Wakati tunapojiandaa kwa kuianza Ramadhani, tunapaswa kujua kwamba, amri ya kufunga ni yake Mwenyezi Mungu. Na wala amri hii haikuwa ya yeyote yule kati ya viumbe. Muda huu wa Saumu mtu hutakiwa kufanya ibada kwa wingi. Kuomba, kusoma dua mbali mbali na kuomba maghfira.
Na masharti yafuatayo ukiwa umeyakamilisha utalazimika kuanza Saumu, na wala hutokuwa na udhuru wowote ukuzuiao kufunga.
Mwenyezi Mungu anaamrisha wasali lakini shuruti (watawadhe au watayammamu). Basi kafiri pia inampasa afunge, lakini shururti za kusihi hiyo saumu yake ni kukubali Islamu, na Kafiri anaweza kusilimu.
Mtu anaweza kila usiku wa Ramadhani kuweka nia ya kufunga kesho yake, na ni vizuri usiku wa mwezi wa Ramadhani aweke nia ya mwezi mzima.
Wakati wa kuweka nia ya Saumu ni kutoka mwanzo wa usiku hadi adhana ya asubuhi (Alfajiri) kwa saumu za fardhi, ama saumu za sunna huanzia mwanzo wa usiku, hadi kiasi cha kunuia kumebaki kufikia magharibi, ikiwa mpaka wakati ule hakutenda kitu cha kuvunja saumu, basi hapo aweke nia ya saumu, na saumu itasihi. Ikiwa mtu bila ya kuweka nia kabla ya Alfajiri akalala, na akaamka kabla ya adhuhuri na hapo akiweka nia, saumu yake itasihi, ikiwa saumu ya fardhi au ya sunna lakini akizindukana baada ya adhuhuri, basi hapo hawezi kuweka nia ya saumu ya fardhi. Ikiwa kabla ya alfajiri kanuia na akalala na asiamke ila baada ya magharibi, saumu hiyo itasihi haidhuru neno.
Lil-Laahi Ta'Ala, maana yake, kufunga kwake iwe Lil-Laahi, Ta'aala tu, au akiongeza Riya (kwa kujipendekeza) tu hapa saumu yake haitasihi.
Mzee mkubwa, na kadhalika kikongwe wasio na uwezo wa kustahamilia Saumu, wanaruhusiwa na sheria wale na watoe sadaka ya kibaba (sawa na kilo kasorobo) kwa kila siku. Kibaba hiki kiwe ni cha chakula kitumiwacho sana na watu wa sehemu hiyo, na pia hukumu hii humhusu mwanamke anayenyonyesha na aliye na mimba wakijichelea au kuchelea wana wao, wanaruhusiwa na sheria kufuturu. Isipokuwa hawa wawili wa mwisho watalazimika kulipa nyudhuru zao zikusha kabla ya Ramadhani nyengine kufika.
Msafiri asafiriye umbali wa Km. 48 halazimiki kufunga, bali atafuturu ingawa haambiwi ale bali atajizuia vivyo hivyo na kulipa baada Ramadhani kumalizika. Na safari, sharti iwe ya halali, isiwe kazi yake kama kondakta, dreva nahodha n.k. asiwe atakaa huko zaidi ya siku 10 akiwa atakaa zaidi ya siku 10 atafunga hata huko huko safarini.
Kafiri wa kuzaliwa akisilimu halazimiki kulipa Saumu zilizompita alipokuwa ukafirini. Kadhalika mtoto akibaleghe, na aliyekuwa na kichi (wazimu). Ama aliyepitiwa na Saumu kwa kuwa na hedhi, nifasi, ugonjwa,n.k. hulipa.
Ili kuthibitisha utiifu wetu kwa Mwenyezi Mungu na ili Saumu zetu zikubaliwe, ni sharti tutekeleze amri zake zote pasina kuziacha zinine. Sala i mojawapo wa mahimizo makubwa kwa Mwislamu na lau atajisumbua kwa kuumwa na njaa bure pasina kusali, ajuwe kuwa hana fungu lolote katika Saumu yake. Kwa hivyo tukiwa tunataka thawabu zaidi na zaidi ni lazima hata tusiziache.
Sala ni nguzo ya pili katika nguzo za Islamu, na tukumbuke kwamba, tukiwa na sala pungufu, hata mali zetu zi katika mafungu yasiyotakikana, na zikiwa kamili, hata ibada zinginezo zitakuwa makbuli Inshaallah.