa yametajwa kwa jumla (generally) tu. Hayo, kinyume na yale yaliyotasuliwa tuliyoyataja
hapo juu, yana uwanja mkubwa wa jinsi ya kuyatekeleza maadamu hayatachanganywa na ya haramu. Hebu tuangalie mifano miwili
mitatu:
1.
Mayatima: Tunaposoma
Qur'ani na / au Hadithi, tunaona kwamba tunahimizwa kwa jumla tuwatizame,
tusiwatupe; tuwahurumie, tusiwatese. Vipi? Hilo hatukutajiwa tafsili zake
isipokuwa tumeachiwa sisi, bora tu
tusitie la haramu. Kwa sababu hii ndio ukaona hakuna aliyezuia kujengwa
nyumba za mayatima (orphanages)
japokuwa hazikutajwa kwa jina katika Qur'ani wala Hadithi za Mtume Muhammad
(s.a.w.w.)!
2.
Ilimu: Tunaposoma
Qur'ani na / au Hadithi, tunaona jinsi tunavyohimizwa, bali kufaradhiwa, kusoma
na kuitafuta ilimu popote ilipo. Hatukupawa tafsili ya namna ya kulitekeleza
hilo. Kwa hivyo, maadamu hatulitii la
haramu, tuko huru kusoma kwa ubao, kitabu, tepu, video, redio, runinga,
mtandao, na kadhaalika; kama ambavyo tuko huru kusoma madrasa, nyumbani,
msikitini, chuoni (college) au kwenye
vyuo vikuu; na kama ambavyo tuko huru kukaa majamvini, vitini au madeskini.
Hakuna hata mmoja wa mashekhe wa wanaopinga maulidi anayewazuia watu kuyafanya
hayo, na tuliyoyataja hapo juu yanayohusu mayatima, kwa sababu tu hayakutajwa kwa jina katika Qur'ani wala Hadithi za
Mtume Muhammad (s.a.w.w.)!
Basi kwa nini kuyapinga maulidi?
Inshallah, katika sura
inayofuatia, tutazidondoa aya za Qur'ani na Hadithi za Bwana Mtume (s.a.w.w.)
ambazo, japokuwa hazikutaja maulidi kwa jina, zinaunga kwa jumla yale yanayofanywa na yanayofanyika maulidini.
3
MAULIDI KATIKA
QUR'ANI NA HADITHI
Japokuwa -- kama
tulivyoeleza katika sura iliyopita -- maulidi hayakutajwa kwa jina katika
Qur'ani wala Hadithi, lakini yamekusanya mengi yaliyoamrishwa au
yaliyopendekezwa na Qur'ani na / au Hadithi. Hapa chini tutayataja baadhi yake
tu:
1.
Kusoma
na kusikiliza Qur'ani: Tunaposoma
Qur'ani (k.m. Sura 73:4 na 20), tunaona jinsi Mwenyezi Mungu anavyotuamrisha
tuisome. Na tunapokuja kwenye Hadithi zake, tunaelezwa kwamba Bwana Mtume
(s.a.w.w.) alikuwa akipenda sana mtu amsomee yeye Qur'ani, na yeye akisikiliza.
Jee, pale
tunapoyafungua maulidi yetu kwa mmoja wetu kuisoma Qur'ani, na wengine tukawa
tunamsikiliza, huwa -- kama hatukufanya la sunna
-- tumefanya lipi la bid'a?
2.
Kumswalia
Mtume (s.a.w.w.): Katika Qur'ani Tukufu (Sura 33:56), Mwenyezi Mungu
anatuamrisha tumswalie Mtume Wake (s.a.w.w.) baada ya kutwambia kuwa Yeye na
Malaika Wake hufanya hivyo pia. Isitoshe! Na kila Ijumaa, khatibu hutukumbusha
juu ya mimbari, kwa kututajia Hadithi ya Mtume (s.a.w.w.), kuwa yoyote
atakayemswalia yeye mara moja, Mwenyezi Mungu atamswalia (atamrehemu) mtu huyo
mara kumi!
Jee, katika kikao
kimoja tu cha maulidi, waliohudhuria humswalia Mtume (s.a.w.w.) mara ngapi? Zidisha
mara hizo kwa kumi ujue Mwenyezi Mungu hukurehemu wewe mara ngapi katika kikao
hicho. Jee, ni lipi hapo -- kama halitakuwa sunna
-- lililo bid'a?
3.
Kumhishimu
na kumtukuza Bwana Mtume (s.a.w.w.): Katika Qur'ani Tukufu (Sura
7:157), Mwenyezi Mungu anawasifu, na kuweta "wenye kufaulu", wale
ambao humtukuza na kumhishimu Mtume Wake (s.a.w.w.), wakamsaidia na kuyafuata
yale aliyoyaleta. Lakini tutawezaje kuyafanya hayo kama mtu mwenyewe hatumjui
vilivyo?
Waswahili husema:
"Jambo usilolijua ni usiku wa kiza"; na "asiyekujua
hakuthamini". Kwa hivyo, bila ya kumjua Mtume (s.a.w.w.) vilivyo --
historia yake, sifa zake, cheo chake, utukufu wake, na kadhaalika -- vipi
tutaweza kumthamini na kumtukuza? Ndipo wanazuoni, kwa kuwa si kila mtu aweza
kusoma vitabu, wakabuni maulidi ili yawe ni chombo cha kumjulisha Bwana Mtume
(s.a.w.w.) apate kuhishimiwa na kutukuzwa. Hivyo katika maulidi, watu hupata
fursa ya kuelezwa yote ya Mtume (s.a.w.w.). Na kwa kuyajua hayo, watu humpenda;
na kama ilivyo dasturi ya kila apendaye kumfuata yule anayempenda, watu
humfuata.
Jee, kama maulidi
yanasaidia watu kumjua Mtume (s.a.w.w.), kumkumbuka na kumpenda, ni lipi hapo
la bid'a?
4.
