MAFUNDISHO  KUHUSUTAYAMMAM

BISMILLAHIR  RAHMAANI  RAHIIM

 SEHEMU YA KWANZA

 MAANA YA TAYAMMAM

Tayammum ni kutawadha kwa kutumia mchanga au udongo kutokana na udhuru wa kisheria kama kukosa maji au ugonjwa. Na tayammum huwa badala ya udhu au ghusli na ni wajibu pindi maji yanapo kosekana maji ya kutawadhia, au kama kukiwa na udhuru wa kutumia maji kama kuwa na ogonjwa au kutokana na baridi au kuogopa kuyatumia maji kwa sababu ya kuyahitaji kwa kunywa au kutokuwepo nyenzo ya kutowezesha kuyafikia maji hayo. Na haifai kutumia kitu chochote katika tayammam tafauti na mchanga halisi au udongo.

MAMBO YAWAJIBISHAYO   TAYAMMAM

Kwa ujumla ni  nyudhuru  ambazo huangusha wajibu wa kutumia maji, na nyudhuru hizo ni kama zifuatazo: 

KWANZA: Kuto patikana maji   yatoshayo kutawadhia au kuoga, hata kama  yatakayo patikana  hayata kuwa na sifa zizingatiwazo katika suala la maji.

MAS’ALA:  Haijuzu  kwa msafiri kufanya tayammam pale tu atakapo tambua ya kuwa hakuna maji, bali hapana budi kuthibitisha kuto kuwepo kwa maji kwa kuyatafuta, na ikiwa atakuwa na ihtimali juu ya kuwepo maji kati ya watu wale anao safiri nao au katika msafa wake au kwa baadhi ya wapita njia, itakuwa ni wajibu kwake kuyatafuta hadi awe na yakini au uhakika wa kuto kuwepo kwa  maji,  lakini ikiwa atafahamu ya kuwa maji hayapatikani kabla ya kutafuta na akawa na matarajio ya kupatikana maji hayo, haitawajibika kwake kuyatafuta, na ikiwa atakuwa jangwani na akawa na ihtimali ya kupatikana maji sehemu iliyo  karibu nae au njiani, itakuwa ni wajibu kwake kuyatafuta, na kauli iliyo ahwat na ya wajibu  ni kuwa  inabidi maji hayo ayatafute pande nne.

UTAFUTAJI WA MAJI.

Sehemu za milimani  atatupa mtupo mmoja wa mshale, na  sehemu ya tambalale atatumia mitupo miwili ya mishale, na ikiwa  anayo ihtimali  ya kuto kuwepo maji sehemu hizo, si wajibu kwake kuyatafuta sehemu hizo, na ikiwa  atakuwa na   ihtimali  kati ya sehemu  moja wapo kati ya hizo itamuwajibikia kuyatafuta  sehemu hiyo, na  kuwepo dalili au uthibitisho ni sawa na kuwa na yakini juu ya kuwepo kwake, na ikiwa atashuhudia kutokuwepo maji katika  pande fulani haita muwajibikia kuyatafuta  sehemu hizo.

MAS’ALA:  Ikiwa atayatafuta maji  kabla ya kuingia wakati wa sala na hakuweza kuyapata, haitamlazimu kuyatafuta tena baada ya kuingia wakati wa  sala, hata kama  atakuwa na ihtimali ya kupatikana  kwa maji hayo,  na ikiwa  hakuya tafuta katika baadhi ya sehemu   kutokana na kuwa na yakini ya kutokuwepo maji sehemu hiyo, kisha  akawa na shaka  ya kuwa kuna maji au hakuna,  hapana budi kwake kukamilisha  utafutaji, vile vile ikiwa atahama kutoka sehmu hiyo  itamlazimu  kukamilisha utafutaji  wake huo.

MAS’ALA:  Ikiwa atayatafuta maji  kwa ajili ya sala fulani, utafutaji huo utatosheleza kwa ajili ya sala zinginezo, na si wajibu kwake kutafuta tena kila ufikapo wakati wa sala hizo, hata kama atakuwa na matarajio ya kupatikana  maji  ikiwa  atatafuta  tena, kwa matarajio ya kuyapata maji hayo.

MAS’ALA:  Ulazima wa kutafuta maji  huporomoka pindi wakati wa sala unapo kuwa finyu kwa kiasi cha kuweza kusali sala ile,  pia huporomoka  ikiwa  ataogopa kupatwa na madhara juu ya nafsi yake  au mali yake  kutokana na wezi au wanyama wakali au mfano wa hayo, au akiwa na ihtimali  ya kutokea madhara asiyo weza kuyastahamilia.

