Mwanamke atasema nimekuoza nafsi yangu kwa muda fulani kwa mahari kiasi fulani. Mume aseme nimekubali.
Ni lazima katika ndoa ya Mut'a kitajwe kiwango cha mahari walichokubaliana. Na isipotaiwa ndoa haisihi.
Ndoa ya Mut'a haina haja ya walii wala shahidi.
Hapa wamekhtilafiana, wako waliosema kuwa, mwanamke bikra anaweza kuolewa Mut'a bila ya idhini ya walii wake. Na wako waliosema: Mwanamke bikra lazima asimamiwe na walii wake iwe ni ndoa ya Mut'a au ya daima. Na hii ndiyo Fat'wa ya Asayyid Abdul'qasim Al'musawy Al,khui.
Mume na mke wana haki ya kuwekeana sharti, kwa mfano, mume hataki wazae na mkewe muda huu. Au mume na mke wamekubaliana kuwa watarithiana pindi mmoja wao atafariki.
Mtoto anaezaliwa katika ndoa ya Mut'a ana haki zote sawa na mtoto wa ndoa ya daima.
Mke wa ndoa ya Mut'a hana talaka, umalizikapo muda waliokubaliana kuoana basi ndoa hukatika. Na kuanzia hapo atakaa eda kwa muda wa hedhi mbili, ikiwa ni mwanamke asiyepata hedhi, basi atakaa eda siku arobaini na tano.
Inajuzu katika ndoa ya Mut'a kuoa wake wengi, kwa sababu wake wa Mut'a hawaingii katika idadi ya wake wa ndoa ya daima. Kwa hivyo unaweza kuoa wake alfu moja wa Mut'a. Amesema Shafii kuwa:- "Ibnu Jurayhi aliowa Mut'a wake tisini."