Kumsifu
Bwana Mtume (s.a.w.w.): Tunaposoma maisha yake, tunaambiwa kwamba,
miongoni mwa maswahaba, walikuwako waliotunga mashairi ya kumsifu Bwana Mtume
(s.a.w.w.) ambayo walikwenda nayo mbele zake na kumsomea. Bwana Mtume
(s.a.w.w.) hakuwafukuza watu hao wala hakuwakataza, bali aliwasikiliza na
kuyafurahia yote waliyomsomea. Kwa kitendo hicho kwa hivyo, Bwana Mtume
(s.a.w.w.) alitufungulia mlango wa kumsifu. Tafauti ya pekee iliyoko baina ya
maswahaba na sisi ni kwamba wao walimsifu machoni mwake, hali sisi tunamsifu
akiwa hayuko na sisi kimwili. Sasa, kwa kitendo hiki, tunafanya jambo gani
ambalo halikufanywa na maswahaba na kukubaliwa na mwenyewe Bwana Mtume
(s.a.w.w.)?
Kama kufanya
hivyo ni bid'a, basi sunna ni ipi?
5.
Kutoleana
waadhi: Katika Qur'ani Tukufu (Sura 16:125) Mwenyezi Mungu anatuamrisha
tulinganiane kwa hikima na mawaidha mema. Na vivyo hivyo ndivyo Bwana Mtume
(s.a.w.w.) anavyotuhimiza katika Hadithi zake nyingi.
Jee, maulidini
hatutoleani mawaidha na kulinganiana mema? Hayo nayo kama ni bid'a, sunna ni ipi?
6.
Kumpenda
Mtume (s.a.w.w.): Hadithi zake (s.a.w.w.) zatuhimiza tumpende, bali
zinatueleza waziwazi kwamba hatuwi ni waumini mpaka tumpende yeye kuliko nafsi
zetu, kuliko mali yetu na ahli zetu, bali kuliko watu wote.
Jee sifa zote
zile anazosifiwa Mtume (s.a.w.w.) maulidini, furaha zote na nderemo
zinazoonyeshwa maulidini, haziwi ni ushahidi wa mapenzi yetu kwa Mtume Muhammad
(s.a.w.w.)? Mambo kama hayo hufanyiwa asiyependwa?
Kama kuonyesha
mapenzi yetu kwa Mtume wetu ni bid'a,
sunna ni ipi?
7.
Kujumuika
na kushikamana: Qur'ani Tukufu (Sura 3:103) inatuhimiza tushikamane
na tusifarikiane. Na Mtume naye (s.a.w.w.) anatuhakikishia, katika Hadithi
zake, kwamba popote ambapo tutajumuika kwa kheri -- na sidhani kuwa maulidi ni
shari -- basi Malaika watatuzunguka, rehema za Mwenyezi Mungu zitufinike, na
utulivu wa nyoyo utushukie.
Jee, tunapokusanyika
maulidini, hatuyaoni hayo? Ule umoja na mshikamano unaopatikana maulidini, wa
wafuasi wa madhihabi mbalimbali kusahau hitilafu zao na kuwa kitu kimoja, ni
rehema ndogo?
8.
Kutembeleana
na kukirimiana: Bwana Mtume (s.a.w.w.), katika Hadithi zake, ametunasihi
tuwe tukifanyiana hayo; na hayo huyapata kwa ukubwa siku za maulidi. Waislamu
wa mtaa mmoja, au mji mmoja, au hata nchi moja -- kwa kuhudhuria sherehe za
maulidi ya wenzi wao -- hupata fursa ya kutembeleana na kukirimiana. Kwa njia
hii hujuana hali, wakasaidiana na kupanana (peana) moyo. Hilo huleta mapenzi na
mshikamano baina yao. Na iwapo pale pasomwapo maulidi Waislamu ni wachache,
kutembelewa kwao na ndugu zao wanaotoka sehemu nyengine huwatia moyo, na pia
huwafanya wahishimiwe na wale jirani zao wasio Waislamu.
Katika hayo, ni
lipi la bid'a, kama hapana la sunna?
9.
Kutangaza
Uislamu na kusilimisha wengine: Katika Qur'ani Tukufu (Sura
5:67) Mwenyezi Mungu anamwamrisha Mtume Wake (s.a.w.w.) awafikishie watu Ujumbe
aliompa. Na katika khutba yake ya mwisho, Bwana Mtume (s.a.w.w.) alituamrisha
sisi wafuasi wake tuufikishe Ujumbe huo kwa yule ambaye haujamfikia. Na hilo
limepatikana -- na linaendelea kupatikana -- maulidini kwa ushahidi wa rikodi
ya wengi waliosilimu baada ya kuhudhuria maulidini na kusikiliza kaswida na
khutba zinazotolewa huko.
Jee, bid'a ni ipi hapo?
10.
Kumkumbuka Mtume Muhammad
(s.a.w.w.): Qur'ani Tukufu (Sura 41:34) inatwambia kuwa jema na
ovu si sawa. Ukitaka kuliondoa ovu, liondoe kwa jema ndipo ovu litakapofutika.
Na Mtume (s.a.w.w.) naye ametwambia vivyo hivyo. Hali kadhaalika wazee nao
wanatwambia kwamba tukitaka kumpokonya mtoto wembe ili asijikate, tusimwache
mikono mitupu maana ataurudia. Badali yake tumpe kitu chengine kisicho na
madhara (k.m mpira) ashike. Kwa njia hii tutamwokoa na madhara.
Katika zama kama
hizi zetu ambapo Waislamu kwa jumla, na watoto wao khaswa, wanayajua zaidi ya
viongozi wasio Waislamu, bali hata ya walio maadui wa Uislamu, katika nyanja
mbalimbali, na husherehekea mazazi yao -- ni lipi bora? Tuwaache waendelee
vivyo hivyo? Au tuwaambie waache kufanya hivyo bila ya kuwawekea badali yake?
Au tuwawekee badali iliyo nzuri (ya sherehe za mazazi ya Mtume (s.a.w.w.) na
viongozi wengine wa Kiislamu) ili tuwaachishe hayo waliyoyashika? Jawabu hapo
ninakuachia wewe, ndugu Mwislamu.
Mpaka hapa
tumemaliza majibu yetu ya hujja zinazotolewa na wanaopinga maulidi; na
kuwafikiwa ni kwa Mwenyezi Mungu. Sasa, kama tulivyoahidi katika sura ya pili
humu, tutayajibu ya Ahlu-Tawheed waliyoyasema katika makaratasi yao,
"Uzushi na Shirk Ndani ya Barzanji na Vitabu Vyengine vya Maulidi".