MAS’ALA:  Ikiwa  ata acha kutafuta maji na badala yake akafanya tayammam na kusali  katika wakati  mrefu, kwa kutaraji kuwa  ametekeleza  sheria, tayammam yake na sala yake vitakuwa na ish’kali katika kusihi kwake, hata kama itabainika kuto kuwepo kwa maji.

MAS’ALA:   Ikiwa  atakuwa na maji na akasahau  au akaghafilika  ya kuwa alikuwa na maji, na akafanya tayammam  na kusali  kisha akakumbuka  ya kuwa  anayo maji kabla ya kumalizika wakati wa sala hiyo, ni juu yake wakati huo kutawadha na kuirudia sala hiyo.

MAS’ALA:   Ikiwa atayatafuta  maji na hakuweza kuyapata  na kukata tamaa ya kupata maji katika wakati wa sala  na akafanya tayammam  na kusali, kisha ikabainika  ya kuwa kuna maji sehemu hiyo  aliyo tafutia kwa mtupo mmoja au miwili au katika  msafara  au kati ya wale alionao safarini, sala yake aliyo Sali ni sahihi na si wajibu kwake kuirudia au kuilipa sala hiyo.

PILI: kuto kuwepo urahisi wa  kuyafikia maji yaliyopo, ima kwa kushindwa  kuyafikia kutokana na maumbile kama kuwa na umri mkubwa  na mfano wa hayo,  au kuyafikia kwake  kutamlazimu kufanya tendo la haramu  kama kutumia chombo cha ghasbi (kilicho nyang’anywa), au  kwa kuiogopea nafsi yake  au heshima yake au mali yake  kutokana na wezi au kupotea na mengineyo.

TATU:  Kupatikana madhara kwa kutumia maji, kama kuwa na baridi kali,  sawa baridi hiyo iwe ni yenye kuleta  madhara au kuzidisha maradhi au yakiwa ni sababu ya kuchelewa kupona, pia kuwa na vipele vinavyo zuwia kutumia maji ikiwa havikusitiriwa, ama ikiwa  vime sitiriwa  kwa dawa, hapo jukumu litakuwa ni  kufanya  udhu wa  jabira (pio pio)  kama tulivyo  tangulia kueleza katika  udhu, pia ikiwa kuna mikwaruzo   ambayo haiwezekani  kuivumilia  ikiwa  itamwagiwa maji  (yaani ikiwa atakuwa na ugonjwa wa ukoma)  nao ni ugonjwa  ambao hupelekea baadhi ya sehemu za ngozi  kuchanika chanika,  wakati huo si lazima kuwa na yakini au matumaini juu ya kupatikana madhara kwa kutumia maji, bali inatosha kuwa na ihtimali  itumikayo kwa watu wenye akili, na ambayo huitwa  kwa jina la khofu  (woga).

NNE:  Taabu na matatizo ambayo   ni vigumu kuyastahamili, sawa iwe ni katika kuyafikia maji au kuyanunua  kwa thamani  ambayo itasababisha  madhara katika mali yake,  la sivyo  itamlazimu kuyanunua hata kama  ni kwa kiwango cha juu, au kukawa na madhara katika kuyatumia maji hayo kutokana  na baridi kali au kubadilika kwa maji kwa kiwango  ambacho  kina pingana na maumbile yake, au ikiwa yatasababisha  madhara kwa kuyatumia kwake,  kama ikiwa  anayo maji kidogo ambayo hayatoshi  kuweza  kutawadhia au kuoga au kuloweshea kichwa  kutokana na kuyahitaji  wakati wa joto kali, kiasi  kwamba akiyakosa maji hayo atajiweka katika taabu kubwa.

TANO:  Kukhofia  kiu  juu yake mwenyewe  au mwenziwe  kwa wale wenye mahusiano nae na ambao ni wajibu wake kuwalinda na kuwahifadhi na kuyashughulikia  mambo yao,  hata kama si nafsi zenye kuheshimika  sawa awe mwanadamu au mnyama. Na ikiwa ataogopa kiu kwa watu wengine ambao hawahusiani nae au mambo yao haya muhusu, lakini kisheria  analazimika  kumuhifadhi, au ikiwa hakumuhifadhi  na kumuangalia  itamlazimu  mtu yule kupatwa na madhara au matatizo, khofu kama hiyo itaungana na mambo yale mengine tuliyo yataja  yawajibishayo tayammam.

