rudi maktaba > Fiqh > Yaliyomo >

'SAUMU' KATIKA BIBLIA

Saumu kama ilivyopokewa katika Qur'an kadhalika imepokewa katika vitabu vya dini mbali mbali.

Kulingana na ushahidi wa Aya tuliyoitaja huko nyuma inayosema "Enyi mlioamini, mmefaradhiwa kufunga kama walivyofaradhiwa wa kabla yenu ili mpate kumcha Mwenyezi Mungu! Ulazima wa Saumu kwa watu wote wa leo na wa kale umethibiti.

Ingawa katika Aya hiyo Mwenyezi Mungu tujulisha kama, jee Saumu tuliyofaradhiwa sisi ndiyo ile ile na kwa namna ile ile na kwa idadi zile zile walizofaradhiwa wa kabla yetu ama kwa namna iliyo tofauti? Hata hivyo si lazima juu yetu kujuwa. Na Mwenyezi Mungu alitujulisha hili ili tusiwe na malalamiko (kama ilivyo ada ya mwanadamu) kuwa, kwa nini sisi tulazimishwe Saumu na hali wa kabla yetu hawakufunga na hali wao ni waja kama sisi? Ndiyo maana Akatujulisha mapema kabla ya nyudhuru zetu kutolewa.

Ingawa ndugu zetu Wakristo wanatambua wazi Fardhi hii, kwa bahati mbaya wao hawakuijali bali wameyashughulikia mengine.

Hebu na tuangalie katika kitabu chao (Biblia - Agano jipya).

Katika MATHAY0 6, kifungu cha 16 hadi 18 kumeandikwa hivi: "Tena mfungapo msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana maana hujiumbua nyuso zao ili waonekane na watu kuwa wanafunga. Amin nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao. Bali wewe ufungapo jipake mafuta kichwani, unawe uso, ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini na Baba yako aonaye sirini atakujazi."

Pia katika MATHAYO 4, kifungu cha 1-2 imeandikwa hivi: "Kisha Yesu alipandishwa na Roho nyikani, ili ajaribiwe na Iblisi. Akafunga siku Arobaini mchana na usiku, mwisho akaona njaa."

Ndugu mpendwa, jee pana udhuru wowote tena wa kutofunga kwa Wakristo baada ya ushahidi huu? Jee inafaa kutumia mbinu zozote zile za ulaghai ili kuupuza maamrisho ya Allah? Jee inasihi mtu kutangatanga mabarabarani akinadi kwa kila namna ya vishindo eti "Mimi nimeokoka.....Mimi nimeokoka..." Na hali anaihepa Saumu? Hasha Wakalla.......hilo haliwi.