4
WALIYODAI "AHLU
- TAWHEED"
Katika makaratasi yao hayo,
ndugu zetu hao wamenukuu baadhi ya maneno yaliyomo katika Barzanji na Burdah
(vitabu viwili vinavyoeleza sifa za Mtume Muhammad s.a.w.w.) na kujaribu, kadri ya ujuzi na uweza wao,
kuonyesha kwamba kusema maneno hayo ni shirki.
Lakini, kabla ya kutoa majibu yetu, tuanze kwa kuyanukuu maneno yenyewe. Nayo
ni mane yaliyotolewa katika Barzanji,
na mawili katika Burdah.
Katika Barzanji wameyatoa yanayofuata:
1.
"Na
kama si yeye (Mtume s.a.w.) asingekuwa Alkhalilu (Ibrahim) na Adam. Na Musa
(asingekuwepo) na Issa, bali hata Mulku Suleimani (usingekuwepo)."
2.
"Ilisemekana
alipotaka Mwenyezi Mungu, Mwenye Ezzi na Alietukuka, kumdhihirisha Mbora wa
viumbe vyake, Muhammad, Rehma na Amani za Mwenyezi Mungu zimfikie. Akamuamrisha
Jibril achukue Udongo wake (wa
kumuumbia nao) kwenye mahali pa kaburi
lake karimu".
3.
"Alikuwa
Mtume akikua mchana mmoja kama anavyokua mtoto mwengine kwa mwezi mzima kwa
ajili ya kushughulikiwa na Mwenyezi Mungu".
4.
"Akamwonyesha
kwa haya macho ya kichwani (ya usoni) aliyomwonyesha. Nayo ni yeye mwenyewe
Mwenyezi Mungu."
Na katika Burdah wameyatoa yanayofuata:
5.
"Kama
si yeye (Mtume s.a.w.w.) usingetoka ulimwengu (usingeumbwa)."
6.
"Haukupata
kunipiga vita Ulimwengu, nikataka nusra kwa Mtume, ila huipata tu."
Hayo ndiyo maneno
waliyoyanukuu ndugu zetu wa Ahlu-Tawheed kuthubutisha kwamba, katika vitabu
hivyo, muna shirki. Wakayaandamiza,
pia, na hujja zao za kuyabatilisha hayo.
MAJIBU
YETU : Kwanza; tukumbuke
kwamba tunalojadiliana si kuwa, katika vitabu vya maulidi, muna shirki au
hamuna; la! Tunalojadiliana ni: maulidi ni bid'a
au si bid'a; ni haramu au si haramu?
Sisi, kwa upande wetu, katika makala yetu yaliyopita, kwa kujibu hujja
zinazotolewa na wapinga maulidi, tumeonyesha kwamba maulidi si bid'a wala si haramu. Kwa hivyo sasa
tunalolingojea kwa wapinga maulidi, wakiwamo Ahlu-Tawheed, ni majibu yao ya
hujja tulizozitoa -- kiilimu na kimantiki, kama tulivyofanya sisi.
Pili; hata kama
itakubaliwa kuwa hayo maneno waliyoyanukuu ni shirki -- na hilo hatulikubali kwa hujja tunayoitoa hapa chini --
hilo haliwi ni hujja ya kuharamishia maulidi au kuyasusia. La sawa kufanywa
hapo ni kuyatoa hayo yanayoonekana ni shirki
na / au kuyasahihisha; si kuzuia watu kuyasoma. Hivyo, kwa mfano, ndivyo
alivyofanya marehemu Sheikh Abdulla Swaleh Farsy katika Wasila wa Nabahani. Yeye alipoona kwamba "Lawlaahu maa kunnaa walaa baaqiina" si sawa, hakuzuia
watu, wala yeye hakuacha kuusoma. Alichofanya ni kukibadilisha kipande hicho na
kukisoma alivyoona yeye ni sawa: "Lawlal
ilaahu
" Hakuutupa wasila wote, wala hakuzuia watu kuusoma kwa sababu tu muna kipande cha maneno
asiyoyakubali.
Tatu; tunapoyataamali
yote madondoo sita waliyoyanukuu Ahlu-Tawheed, ambayo nasi tumeyanukuu hapo
juu, hakuna hata moja liwezalo
kusemwa ni shirki kwa hujja ifuatayo:
Shirki ni kusema /
kuamini kuwa Mwenyezi Mungu ana mwenziwe, au ana aliye sawa naye, au ana
mfanowe, au ana anayetokana naye. Pia kusema / kuamini kuwa yuko muumbaji
mwengine wa ulimwengu asiyekuwa Yeye, au muendeshaji (mudabbir) ulimwengu asiyekuwa Yeye, au mwenye haki ya kuweka
sharia asiyekuwa Yeye, au anayelazimika kutwiiwa asiyekuwa Yeye, au kuna
mtawala (haakim) asiyekuwa Yeye, au
kuna mwenye haki ya kuabudiwa asiyekuwa Yeye.
Kwa kuwa hakuna hata moja,
ya madondoo sita waliyoyanukuu Ahlu-Tawheed kutoka katika Barzanji na Burdah,
linalosema hivyo, vipi basi mutakuwa muna shirki? Kama lipo, tunaomba watwambie
ni dondoo lipi kati ya hayo waliyotutajia, na linaingia wapi katika hiyo
taarifa ya shirki tuliyoieleza sisi
hapo juu. Kama taarifa yetu imeacha mengine yaliyo shirki, basi tunaomba tukumbushwe.
Kwa hakika
haikuwa nia yangu kuingia katika masiala ya shirki
kwa sababu hilo li nje ya maudhui yetu. Maudhui yetu ni maulidi ni bid'a au si bid'a; ni haramu au si haramu. Na hilo tushalijibu vya kutosha.
Lakini, kwa kuwa wafuasi wa madhihabi ya wapinga maulidi hupenda kukibandika
jina la bid'a au shirki kila wanachokipinga
wao, nimeona japo kwa ufupi niwaeleze wasomaji wangu jamaa zetu hao hupotelea
wapi katika kuielewa shirki ni nini,
na si nini!