SITA:  Awe amekalifishwa  kufanya wajibu ambao hautimii  isipokuwa kwa kutumia maji, kama kuondoa  khabathi  msikitini. Hakika ni wajibu kwake kutayammam na kuyatumia maji katika kutwahirisha msikiti, hivyo hivyo ikiwa mwili wake  au nguo zake zitakuwa  zime najisika, na maji yaliyopo  hayatoshelezi kutwahirisha  hadathi na khabahi kwa pamoja, wakati huo itamlazimu  kuyatumia maji hayo kwa kuondoa  au kutwahirisha khabathi, japo kuwa ni bora zaidi  katika sehemu hiyo  kwanza kuyatumia maji  kwa kuondoa  khabthi kisha baada ya hapo kutayammam.

SABA:    Ufinyu wa wakati katika kuyafikia maji  au kuyatumia , kiasi kwamba  ikiwa  atatawadha  au kuoga  itamlazimu kuisali sala ile  au baadhi ya sehemu ya sala hiyo nje ya wakati,  wakati huo itafaa kutayammam katika sehemu zote zilizo tajwa.

MAS’ALA:  Ikiwa itawajibika kufanya tayammam  kutokana na kukosekana  baadhi ya  masharti ya kutawadha au kuoga, na akatawadha au  kuoga  kwa  kusahau au kwa  kughafilika au kwa kuto jua,  udhu au ghusli hiyo haito swihi.

 SEHEMU YA PILI

VITU VITUMIKAVYO  KATIKA   TAYAMMAM

Kauli yenye nguvu inasema kuwa  inajuzu  kutayammam  kwa kila kitu kiitwacho kwa jina la Ardhi, sawa uwe mchanga, udongo, changalawe, au mawe, pia matofali na ardhi ya chokaa  kabla ya kuchomwa, japo kuwa kauli iliyo ahwat na ya sunna  inasema ni bora kutumia udongo tu ikiwa itawezekana, pia kauli  iliyo ahwat  kama si yenye nguvu zaidi inasema  kuwa  kitu kitumikacho kutayammam  kiwe ni chenye kugandia  juu ya mikono, haitoshi kutayammam juu ya kitu kama jiwe mororo lisilo na vumbi juu yake.

MAS’ALA:  Haijuzu  kutayammam  kwa kutumia kitu  kisicho  faa kuitwa Ardhi, hata kama asili yake ni  ardhini, kama majivu, mimea, na baadhi ya madini kama Dhahabu na Fedha,  ama jiwe la  akiki na Fairuzi na mfano  wa hayo kati ya mawe  matukufu,  kauli yenye nguvu  inasema ya kuwa  inajuzu kutayammam kwa kutumia vitu hivyo  pamoja na kuthibiti ugandiaji, vile vile vyombo vya dongo, chokaa, na matofali baada ya kuyachoma, japo kuwa kauli yenye nguvu  inasema kuwa ni bora kuvitanguliza vitu vingine juu ya vitu hivi.

MAS’ALA: Haijuzu kutayammam  kwa kitu kilicho najisi, wala  kilicho cha ghasbi (kilicho nyang’anywa au kutumika bila ruhusa ya mmiliki wake), wala  kilicho changanywa  na kitu kingine  kiasi kwamba halithibiti juu ya kitu hicho jina la Ardhi, ndio,  haitadhuru  ikiwa  kitu kilicho changanywa hakidhihiri katika udongo au mchanga huo kwa kawaida,  na ikiwa mtu atalazimishwa  kukaa kwa muda mrefu katika sehemu aliyo nyang’anywa  au kudhulumiwa, kauli  iliyo wazi inasema  kuwa inajuzu  kutayammam  kwenye ardhi hiyo aliyopo, lakini atatosheka tu na kuweka mikono na wala asipige juu ya Ardhi kwa mikono yake.

MAS’ALA: Ikiwa  kutakuwa na  shubha kati ya udongo  ulio maghsub  na ulio halali itawajibika  kuto tumia aina zote mbili  hizo,  na ikiwa kutakuwa na shubha kati  ya majivu  na  mchanga  na akatayammam kwa kutumia vitu viwili hivyo  tayammam yake itakuwa sahihi, bali ni wajibu kufanya hivyo ikiwa hakuna kitu kingine cha kutumia, na hukumu ni hiyo hiyo  ikiwa kutapatikana shubha kati ya mchanga twahara na najisi.

