rudi maktaba >Maadili >Yaliyomo >

SHEREHE ZA MAULIDI

Muandishi: Abdillahi nassir

Maulidi ni Kiswahili cha neno la Kiarabu, mawlid. Neno hili lina maana ya "mazazi" au "kuzaliwa kwa…" (birthday). Kwa kawaida, linapotumiwa na Waislamu, huwa na maana ya siku aliyozaliwa Mtume Muhammad (s.a.w.w.), au hafla ya kuisherehekea siku hiyo.

Waislamu wa ulimwengu mzima, ifikapo tarehe 12 ya Mfungo Sita (Rabiul Awwal), husoma maulidi na kuisherehekea siku hiyo kwa furaha kubwa. Sherehe hizo, kwa dasturi, haziishii tarehe hiyo tu, bali huendelea hata kwa miezi miwili mitatu baada ya hapo. Hili huwa ni kwa sababu ya Waislamu wa kila nyumba, kila mtaa, kila mji na kila nchi kutaka kushiriki katika sherehe hizo na kupata baraka zake. Vile vile huwapa Waislamu nafasi ya kutembeleana na kushirikiana katika sherehe hizo - jambo ambalo lisingewezekana lau watu wote wangeliamua kuzifanya sherehe hizo siku hiyo hiyo moja tu.

Kwa nini kusoma maulidi?

Waislamu husoma maulidi kwa sababu mbalimbali. Kati ya hizo ni:

kuikumbuka na kuitukuza siku aliyozaliwa mbora wa viumbe vyote, aliyetutoa vizani na kututia kwenye nuru;

ni njia moja ya kutoa shukrani zetu kwa neema hiyo;

katika sherehe hizo, hupatikana fursa ya kukumbushana maisha ya bwana mkubwa huyo na mafunzo yake;

hupatikana fursa ya Waislamu wa madhihabi na mataifa mbalimbali kushirikiana na kuziweka kando hitilafu zao; na

mikusanyiko hiyo huleta athari kwa wasio Waislamu ya kuupenda Uislamu, na hata kusilimu.

Wanaopinga na sababu zao

Lakini, hata hivyo, kuna baadhi ya Waislamu -- japokuwa wao si wengi kama wanaoyasoma -- ambao hupinga kusomwa maulidi; na hutoa sababu zao. Kati ya sababu hizo ni:

maulidi hayakuwako zama za Mtume Muhammad (s.a.w.w.). Basi kwa nini yazuliwe sasa?

hayakusomwa na maswahaba wala waandamizi wao. Kama kweli yangelikuwa ni sawa kuyasoma, bila shaka mabwana wakubwa hao wangelikuwa ni wa mbele kufanya hivyo;

kuweka ada ya kusoma maulidi ni kuigiza Wakristo walioweka siku ya Krismasi; na Mwislamu haruhusiwi kufanya hivyo;

kwenye sherehe za maulidi hufanywa baadhi ya mambo ambayo ni ya munkar (yanayochukiza, bali ni haramu kamwe, katika sharia ya Kiislamu); na

hakuna ushahidi wowote, wa Qur'ani wala Hadithi za Mtume Muhammad (s.a.w.w.), unaothubutisha usawa wa kuyasoma maulidi, sikwambii kuyatilia nguvu.

Kwa nguvu ya hujja hizo, mara nyingi viongozi wa wanaopinga maulidi huwaonyesha wafuasi wao kuwa wale wanaosoma maulidi ni watu waliopotea kwa "kuzua" mambo yasiyo na msingi katika dini yetu hii. Jambo hili limeleta mchafuko -- unaofufuka aghalabu kila ifikiapo miezi ya kusoma maulidi -- ambao unahatarisha umoja na masikizano, sio baina ya Waislamu wa madhihabi mbalimbali peke yao, bali hata wale wa madhihabi mamoja!

Mchafuko huu huzidi kukua kwa sababu ya lugha kali inayotumiwa na pande zote mbili -- za wanaounga na wanaopinga maulidi -- katika kutetea misimamo yao; na hilo haliwezi kusaidia katika kutatua usawa uko wapi. Liwezalo kutatua hitilafu hii ni kuijadili ki-ilimu na kwa lugha nzuri ya kuhishimiana. Na hilo ndilo nililokusudia kulifanya, kuanzia makala yanayofuatia haya, Inshallah.