5
Kwa taarifa tuliyoitoa (na
tunaomba tuelezwe kama tumeacha kitu katika taarifa hiyo), kati ya madondoo
sita yaliyonukuliwa na ndugu zetu hao, matano yametushinda kuelewa vipi yaweza
yakawa ni shirki. Kwa hivyo
hatutashughulika nayo kwa leo mpaka hapo tutakapofafanuliwa inshallah.
Tutakaloshughulika nalo leo ni moja tu lililobaki ambalo, kwa hujja walizozitoa
kulipingia, tumeweza kulifahamu lililowafikirisha wao kuwa ni shirki. Nalo ni
lile la Buswiri kusema katika Burdah:
"Haukupata kunipiga vita Ulimwengu nikataka
nusra kwa Mtume ila huipata tu."
Kulikosoa hilo, Ahlu-Tawheed
wameitaja Sura 3:126 ambayo wameifasiri hivi: "Na msaada hautoki (kwa mwengine yoyote) isipokuwa kwa
Mwenyezi Mungu, Mwenye Nguvu na Mwenye hikima". Kwa kuitaja aya hii, kwa
hivyo, tumeelewa kwamba ndugu zetu hao wameyaelewa maneno ya Buswiri hivi:
"Kwa kuwa msaada (nasr) hautoki
isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu, kuuomba kwa mtu mwengine yoyote asiyekuwa
Mwenyezi Mungu, hata awe ni Mtume (s.a.w.w.), ni sawa na kumfanya mtu huyo ni
Mwenyezi Mungu! Na kufanya hivyo ni shirki;
kwa hivyo katika Burdah muna shirki!"
MAJIBU
YETU : Kwanza; katika tafsiri yao
ya hiyo Sura 3:126 wameongeza maneno katika pinde, tuliyoyachapa kwa italiki, ambayo hayamo katika aya
hiyo, wala hayaipunguzii maana lau yasingeongezwa.
Pili; kama maana ya
"msaada hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu" ni kwamba haturuhusiwi
kutafuta msaada kwa asiyekuwa Yeye, au asiyekuwa Yeye hana msaada wa kuutoa,
basi ilikuwaje watu wa Madina wakaitwa answaar
(wasaidizi)? Walimsaidia nani? Huyo aliyesaidiwa, aliukosa msaada wa Mwenyezi
Mungu hata wakaingia kati wao? Na sisi Waislamu, pamoja na Mtume wetu
(s.a.w.w.), tunamshirikisha Mwenyezi Mungu kwa kuwaita answaar watu wa Madina?
Tunaposoma Sura 3:81 tunaona
jinsi Mwenyezi Mungu alivyochukua ahadi kwa Mitume Yake kwamba itamsaidia /
itamnusuru (latansurunnahuu) Mtume
Muhammad (s.a.w.w.). Jee, kama "msaada hautoki (kwa mwengine yoyote)
isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu," ilikuwaje hapo, Yeye Mwenyewe, akautaka kwa asiyekuwa Yeye? Jee, kwa kitendo hicho,
Mwenyezi Mungu -- Mwenyezi Mungu apishe mbali! -- alikusudia kuifanya Mitume
Yake ni miungu?
Katika Sura 7:157, kati ya
sifa za waumini ambao "ndio wenye kufaulu", ni wale ambao wamemsaidia
/ wamemnusuru (wanaswaruuhu) Mtume
Muhammad (s.a.w.w.). Jee, kama "msaada hautoki (kwa mwengine yoyote)
isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu", kwa nini akawaagiza waumini wamsaidie Mtume Wake? Kwa sifa hiyo
hapo, ndio Mwenyezi Mungu amewafanya waumini kuwa ni miungu? Mwenyezi Mungu --
Mwenyezi Mungu apishe mbali -- hapo amefanya shirki?
Hali kadhaalika; tunaposoma
Sura 28:15 tunaona jinsi jamaa yake Nabii Musa (a.s) "alivyomuomba
msaada" (fastaghaathahuu) juu ya
adui yake. Jee, Nabii Musa (a.s) alimrukia jamaa yake huyo, na kumwambia
asilete shirki kwa kumuomba yeye
msaada badali ya Mwenyezi Mungu? La! Alimsaidia; na siku ya pili (Sura 28:18)
yule aliyeomba msaada jana (istanswarahuu) akamuomba tena! Jee,
kama "msaada hautoki (kwa mwengine yoyote) isipokuwa kwa Mwenyezi
Mungu", kwa kutoa msaada wake huo, Nabii Musa (a.s) alikuwa Mwenyezi
Mungu, au hakujua kuwa "msaada hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi Mungu"?
Kwa kutaja mifano hiyo hapo
juu, sisi tusomao maulidi hatukusudii kukanusha yaliyomo katika aya iliyotajwa
na wapinga maulidi, kuwa "msaada hautoki isipokuwa kwa Mwenyezi
Mungu"; hasha! Tunalokusudia ni kufahamisha kwamba: maneno yanapofanana, si lazima na maana yafanane (yawe mamoja). Kwa hivyo,
msaada ambao Buswiri aliuomba kwa Bwana Mtume (s.a.w.w.), na sisi huukariri
tunapoisoma hiyo Burdah, sio msaada
ambao huombwa kwa Mwenyezi Mungu. Ni majina tu kufanana -- kama ulivyokuwa ule
ambao Mwenyezi Mungu alimtakia Mtume Wake kwa Mitume mengine, na aliotutaka
sisi waumini tumpatie Mtume Muhammad (s.a.w.w.), na ambao watu wa Madina
walimpatia Bwana Mtume (s.a.w.w.) hata wakaitwa answaar (wasaidizi wake), na ule ambao Nabii Musa (a.s) alimpatia
jamaa yake.
Msaada wa Mwenyezi Mungu
unatokana na Yeye Mwenyewe; hakupawa na
yoyote uweza huo wa kusaidia. Lakini wa asiyekuwa Mwenyezi Mungu, akiwamo
Mtume Muhammad (s.a.w.w.), si wake
mwenyewe; ni wa kupawa (kuwezeshwa na Mwenyezi Mungu). Na hapo ndipo palipo
na tafauti baina ya shirki ni nini,
na si nini.