MAS’ALA:  Vumbi lililo kusanyika  juu ya nguo au mfano wa nguo ikiwa  litahesabika kuwa ni mchanga  kiasi kwamba ukawa  kama mchanga  katika mazowea ya watu,   itajuzu kutayammam kwa kutumia vumbi hilo kutokana na kauli iliyo wazi, japokuwa kauli  iliyo ahwat inasema ni bora kutumia kitu kinginecho  tofauti na vumbi hilo,  na ikiwa vumbi ni jingi na lenye kukusanyika  juu ya nguo kwa mfano  na kukawa na uwezekano wa kulikung’uta na kulikusanya   kiasi likionekana  itathibitika kuwa ni mchanga  itabidi kulitumia vumbi hilo, ikiwa haikuwezekana kutumia kitu kingine.

MAS’ALA:  Ikiwa  haikuwezekana kutayammam kwa kutumia Ardhi na vitokanavyo na Ardhi  kama vumbi,  hapo itamlazimu kutayammam kwa udongo, nao ni udongo ulio changanyika na maji mfano wa tope na ambao hugandia juu ya mikono, na  haijuzu kuuondoa udongo wote,  bali kauli iliyo ahwat inasema kuwa haifai kuondoa kitu kwenye mikono  isipo kuwa kile ambacho kukiondoa kwake kutathibitisha kuwa  umetumika mkono katika upakaji, na ikiwa itawezekana kuukausha  na kuutumia kwa kutayammam itabidi kufanya hivyo, na wakati huo  haitajuzu   kutayammam kwa udongo. Na  ikiwa itashindikana  kutumia vitu vilivyo tajwa hapo kabla  kutayammam,  itabidi kutayammam kwa kutumia kitu chenye vumbi  yaani kitu ambacho  kina vumbi jingi au chenye mkusanyiko  wa vumbi mkusanyiko ambao  hukubalika kuwa ni mchanga  ulio laini kama tulivyoeleza hapo kabla.

MAS’ALA:  Ikiwa atashindwa   kuipata Ardhi, vumbi, na udongo  au kitu chenye vumbi, hapo atakuwa amekosa twahara, na kauli iliyo adh’har  wakati huo  ni kuwa sala ita anguka katika wakati wake na itakuwa ni wajibu kuilipa nje ya wakati wake. Na ikiwa  mtu ataweza kupata barafu na kaweza  kuiyayusha  na kuitumi katika udhu, au akaweza  kuitumia kupaka uso na mikono  kiasi kwamba itathibiti anuani ya kuosha na kupaka  kichwa  na miguu miwili  kwa unyevu nyevu wa mikono  itabidi kufanya hivyo   na haitafaa kutayammam,  ama ikiwa hakuweza  kupaka  kwa kutumia barafu hiyo  kiasi kwamba haitathibiti anuani ya kupaka, kauli iliyo wazi inasema itabidi kutayammam  japo kuwa kauli iliyo ahwat na ya sunna inasema,  inabidi kukusanya  kati ya tayammam  na kupaka kwa kutumia barafu hiyo  na kuisali sala hiyo ndani ya wakati.

MAS’ALA: kauli iliyo ahwat ni kuwa ni sunna kukung’uta  mikono baada ya kupiga juu ya Ardhi, na kauli ya ahwat  ya wajibu ni kuwa vitu vitumikavyo  kutayammam  viwe safi kwa hali ya kawaida, na ni sunna  viwe ni katika Ardhi halisi na ziwe ni sehemu za juu, na ni makruhu  kuwa ni   sehemu ya  bondeni,  na usiwe ni mchanga wa njiani.

NAMNA YA  KUTAYAMMAM.

Utaanza kwa kupiga vitanga viwili juu ya  Ardhi  na inatosha kuweka vitanga hivyo juu yake vile vile- na kauli ya ahwat ya wajibu ni kuwa inabidi kufanya hivyo mara moja-.