Ukiamini kwamba Mtume
(s.a.w.w.) -- yeye mwenyewe, bila ya
kupawa uweza huo na Mwenyezi Mungu -- aweza kusaidia; hiyo ni shirki. Na hilo silo alilokuwa akiliamini Buswiri, wala
silo tunaloliamini sisi tusomao maulidi. Lakini ukiamini kuwa msaada uwezao
kupawa na Mtume (s.a.w.w.) ni ule aliowezeshwa yeye na Mwenyezi Mungu; hiyo si shirki. Na hilo ndilo
alilokusudia Buswiri katika Burdah,
na ndilo tunaloliamini sisi tunaosoma maulidi. Kwa hivyo kubwa ambalo wapinga
maulidi waweza kutwambia sisi ni kuwa Mtume (s.a.w.w.) hakuwa / hana uweza huo;
kwa hivyo ni kazi bure kumuomba hivyo -- jambo ambalo hatulikubali kwa sababu
ya hujja tulizonazo. Lakini hawawezi kutwambia ni shirki, kwa mifano mingi tuwezayo kuwatolea katika Qur'ani Tukufu.
Wapinga
maulidi hupotea wapi
Wapinga maulidi, wanaposoma
vitabu vya maulidi, wakaona kuwa Mtume (s.a.w.w.) amesifiwa kwa neno
alilosifiwa Mwenyezi Mungu, au kitendo chake kimetajwa kwa neno ambalo, kwa
kawaida, hunasibishwa nalo Mwenyezi Mungu -- wanapoona hayo, moja kwa moja
husema ni shirki, kwa sababu hivyo
ndivyo wanavyoielewa wao shirki, na
hali hivyo sivyo.
Neno lililotumiwa kumsifia
Mwenyezi Mungu, linapotumiwa kumsifia Mtume (s.a.w.w.), halimfanyi Mtume kuwa
ni Mungu (kwa hivyo si shirki) kama
ambavyo, vile vile, neno lililotumiwa kuelezea kitendo cha Mtume (s.a.w.w.),
halimfanyi Mtume kuwa ni Mungu. Kwa kutolielewa hili ndipo wapinga maulidi --
wao na viongozi wao -- walipokosea na kudai kuwa vitabu vya maulidi vina shirki!
Kuthubutisha kosa lao hilo,
hapa chini tunayataja mifano michache tu (sio
yote) kutoka katika Qur'ani Tukufu:
1.
Tunaposoma Sura 2:143, tunamuona Mwenyezi
Mungu anavyojisifu kuwa Yeye ni rauufun
(Mpole) na rahiimun (Mwenye
kurehemu). Na tunaposoma Sura 9:128, tunamuona Mwenyezi Mungu, Yeye Mwenyewe, anamsifu Mtume Wake
(s.a.w.w.) kwa sifa zizo hizo za rauufun rahiimun! Jee, kwa kufanana
matamko ya sifa hizo, Mwenyezi Mungu alikusudia kumfanya Mtume Wake ni Mungu kama Yeye? Jee, sisi tunapomsifu Mtume kwa sifa hizo, huwa tumefanya
shirki kwa sababu tu matamko
yaliyotumiwa yanafanana?
Jawabu ni: La! Isipokuwa kama tutaamini
kuwa uraufu na urahimu wa Mtume (s.a.w.w.) ni sawa na ule wa Mwenyezi Mungu! Na
hilo, sisi watu wa maulidi, hatulisemi wala hatuliamini. Tunaloliamini sisi ni
kwamba uraufu na urahimu wa Mwenyezi Mungu ni Wake Mwenyewe kwa asili (bil aswaala / independently); wa Mtume
(s.a.w.w.) ni wa kupawa na Yeye, Mola
wake. Kama kumsifu Mtume kwa sifa hizo ni shirki
kwa sababu tu zimefanana na za Mwenyezi Mungu, basi na wapinga maulidi nao
pia ni mushrikina kwa sababu
hatuamini kwamba wanapoifikia aya hiyo (Sura 9:128), kama Waislamu, huiruka
wakaacha kuisoma, au huibadilisha maneno yake.
2.
Tunaposoma Sura 16:70, tunaona kwamba
Mwenyezi Mungu ndiye aliyetuumba na ndiye anayetufisha / anayetuuwa (yatawaffaakum); na tunapoisoma Sura
32:11, tunaona kwamba atakayetufisha (yatawaffaakum)
sisi ni "malaika wa mauti". Sasa tushike lipi hapo, maana neno
lililotumiwa kuelezea kitendo hicho cha kutoa roho ni lilo hilo moja: yatawaffaakum? Afishaye ni Mwenyezi
Mungu, au ni huyo malaika?
Tukisema ni
Mwenyezi Mungu peke Yake, tutakuwa tunaikanusha Qur'ani kwa sababu Qur'ani yiyo
hiyo imetwambia kuwa na malaika huyo naye huifanya kazi hiyo. Na tukisema ni
malaika peke yake, tutakuwa vile vile tunaikanusha Qur'ani kwa sababu Qur'ani
yiyo hiyo imetwambia kuwa Mwenyezi Mungu naye huifanya kazi hiyo. Sasa ni nani
basi? Ni wote wawili?
Jawabu ni: Ndiyo! Ni wote wawili;
lakini pana tafauti. Japokuwa maneno (yatawaffaakum)
yaliyotumiwa yanafanana, tawaffaa ya
Mwenyezi Mungu si sawa na ya malaika. Ya Mwenyezi Mungu ni ya uweza Wake
alionao Yeye Mwenyewe kwa asili. Ile ya malaika si hivyo. Yake ni ya "kuwakilishwa" (alladhii wukkila bikum) na Mwenyezi Mungu, kama aya yake (Sura
32:11) inavyofafanua. Kwa hivyo, ukiamini hivyo; hiyo si shirki. Lakini ukiamini kuwa uweza wa kufisha alionao malaika ni sawa na ule alionao Mwenyezi Mungu;
hiyo, bila shaka yoyote, itakuwa ni shirki.
Na ni Mwislamu gani anayeamini hivyo?
3.
Tunaposoma Sura 22:6, tunaona kwamba Mwenyezi
Mungu ndiye anayefufua (yuhyii) wafu;
na tunaposoma Sura 3:49, tunamuona Nabii Isa (a.s), mtume wa Mwenyezi Mungu,
anasema kuwa yeye naye anafufua (uhyii)
wafu! Sasa basi, kwa kusema hivyo, Nabii Isa hapo alijifanya ni Mungu? Au sisi,
tunapoisoma aya hiyo katika Qur'ani, huwa tunamshirikisha Nabii Isa na Mwenyezi
Mungu?
Jawabu ni: Ndiyo, kama tutaamini kuwa
Nabii Isa (a.s) alikuwa nao uweza huo yeye
mwenyewe. Lakini kama tutaamini, kama alivyoeleza yeye mwenyewe Nabii Isa
katika aya yiyo hiyo, kuwa aliweza kufanya hilo "kwa idhini ya Mwenyezi
Mungu" (bi idhnillaahi), hapo
hatutakuwa tumemshirkisha na Mwenyezi Mungu japokuwa
neno lililotumiwa kwa wote wawili -- yuhyii
na uhyii -- ni lilo hilo moja.
4.
Tunaposoma Sura 25:2, tunaona kuwa Mwenyezi
Mungu ndiye aliyeumba kila kitu. Sisi binadamu (Sura 32:7) alituumba (khalaqa) kwa udongo, kisha (Sura 32:9)
akatuvivia / akatupulizia (nafakha fiihi)
roho Yake, tukawa. Hali kadhaalika Nabii Isa (a.s); kwa mujibu wa Sura 3:49
anasema, "
Ninawaumbia nyinyi (akhluqu lakum) kwa udongo, kama sura ya
ndege, kisha nampuliza (anfukhu fiihi),
mara anakuwa ndege
"
Jee, Nabii Isa
hapo alikuwa Mungu? Au sisi Waislamu -- tunaosoma maulidi na tunaoyapinga --
tunapoisoma aya hiyo, pamoja na kuwa ametumia maneno yale yale (akhluqu lakum na anfukhu fiihi) yaliyotumiwa na Mwenyezi Mungu, humfikiria Nabii Isa
(a.s) kuwa ni Mungu? Hasha! Kwa nini? Kwa sababu, katika aya hiyo hiyo, amesema
kuwa ameweza kulifanya hilo "kwa idhini ya Mwenyezi Mungu" (bi idhnillaahi); si kwa uweza wake yeye
mwenyewe.
Kwa mifano mine hiyo
tuliyoitaja hapo juu, tumeona kwamba linalozingatiwa katika kuhukumu jambo kuwa
ni shirki au la, si maneno yanayotumiliwa Mwenyezi Mungu na Mtume Wake kufanana;
hasha! Linalozingatiwa ni hilo tunalomnasibisha nalo Mtume, au kiumbe yoyote,
linatokana na uweza alionao yeye mwenyewe
kwa asili au aliopawa na Mwenyezi
Mungu? Tukiamini hilo la kwanza,, itakuwa ni shirki. Tukiamini hilo la pili, itakuwa si shirki. Na hili ndilo aliloliamini Buswiri na wanaoyakubali ya Burdah: kwamba uweza alionao Mtume
(s.a.w.w.) wa kutoa msaada ni wa kupawa
na Mwenyezi Mungu; si wake mwenyewe kwa asili.
6
Sasa tuyajibu
yaliyochapishwa na "Wakereketwa wa Sunnah Malindi" kwa jina la
"Majibu ya Abdillah Nassir". Makala tunayoyajibu humu ni yale ya
"chapa ya kwanza". Sijui kama, baada ya hiyo, wametoa chapa nyengine
kwa sababu mimi sijaziona.
Katika makala yao hayo,
walianza kwa kusema: "Tunashindwa kukuelewa tukueke wapi
"
MAJIBU:
Tunalolijadili ni maulidi ni bid'a au ni haramu, au
si bid'a wala si haramu? Sijadiliwi mimi niwekwe wapi. Kwani
"wakereketwa" wakishajua pa kuniweka, ndio watajua hukumu ya maulidi
ni ipi; ni bid'a / haramu au si bid'a / haramu?
Kisha wakasema: "
Sifa
za mwanzo ilikuwa sunna, ukawa mstari wa mbele kwa kuamrisha, kufanya, kukataza
lolote la uzushi au haliambatani na sheria ya Mwenyezi Mungu na Sunna ya Mtume
S.A.W."
MAJIBU:
Hilo ni kweli; na mpaka hii leo msimamo wangu
ungali huo huo. Tafauti iliyoko hapa, baina ya "wakereketwa" na mimi,
ni kwamba baadhi ya mambo wanayoyaona wao kuwa ni "uzushi", mimi
siyaoni hivyo kwa sababu bid'a
wanavyoielewa wao sivyo ninavyoielewa mimi. Kwa ajili hii, katika uhai wangu
wote mpaka hapa nilipofika, sijapata kupinga maulidi hata siku moja. Kinyume
cha hilo, nimekuwa nikihudhuria
maulidini, na wakati mwengine kutoa khutba -- si hapa Mombasa tu, bali Afrika
ya Mashariki nzima na hata ng'ambo, kuanzia 1955 (nilipoanza kutoa khutba
hadharani) hadi hii leo. Kama uko ushahidi wa mimi kupinga maulidi, nawaomba
"wakereketwa" watutolee.
Wakasema tena: "PILI: Ukawa kadiani ukapinga kwamba
Mtume S.A.W siyo Mtume wa mwisho ikawa
Gulam Ahmed ndiye wa mwisho kuambatana na safari yako isiyoeleweka, ukapinga
kabisa thibitisho la Kuran Mtume Muhammad S.A.W
kwamba ndiyo wa mwisho".
MAJIBU: Astaghfirullah! Watu hawa
hawamchi Mola wao? Hayo yote ni uwongo! Kama "wakereketwa" wadai
hivyo, ninawaomba wawatolee Waislamu ushahidi wao. Wangu mimi, mbali na
ninayoyasema katika darasa zangu, ni kijitabu changu kiitwacho Hakika ya Ukadiani ambacho, miaka
isiyopungua thalathini iliyopita, kilichapishwa na kuenezwa na National Union
of Kenya Muslims wakishirikiana na Ansaar Muslim Mission ya Mombasa. Humo
nilieleza uwongo wa Mirza Ghulam Ahmad na ukafiri wa Ukadiani.