Kisha  utavitumia vitanga hivyo baada ya kuvipiga juu ya Ardhi  vyote kwa pamoja kupaka  paji  lote  la uso  kisha pande mbili za uso kulia na kushoto kwa kuanzia kwenye maoteo ya nywele  hadi kwenye nyusi na utaendelea   hadi kwenye ncha ya juu ya pua iliyo ungana na paji la uso,  na kauli iliyo ahwat  inasema kuwa ni bora zaidi pia kupaka pande mbili za uso,  kisha utapaka sehemu yote ya juu ya kitanga cha mkono wa kulia  kwa kuanzia kwenye  zand (maungio ya vitanga vya  mkono) hadi kwenye ncha za vidole kwa kutumia mkono wa kushoto, kisha  utapaka  sehemu yote ya  juu ya kitanga  cha mkono wa kushoto  vile vile kwa kutumia  kitanga cha mkono wa kulia.

MAS'ALA:  Si wajibu kupaka kwa kutumia vitanga vyote vya mikono, bali inatosha kupaka  kwa kutumia baadhi ya sehemu ya vitanga hivyo kiasi ambacho kita enea kwenye paji lote la uso na pande mbili za uso pia  kama ilivyo  tangulia.

MAS’ALA:  Kauli iliyo dhahiri  (iliyo wazi)  ni kuwa,  inatosha  kupiga mara moja juu ya Ardhi  wakati wa kutayammam  badala ya  ghusli ( kuoga)  au kutawadha, japokuwa kauli iliyo ahwat na ya sunna inasema ni bora kupiga mara mbili,  pigo la kwanza kwa ajili ya uso,  na pigo la pili kwa  ajili ya vitanga au mikono miwili,  na inatosha katika kufanya ihtiyaat kupaka  mikono na uso katika pigo la kwanza, kisha   utapiga pigo la pili na uta paka mikono yako,  na utafanya hivyo hivyo  iwapo utaweka mikono  juu ya Ardhi.

MAS’ALA:  Ikiwa itashindikana  kupiga na kuweka, pia  kupaka kwa kutumia sehemu ya ndani ya vitanga vya  mikono, utatumia  sehemu ya juu ya vitang hivyo,  vilevile ikiwa vime tapakawa na najisi  sehemu zote  hadi kwenye kitu kitumikacho kutayammam, na hukuweza kuiondoa najisi hiyo, ama ikiwa najisi si yenye  kutapakaa sehemu zote, utaitumia sehemu ile isiyo na najisi kwa kupiga juu ya Ardhi au kuweka juu yake  kisha utapaka  kwa  kutumia sehemu hiyo,  bali kauli iliyo  dhahiri   ni kuwa  si lazima kiungo chenye kupaka na chenye kupakwa  viwe twahara. Na ikiwa juu ya kiungo kinacho pakwa  kuna kizuwizi  kama bandeji au pio pio na hakuna uwezekano wa kulitoa, itamlazimu kupaka juu yake,  ama   pio pio au bendeji  likiwa  sehemu ya kupakia, ikiwa halikufunika sehemu yote, utapaka kwa  kutumia sehemu iliyo bakia, ama ikiwa hakuna sehemu iliyo wazi  kauli ya ahwat na ya wajibu inasema  itakuwa ni wajibu kukusanya kati ya kupaka kwa kutumia mkono  wenye pio pio na kupaka kwa kutumia sehemu ya juu ya mkono baada ya kupiga juu ya Ardhi au kuweka.

MAS’ALA: Mwenye hadathi  ndogoatafanya  tayammam  badala ya udhu. Na mwenye janaba  atafanya tayammam badala ya ghusli ( kuoga),  na mwenye hadathi kubwa tofauti na janaba atafanya tayammam  badala ya ghusli,  na ikiwa  atakuwa na hadathi ndogo, kauli ya ahwat na ya sunna inasema, ni sunna pia kutawadha, na ikiwa hakuweza kutawadha  atafanya tayammam badala ya udhu, na ikiwa ataweza kuoga itamlazimu kuoga, na ikiwa  ataoga haita hitaji kutawadha kwani josho hilo linatosheleza kutawadha, isipokuwa  katika istihadha  mutawassit  (istihadha ya kati)  katika hali hiyo itamlazimu  kutawadha, na ikiwa hakuweza kutawadha  atafanya tayammam  badala ya udhu,  vilevile ikiwa hakuweza kuoga, kuli iliyo dhahiri ni kuwa  atafanya  tayammam moja na  itakuwa imetosheleza kwa ghusli na udhu.

 SEHEMU YA TATU

MASHARTI  YA KUFANYA TAYAMMAM

Ni sharti katika tayammam  kutia Nia  (kunuwia)  kama  ilivyo tangulia kwenye udhu,  na  Nia  hiyo  inabidi iambatane na tendo  la kupiga juu ya Ardhi  au kuweka mikono juu ya Ardhi  kwa kauli iliyo ahwat.