Vile vile, miezi michache
inayokuja inshallah, nina azma ya kuchapisha tafsiri ya Kiswahili ya Sura Al-Ahzaab ambamo ndani yake nimetoa
ushahidi mwingi sana, ambao haujapatapo kuchapishwa kwa urefu hivyo kwa lugha
ya Kiswahili hadi hii sasa, kuthubutisha kuwa Muhammad (s.a.w.w.) ni Mtume wa
Mwisho, na kuwa hakuna mtume mwengine baada yake. Pia nimejibu kwa tafsili
upotofu wote ambao Makadiani wameuandika katika maelezo yao ya Sura 33:40
katika tafsiri yao ya Kiswahili ya Qur'ani
Tukufu.
Wakaendelea kusema:
"TATU: Ukawa Shia, ukamkadhibisha Mwenyezi Mungu pamoja na Mtume wake
S.A.W. na kwamba Jibril alifanya hiana,
kwamba Kuran ina kasoro ukawatukana wake za Mtume S.A.W. pamoja na maswahaba
zake radhia allahu anhum
"
MAJIBU: Ni kweli mimi ni Shia Ithnaashari. Hilo
silifichi wala silionei aibu kwa sababu ninaamini kwamba kuwa Shia si kuwa
kafiri. Nguzo tano zinazokubaliwa na Waislamu wote, mashia vile vile
wanazikubali. Hali kadhaalika nguzo za imani.
Kuwa Shia
"wanamkadhibisha Mwenyezi Mungu pamoja na Mtume wake S.A.W."; huo ni
uwongo ulio wazi. Kwa Shia, yoyote anayefanya hivyo huwa ni kafiri wa kutiwa
Motoni. Hilo ndilo lililomo katika vitabu vyao.
"Kwamba Jibril alifanya
hiana"; hilo nalo pia ni uwongo. Ukisoma vitabu vya fiqhi vya madhihabi ya
Shia utaona kwamba anayeamini hivyo si kafiri tu, bali ni najisi kamwe! Ngozi ya mwili wako ikigusana na ngozi ya
mwili wake lazima yako uioshe. Haya! Ikiwa hiyo ndiyo imani yao, vipi watu hao
watarudi waseme wao kuwa "Jibril alifanya hiana"?!
"Kwamba Kuran ina
kasoro"; hilo pia ni uwongo. Imani ya Shia ni kama ile ya Waislamu wote:
kuwa hii Qur'ani tuliyonayo sasa ndiyo
ile ile iliyokuwako wakati wa Mtume Muhammad (s.a.w.w.) shilingi kwa ya
pili. Haikubadilika hata kitone. Kwa maelezo zaidi juu ya jambo hili, kwa
anayetaka kujua msimamo wa Shia, ninamshauri asome kitabu changu kiitwacho Shia na Qur'ani : Majibu na Maelezo,
kinachoweza kupatikana bure kutoka
ofisi yoyote ya Bilal Muslim Mission ya Mombasa (S.L.P. 82508) au ya Dar es
Salaam (S.L.P. 20033). Humo utaona majibu ya Shia juu ya tuhuma zote juu ya
Qur'ani Tukufu zinazotolewa na watu kama kina "wakereketwa".
Kuwa nimewatukana "wake
za Mtume (s.a.w.w.) pamoja na maswahaba zake radhia allahu anhum"; hilo
pia ni uwongo. Nimewatukana wapi? Ninawaomba "wakereketwa" watoe
ushahidi wa nilipofanya hivyo.
Imani yangu mimi, na imani
ya Shia wote, juu ya maswahaba nimeieleza katika kitabu changu chengine
kiitwacho Shia na Sahaba : Majibu na
Maelezo ambacho, vile vile, unaweza kukipata kutoka Bilal Muslim Mission.
Humo nimechapisha kwa Kiarabu, pamoja na tafsiri yake ya Kiswahili, dua ya
kuwaombea Mwenyezi Mungu maswahaba ambayo Shia huisoma. Kwa wale wasiolijua
hilo, dua kama hiyo haipatikani katika madhihabi yoyote mengine ya Kiislamu isipokuwa ya Shia. Basi vipi watawaombea
Mungu na hapo hapo wawatukane?
"Wakereketwa wa sunnah
Malindi" wameendelea kusema: "NNE: Safari yako ya "Transit"
haijaeleweka itatokomea wapi katika dini, kwa sababu hoja unazotupatiya bado
hatujazielewa rasmi
"
MAJIBU:
Safari
yangu ya transit (mpito)
waliyoikusudia ndugu zetu hao ni hili la mimi kuwa Shia baada ya kuwa mfuasi wa
Imam Shaafi'i (Sunni). Na hayo wameyaandika kwa namna ya kumfikirisha yoyote
anayeyasoma makala yao hayo kuwa nimefanya kosa kubwa -- la kutoka madhihabi
mamoja na kuingia madhihabi mengine. Wala hilo si kweli -- si kosa wala si ila
-- kwa ushahidi wa yaliyofanywa na wanazuoni kadhaa wa kadhaa ambao mimi siwi
hata viatu vyao!
Kwa mfano, tunaposoma
historia tunaona wanazuoni kadhaa wa kadhaa waliobadilisha madhihabi kwa kutoka
yale waliyozaliwa nayo wakaingia mengine, na mara nyengine wakarudi tena katika
yale yale yao ya kwanza!
Katika karne za nyuma,
tunasoma ya Sheikh Muhammad bin Abdalla aliyefariki mwaka wa 268 Hijria. Huyu
kwanza alikuwa akifuata madhihabi ya Imam Maalik. Imam Shaafi'i alipohamia
Misri, mwanachuoni huyo aliwacha madhihabi ya Maalik, akaingia ya Shaafi'i;
kisha akarejea tena kwa Maalik. Mwengine ni Abu Ja'far bin Nasr at-Tirmidhi
aliyefariki mwaka 295 Hijria. Huyu alikuwa mkubwa wa Mashaafi'i huko Iraq.
Lakini mwanzo alikuwa Hanafi; alipokwenda hijja ndipo alipotoka, akawa
Shaafi'i. Wa tatu ni al-Khatib al-Bughdadi al-Hafidh, aliyefariki mwaka wa 493
Hijria. Huyu alikuwa Hambali, kisha akawa Shaafi'i. Wane ni Abuu Said aliyefariki
mwaka wa 562 Hijria. Yeye alikuwa Hanafi mwanzo; kisha akawa Shaafi'i. Wa tano
ni Sayf al-Aamadi, mwanachuoni mashuhuri wa ilimu ya Usuli aliyefariki mwaka wa 631 Hijria. Yeye alikuwa Hambali mwanzo;
halafu akawa Shaafi'i. Wa sita ni Sheikh Muhammad bin Dahhaan aliyekuwa bingwa
wa ilimu ya Nahau (Sarufi). Huyu
alikuwa Hambali mwanzo; kisha akawa Shaafi'i. Khalifa wa zama zake alipotaka
mwanachuoni wa Nahau ili amfundishe
mwanawe fani hiyo, akawa Hanafi. Kisha akarudi akawa Shaafi'i tena!
Kuna na Sheikh Taqiyyud Diin
bin Daqiiq. Huyu mwanzo alikuwa Maaliki, kisha akawa Shaafi'i. Na Sheikh
Abdulaziz bin al-Khuzaa'i aliyekuwa kati ya wakubwa wa madhihabi ya Maalik.
Lakini Imam Shaafi'i alipokwenda Baghdad, aliyawacha ya Maalik akamfuata
Shaafi'i. Kuna na Abu Ja'far at-Twahaawi aliyekuwa Shaafi'i, akasoma kwa
mjombake (al-Muzani). Baadaye akawa Hanafi. Mbali Ibn Faaris. Huyu alikuwa
Shaafi'i kwa kumfuata babake. Kisha akawa Maaliki.
Hayo ni ya karne nyingi
zilizopita, na ya nchi za mbali. Hebu sasa tuangalie ya hii karne yetu, na ya
nchi zetu za Afrika ya Mashariki.
Wa kwanza ni Sheikh Aly bin
Abdalla Mazrui, babake Sheikh Al-Amin bin Aly Mazrui, aliyekuwa Kadhi Mkuu wa
Kenya. Huyu mwanzo alikuwa Ibadhi; kisha akawa Shaafi'i. Wa pili ni Sheikh
Muhsin bin Ali Barwani, babake Sheikh Ali Muhsin Barwani aliyekuwa kiongozi wa
Chama cha Hizbu, Zanzibar na mwandishi wa Tafsiri ya Qur'ani Tukufu kwa
Kiswahili. Huyu naye alikuwa Ibadhi vile vile; lakini kisha akawa Shaafi'i. Wa
tatu ni Sayyid Alwy Ahmad Badawy (Mzee Mwenye) wa Lamu aliyekuwa Shaafi'i;
lakini sasa ni Shia Ja'fari kama mimi. Wane ni Sayyid Hassan Ahmad Badawy wa
Lamu vile vile, aliyekuwa Shaafi'i mwanzo; kisha akawa Shia Ja'fari. Lakini
sasa amerudi kuwa Shaafi'i!
Wala si hao tu, bali hata
wao "wakereketwa wa sunnah Malindi", pamoja na mashekhe wao na
viongozi wao, ni hali kadhaalika. Kabla ya wao kuingia haya madhihabi
wayafuatayo sasa, walikuwa wakifuata madhihabi ya Shaafi'i ambayo ndimo
walimozaliwa.
Sasa ni lipi la kioja
nililolifanya mimi? Naomba nielezwe.
Kwa kuwa Shia, mimi sijatoka
katika Uislamu. Yote ya msingi yanayokubaliwa na Waislamu, na sisi Shia
tunayakubali. Kama ndugu zetu "wakereketwa" waamini kuwa sisi Shia
tuna mambo yoyote ya kikafiri, basi watoe makaratasi yao kuyaeleza hayo moja
moja -- kiilimu na kwa lugha ya adabu, bila ya matusi -- ili tupate kuyajadili
kama tulivyofanya haya ya maulidi.
Kwa faida ya ndugu wasomaji
wa makala haya, kama vile ambavyo kuna mambo ambayo madhihabi ya Kishia
hukhitalifiana na madhihabi mane ya Kisunni, hali kadhaalika kuna mambo ambayo kila madhihabi matatu ya Kisunni
hukubaliana na ya Kishia, na moja tu la Kisunni likawa peke yake. Pia kuna na
mengine ambayo madhihabi ya Kisunni na ya Kishia hukubaliana, na ya kina
"wakereketwa" peke yao yakawa tafauti!. Kama wanataka tuyajadili
hayo, ahlan wasahlan.
Mpaka hapa, tumekoma mjadala
wetu kuhusu maulidi. Twataraji wasomaji wetu -- wa maulidi na wapinzani wao --
wamestafidi.
Ifikapo Rajab ya mwaka huu
tulionao inshallah, tutaanza mfululizo mpya wa makala ya kueleza: hawa wapinga
maulidi, khitma, tawasuli, wakavunja makaburi na mihrabu, na kama hayo, ni kina
nani? Wanafuata madhihabi gani? Madhihabi hayo yalianza wapi? Lini?
Yalianzishwa na nani? Yaliingia lini huku kwetu Afrika ya Mashariki? Vipi? Yameeneaje?
Jee, wanaamini kuwa Waislamu wasiokuwa na itikadi kama zao -- wakiwamo masunni
-- ni Waislamu? Na mengi mengine.
Wassaalaamu alaykum.
basi wale waliomwamini yeye
(Mtume
Muhammad)
na
kumhishimu na kumsaidia,
na
kuifuata nuru iliyoteremshwa pamoja naye;
hao
ndio wenye kufaulu.
(Surah 7:157)
Kimechapishwa na kutolewa na
BILAL MUSLIM MISSION OF KENYA
P.O.
BOX 82508 MOMBASA TEL: 229641 FAX 230909
e-mail :
tableegh@kenbilal.org