MAS’ALA: Si wajibu katika tayammam  kunuwia badala ya udhu au ghusli, bali inatosha tu kutia Nia ya kujikaribisha kwa Allah,  ndio,  ikiwa  atafanya tayammam mbili, moja  badala ya  ghusli na nyingine badala ya udhu, kwa ihtiyat ni lazima kuzitofautisha tayammam hizo kwa aina fulani, na inatosha  kuzitofautisha  kwa kutia Nia ya ubadala.

MAS’ALA: Kauli yenye nguvu ni kuwa tayammam ni yenye kuondoa  hadathi  ikiwa haikutokea  moja wapo  kati  ya vitu vitenguavyo twahara, na wala si wajibu kutia Nia ya kuondoa hadathi au ya sunna, au kwa ajili ya sala kwa mfano.

MAS’ALA: Ni sharti tayammam  ifanywe na mtu mwenyewe bila kusaidiwa na mtu, vile vile ni sharti kufuatanisha, hata katika tayammam ambayo ni badala ya ghusli,  vile vile ni sharti  kufuatanisha  au kufuata mpangilio  kama ilivyo tangulia,  na kauli ya ahwat ya wajibu ni kuwa, ni lazima  katika kupaka kuanzia juu kuelekea  chini.

MAS’ALA: Mtu ambae  moja wapo kati ya  kitanga chake kimekatika  au vyote viwili, atafanya tayammam kwa kutumia  muundi wa mkono,  na mtu ambae moja wapo kati ya mikono yake umekatika  kuanzia kiwikoni, atafanya  tayammam kwa  kutumia mkono ulio bakia, ima kwa kupiga juu ya Ardhi au kwa kuweka juu yake, na atapaka juu ya paji la uso kwa kutumia mkono huo, kisha atapaka  juu ya mkono huo kwa kutumia Ardhi,  ama  alie katika mikono yote miwili kuanzia kwenye viwiko, itatosha kupaka uso wake kwa kutumia Ardhi,  na mtu mwenye pio pio  au mwenye kizuwizi kwenye mkono wake hukumu yake  ime elezwa hapo kabla, na hapa  zitatumika hukumu zilizo tangulia zihusianazo na pande la nyama lililo zidi au mkono ulio zidi.

MAS’ALA: Ikiwa hakuweza kufanya tayammam yeye mwenyewe  isipokuwa kwa kupata  usaidizi kutoka kwa mtu mwingine  kiasi kwamba inambidi  amsaidie au  ashirikiane nae katika kupiga juu ya Ardhi au kuweka mikono  juu ya Ardhi au juu ya kitu akitumiacho kutayammam  kisha kuiweka juu ya paji la uso na juu ya mikono yake pamoja  na kuwa yeye mwenyewe ndie afanyae tendo la kupaka kwa mikono yake, itambidi kufanya hivyo na yeye mwenyewe ndie atakae tia Nia kwa wakati huo, na ikiwa haikuwezekana kufanya tayammam  au kupaka yeye mwenyewe hata kama ni kwa kusaidiwa, itambidi  amuombe mtu amtayamamishe, na atapiga juu ya Ardhi kwa kutumia mikono ya mgonjwa na kupaka uso kwa kutumia mikono hiyohiyo, na ikiwa itashindikana, itatumika mikono ya yule mwenye kutoa usaidizi yeye mwenyewe na atapaka  kwa kutumia mikono yake, na kauli iliyo ahwat katika hali mbili hizo ni kuwa kila mmoja inambidi kuti nia.

MAS’ALA: Nywele zilizo funika  au kuangukia usoni  ni wajibu kuziinua na kupaka  juu ya ngozi iliyo chini ya nywele hizo, ama nywele zilizo ota kwenye uso, kauli iliyo dhahiri ni kuwa itatosha kupaka juu ya nywele hizo.

MAS’ALA: Ikiwa  mtu atakhalifu utaratibu pamoja na kuto fatanisha, tayammam  itabatilika, hata kama ikiwa ni kutokana na kuto jua au kwa kusahau, ama ikiwa  utaratibu na kufuatanisha havi kukosekana baada ya kuirudia,  tayammam itakuwa sahihi.

MAS’LA: Pete izuwiayo mchanga kufika kwenye vitanga, ni wajibu  kuivua wakati wa kupaka.

MAS’ALA: Ni sharti mchanga utumikao kutayammam uwe mubaha (halali), kama ilivyo elezwa hapo kabla, na kauli iliyo ahwat inasema  sehemu na chombo  chenye mchanga wa kufanyia tayammam visiwe ni  vya ghasbi (kunyang’anya) au vya dhuluma.

MAS’ALA: Ikiwa  mtu atatia shaka  kati ya sehemu moja wapo za kufanyia tayammam ya kuwa  ameifanyia tayammam au la, na  shaka hiyo imekuja baada ya kumaliza au kuvuka sehemu hiyo, shaka hiyo hataitilia maanani, ama shaka ikihusika na sehemu ya mwisho na wakati huo hali ya kufuatanisha bado haija toweka na kabla ya kufanya kitendo kingine kama sala na mfano wake, kauli iliyo ahwat na ya wajibu ni kuwa shaka hiyo itatiliwa maanani,  na ikiwa atatia shaka  kuhusu  sehemu Fulani  baada ya kuvuka sehemu hiyo na kuingia sehemu nyingine, hapo shaka hiyo haitatiliwa maanani, japo kuwa kauli aliyo ahwat na ya sunna ni kuwa atairudia sehemu hiyo.

SEHEMU YA NNE

HUKUMU ZA TAYAMMAM

Haijuzu kutayammam kwa ajili ya sala ambayo wakati wake umefika  ikiwa utafahamu ya kuwa udhuru utatoweka na kuna uwezekano wa kujitwaharisha  kwa maji kabla ya kumalizika wakati wake, bali haijuzu kutayammam ikiwa  huja kata tamaa ya kukosekana kwa  maji au kuondoka kwa udhuru pia,  ama ikiwa  uta kata tamaa ya kuwa udhuru hauta ondoka, wakati huo hakuta kuwa na tatizo  ikiwa utafanya haraka kufanya tayammam, na ikiwa utasali kwa kufanya tayammam, kauli iliyo adhahiri ni kuwa si wajibu kuirudia sala hiyo hata kama udhuru huo utatoweka kabla ya wakati wa sala hiyo kumalizika.                                          

            MAS’ALA: Ikiwa mtu atafanya tayammam  kwa ajili ya sala ya faradhi au sunna, kutokana na udhuru  na akaisali sala hiyo, kisha  ukaingia  wakati wa sala nyingine, ikiwa hatakuwa na matarajio ya kutoweka kwa udhuru huo  na kuweza kujitwaharisha kwa  maji, itajuzu kwake  kufanya haraka kuisali sala hiyo katika wakati ulio mpana, na si wajibu kwake kuirudia  ikiwa udhuru utatoweka baada ya hapo, ama ikiwa kuna matarajio ya kuondoka kwa udhuru, kauli iliyo ahwat ni kuwa ni lazima kuchelewa  kufanya hivyo.

MAS’ALA: Ikiwa  yatapatikana maji  katikati ya sala ya faradhi au ya sunna, ataendelea na sala yake, na kauli yenye nguvu inasema  kuwa  sala yake itakuwa sahihi, japo kuwa kauli ya ahwat inasema  ni bora zaidi kuirudia sala hiyo baada ya kujitwaharisha  kwa maji ikiwa maji hayo yamepatikana  kabla ya rukuu, bali hata baada yake  maadamu rakaa ya pili haijamalizikia.                                  

MS’ALA:  Ikiwa mtu mwenye hadathi kubwa  atafanya tayammam, kama mtu mwenye janaba hedhi na mengineyo kutokana na udhuru,  kisha akatokwa na hadathi ndogo, tayammam yake haitabatilika, ikiwa itawezekana atafanya tayammam, la sivyo atafanya tayammam badala ya udhu,  na kauli iliyo ahwat ni kukusanya kati ya kutaymmam badala ya ghusli na kutawadha  ikiwa itawezekana, na  atafanya tayammam kwa makusudio ya kuodoa dhimma  ikiwa haikuwezekana kutawadha.

MAS’ALA: Haijuzu kumwaga maji yatoshayo kwa udhu, au ghusli baada ya kuingia wakati wa sala, bali kutokana na kauli iliyo ahwat ni kuwa  haijuzu kumwaga maji kabla ya kuingia wakati wa sala ikiwa utafahamu ya kuwa hayatapatikana  baada ya kuingia wakati wa sala, na ikiwa  utakusudia kuyamwaga maji hayo itawajibika kufanya tayammam ikiwa pia hakuna matarajio ya kuyapata maji hayo na utasali  kwa kutayammam,na ikiwa utaweza kuyapata maji baada ya kusali sala hiyo kwa tayammam haitawajibika kuirudia  wala kuilipa sala hiyo kutokana na kauli iliyo adh’har (iliyo dhahiri), na ikiwa utakuwa na udhu  haitajuzu kuutengua  au kuubatilisha  udhu huo kutokana na kauli iliyo ahwat ikiwa utafahamu ya kuwa hakuna maji au ikiwa utakata tama juu ya kupatikana maji, na ikiwa  uta ubatilisha udhu katika hali kama hii itakubidi kufanya tayammam na kusali na haita kulazimu kuirudia kama tulivyo tangulia kusema.

MAS’ALA: Ni sheria kutumia tayammam kwa kila jambo ambalo ni sharti kuwa na twahara katika kutekelezwa kwake, kama sala ya faradhi na sunna,  vile vile kila jambo ambalo halitimii isipokuwa  kwa kuwa na twahara ikiwa jambo hilo limeamrishwa na hupelekea kwenye ukamilifu, kama kusoma qur’ani, na kukaa msikitini  na mfano wa hayo, na kutayammam kwa ajili ya kuwa na twahara tu kuna ish’kaal,  na kauli iliyo dhahiri ni kuwa inajuzu  kutayammam kwa ajili ya kutenda  mambo yaliyo haramishwa kwa mwenye hadathi hata kama hakuamriswa kufanya hivyo, (kama kugusa qur’ani na kugusa jina la Mwenyezi Miungu mtukufu) kama tulivyo elezea katika malengo ya udhu.

MAS’ALA: Ikiwa mtu mwenye hadathi atafanya tayammam kwa jili ya lengo fulani, itajuzi kuitumia tayammam hiyo kwa lengo lingine lolote na jambo hilo litasihi, kwa mfano ikiwa atafanya tayammam kwa ajili ya sala itajuzu  kuingia msikitini kwa tayammam hiyo na sehemu za kufanyia ziara kama kwenye makaburi ya maimam na mengineyo kati ya mambo ambayo ukamilifu wake au kusihi kwake au kujuzu kwake ni sharti kujitwahirisha kwa maji. Na ikiwa  atafanya tayammam kutokana na ufinyu wa wakati, itajuzu kusali kwa tayammam hiyo na itajuzu  kuitumia tayammam hiyo kwa lengo lingine kama kugusa qur’ani na kusoma suratul azaaim na mfano wa hayo.

MAS’ALA: Tayammam hutenguka na kubatilika pale tu kunapo kuwa na ewezekano wa kutumia maji hata kama kutapatikana udhuru baada ya hapo, isipokuwa ikiwa uwezekano huo utamkuta  katikati ya sala wakati huo tayammam yake haitabatilika kama ilivyo tangulia. Na  mtualie fanya tayammam mbili –kwa  ihtiyaat- moja badala ya udhu na nyingine badala ya ghusli ikiwa atapata maji yamtoshayo kwa  kutawadhia, tayammam yake iliyo kuwa badala ya udhu itabatilika, na ikiwa atapata maji yamtoshayo kwa ajili ya ghusli,  tayammam zote mbili zitabatilika  sawa maji hayo yaweyatatosha kwa udhu na ghusli kwa pamoja au laa, na wakati huo atafanya ghusli tu. Na hali hii itatumika kwa mtu asie na istihadha mutawassit,  ama mwenye istihadha mutawassit yeye katika hali ya kwanza na katika sura ya mwisho atafanya ihtiyaat kwa kufanya ghusli  na kutawadha, na katika hali ya pili ata tawadha na kufanya tayammam badala ya ghusli kutokana  na  kauli ya ahwat, kutokana na hayo inadhihiri hukumu  wakati  atakapo kosa maji yatoshayo kwa ghusli  kabla ya kuyatumia na kwamba hukumu yake ni sawa na  hukumu ya kabla ya kutayammam.

MAS’ALA: Ikiwa mtu atatia shaka ya kuwa kuna kizuwizi katika baadhi ya viungo vya kufanyia tayammam au laa, hali yake ni sawa na hali ya udhu na ghusli, kwani ni wajibu kufanya uchunguzi  hadi kupata yakini au matumaini ya kuto kuwepo kizuwizi.